Jumamosi, 9 Agosti 2014

AZIMIO LA ARUSHA LITAREJESHA MAADILI NCHINI TANZANIA


 Dk. Camillus Kassala mtoa mada

Na Elias Mhegera
Imetabiriwa kwamba mara ifikapo mwaka 2017 Tanzania itarejea katika kulitambua rasmi Azimio la Arusha bila kujali rais atatoka katika  chama tawala Chama  Cha Mapinduzi (CCM) au upinzani.
Utabiri huo ulifanywa na mwanazuoni maarufu katika masuala ya uchumi, siasa na falsafa Dk. Camillus Kassala  alipokuwa akitoa mada kuhusu uchumi wa soko unaozingatia mahitaji ya jamii.
Alikuwa akitoa mada kwa wanafunzi wa chuo cha Mwalimu Nyerere Kivukoni waliokuwa katika maandalizi ya ziara ya mafunzo nchini Ujerumani. Siku ya Ijumaa tarehe moja, Agosti, 2014.
Wanafunzi kutoka chuo hicho na wale wa Ujerumani wamekuwa katika ushirikiano wa kutembeleana wakitumia kauli mbiu ya Pamoja. Miongoni mwa mambo wanayojifunza katika ziara hizo ni uongozi na maadili yake.
Katika semina hiyo ya maandalizi iliyoandaliwa na Pamoja kwa ushirikiano na shirika la - The Konrad-Adenauer-Stiftung (KAS). Miongoni mwa masuala yaliyozungumziwa ni undeshaji wa uchumi katika muktadha wa soko huria lenye kujali ustawi wa jamii.  
Akiongea kwa kujiamini Dk. Kassala alisema kwamba uchumi wa soko huria usiozingatia jamii ndiyo umeifikisha Tanzania hapa ilipo kwa sasa ambapo kuna tofauti kubwa ya kipato kati ya watu wachache walionacho na wananchi walio wengi wasionacho.
Mada tajwa ililenga katika kuangalia wajibu wa serikali katika kuhakikisha usalama kwa rika la vijana, na kulinda utamaduni wao bila kuathiriwa na mfumo wa utandawazi.




























                                                   Bi Debora Maleyek akiuliza swali 

Katika mijadala iliyoendeshwa katika mdahalo huo ilijidhihirisha kwamba vijana wengi 

wanakutana na changamoto kubwa mara wanapohitimu masomo yao kwa sababu ni wachache wanaopata nafasi za kuendelea na masomo ya juu huku wengi wao wakiwa hawana ujuzi wowote wa kujiajiri au kukabiliana na changamoto za maisha.
Dk. Kassala anasema kwanza tatizo la Tanzania siyo uwepo wa sera bali ni sera zilizopo na zimekosa watekelezaji wake. Anasema kitendo cha vijana wengi kuyakimbia maeneo yao ya asili na kujitafutia ujira wao katika miji mikubwa ni kiashiria cha kukata tamaa kwa tabaka hilo muhimu katika jamii.
Anasema vijana ambao bado damu zao zinachemka huwa wakorofi pale wanapoburuzwa bila kuambiwa ni wapi wanakopelekwa. Na hasa inapotokea kwamba hawahusishwi katika maaamuzi ya namna ya kuendeshja uchumi.
Dk Kassala anakumbusha kwamba vijana hawajawahi kuhusishwa katika mjadala wa namna ya kujitafutia mitaji, wala ubinafsishaji, mizunguko ya pesa katika uchumi na namna mtu mmoja mmoja anavyoweza kushiriki katika uchumi wa taifa.
Anasema Tanzania imejiwekea malengo kwamba itakuwa na uchumi wa daraja la kati mara ifikapo mwaka 2025 lakini haoni dalili zozote zinazoashiria maono hayo. Kwa mfano, ni njia gani zitatumika, katika ngazi gani? na wahusika wakuu ni akina nani.
Mwanazuoni huyo anasema kwamba maono hayo yanatakiwa kuwamo katika bajeti ya taifa ya sasa, namna ya kuanzisha ajira, namna ya kukuza sekta binafsi, namna ya kukuza kilimo ambacho ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wa taifa hili, na namna ya uendeshaji wa taasisi za umma.
Mtaalamu huyu anasema kwa kawaida jamii imekuwa na tabia ya kutupa lawama kwa vijana bila kuangalia kwamba kabla ya kukengeuka kwao walikuwa wamejengewa mfumo gani wa kimaadili ambao hautoi uhakika wa usalama kwao na kutoa uhakika wa maisha yao ya baadaye.
Dk. Kassala anasema vijana wengi huwa na matumaini ya kupata mafanikio kwa haraka na hilo likishindikina ndipo vijana hujiingiza katika mambo maovu. Kimsingi anasema vijana wanatakiwa kuoneshwa kwamba wanakumbukwa na watawala.
Alisema njia nyingine kwa viongozi ni kujenga mazingira ya kukubalika ni kuzingatia maadili, uhuru, na kujiamini kunakoweza kuwafanya wajitegemee hata pale wanapokosa ajira.
Anasema Mwl. Nyerere alipotangaza Azimio la Arusha alilenga kuleta amani, kulinda mali binafsi lakini pia kuweka uwazi na uwajibikaji katika kusimamia ugavi wa raslimali za umma. Anasema kimsingi serikali inatakiwa kujenga mifumo ya kuwalinda wananchi wake ambao ndiyo wazilishaji kiasi kwamba hata wakipata hasara basi waweze kufidiwa.
“Wananchi ni lazima walindwe pale wanapopata hasara, inabidi tuthamini utu kabla ya faida,” anasema kukosa utu kwa tabaka la chini ndiko kumesababisha chuki kutokana na watawala kuwajali wawekezaji badala ya Watanzania.
Mtaalamu huyo anainisha mambo kadhaa ambayo ya naweza kuisadia Tanzania. Kwanza ni utu, kuheshimu maadili, na tamaduni za Kiafrika. Anasema serikali inatakiwa kuondokana na dhana ya kuthamini pesa kuliko utu.                                            

             Bw Deus Fidelis akichangia katika mada hiyo 
Vile vile anashauri kwamba jamii iepukane na tabia ya kuthamini amali za kimagharibi na kuwasahau Watanzania na tamaduni zao. Anashauri kwamba teknolojia mpya kama ipad na mambo mengine yanayohusisha mitandao ya intaneti yalenge kwenye mambo ya kujenga na wala siyo kuupotosha umma.
Nao vijana walipata nafasi ya kutoa michango ya mawazo na kuuliza maswali na hali ilikuwa kama ifutavyo: Bi Deborah Maleyek alitaka kujua Azimio la Arusha ni nini kwa nini lilishindwa kufanya kazi endelevu.
Akijibu hoja hiyo Dk. Kassala anasema kwamba azimio hilo lilikuja kama jibu muafaka katika kipindi cha mwanzo wa uhuru wa nchi hii baada ya kutokea  misigano ya kifikra ya namna ya kuendesha utawala wa nchi hii.
 Anasema wapo waliotaka kupata mafao kama waliyopata watawala wa kikoloni kabla ya uhuru huku wengine wakiona kwamba kufanya hivyo ni kuwadhulumu wanyonge.
“Nyerere aliona kwamba wenzake wanatamaa ya kuvaa viatu vya wazungu na akatafuta uhalali wa kufanya hivyo na azimio hilo likawa ndiyo msingi wa kuondokana na wale wasiotaka kujinyima kwa ajili ya walio wengi” anasema.  
Kassala anasema kwamba Mwl. Nyerere alihakikisha kwamba Watanzania wanapata elimu ya bure katika ngazi zote na ndiyo maana kulikuwapo na elimu ya watu wazima. Msingi wa kufanya hivyo ulitokana na imani kwamba uelewa utasaidia katika maendeleo ya kiuchumi.
Lakini anawaeleimisha vijana kwamba miongoni mwa mambo muhimu aliyoyafanya Mwl. Nyerere ni kuhakikisha kwamba kila Mtanzania anapata ardhi ambayo inasimamiwa na rais wa nchi.
Akijibu sehemu ya pili ya swali hilo msomi huyo anasema kwamba siyo kwamba Azimio la Arusha lilishindwa bali mapokeo ya siasa za kiliberali yalipongia nchini na katika hali ya kurekebisha uchumi baadhi ya watu wenye ushawishi waliweweseka, na kupotoka kiasi cha kushindwa kuona mazuri ya azimio hilo.
Naye mwanachuo Kamala Dickson aliomba kufahamu iwapo kufufuliwa kwa Azimio la Arusha ni jambo linalowezekana katika hali ambapo uchumi wa soko ndiyo unaotawala.
Akajibu swali hilo Dk Kassala anasema hilo ni jambo linalowezekana kwa sababu Tanzania inaendeshwa katika mfumo wa uchumi mchanganyiko uanaozingatia mahitaji ya kibinadamu.


Kwa upande wake Semainda Fredrick alitaka kujua matokea hasi ya mfumo wa soko ambayo labda Mwl Nyerere aliyahofia katika enzi za utawala wake. Akijibu swali hilo  Dk Kassala anasema kwamba hakuna mfumo usiokuwa na hitlafu zake lakini kilichokosena ni udhibiti wa serikali baada ya Mwl. Nyerere kustaafu.
Kwa maana hiyo anasema kwamba uchumi wa kijamaa bado unakubalika sehemu nyingi mpaka sasa isipokuwa udhibiti wa serikali hupishana sehemu moja hadi nyingine.
“Nimetembea hadi Venezuela nikashangaa kuona kwamba chini ya utawaka wa marehemu Hugo Chavez Azimio la Arusha lilitafsiriwa kwa Kireno ili kila mmoja alifahamu vilivyo kwa hiyo udhaifu haukuwa kwa nadharia yenyewe bali katika utekelezaji wake.
Lewis Mmbando anauliza iwapo kiwango cha maendeleo ya sayansi na teknolojia kinaruhusu mfumo wa soko huru kufanya kazi vizuri. Anasema jambo la msingi ni kukubalika kwa dhana zenyewe kwa Watanzania. 
                                                                                                                                      Bi. Agnes Kessy akiuliza swali

4.     
Naye Cacilie Radert –akiwakilisha taasisi ya KAS anasema kwamba historia ya Wajerumani iliwasidia sana katika kuleta maendeleo ya kiuchumi kwa sababu waliona wana wajibu wa kulinda hadhi ya taifa lao katika misingi ya uzalendo.
Anasema kitendo cha Ujerumani kutengwa baada ya vita ya pili ya dunia kiliwafanya wananchi wa taifa hilo kujiuliza wao wanaweza kuifanyia nini nchi yao. Hata hivyo anasema kwamba changamoto kubwa iliyokuwapo  ni kwamba kulikuwa na uhaba wa fedha za kuyasaidia makundi yasiyozalisha likiwamo kundi la wazee.
Vile vile Ujerumani ilipata kazi kubwa ya kupambana na wapinzani wake wa nje lakini pia namna ya kurejesha nguvu ya taifa katika uzalishaji.
1
3.  

Jumamosi, 19 Julai 2014



Mkuu wa Jeshi la Polisi Mstaafu Said Mwema
JESHI LA POLISI WAZINGATIE MAADILI WARUDHISHE IMANI YA WANANCHI

Novemba 04, 2007 Mtanzania Jumapili

Na Elias Mhegera
Siku ya Jumamosi tarehe 20 Oktoba mwaka huu wananchi wa kijiji cha Ilongero mkoani Singida walijichukulia sheria mikononi, wakavunja kituo cha polisi kwa lengo la kumsulubu mtuhumiwa wa ubakaji na mauaji aitwaye Mile ambaye hatimaye wananchi hao walimuua.

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Inspekta Jenerali wa Polisi Said Mwema ametoa tamko kali kukemea kitendo hicho cha wananchi hao, nami nimeona ni muhimu kulizungumzia suala hilo.

Katika vipindi vingi vya matukio katika redio zetu na hata katika habari zitolewazo magazetini matukio ya ukatili yamekuwa yakijitokeza kwa kiwango kikubwa na cha kutisha.

Mara kadhaa kumekuwapo na ripoti zenye kuleta simanzi kwa sababu ya watu kufanyiana vitendo viovu vya ukatili, kuuana na mambo kadhaa yasiyopendeza ili mradi kila jambo baya la aina hiyo hutokana na utovu wa maaadili kwa namna moja au nyingine.

Nimeshawishika kuandika makala hii ili nitoe mchango wangu mdogo katika jamii katika kuimarisha amani na utulivu.

Kwa namna yoyote ile katika dunia ya waungwana tunayojitahidi kuijenga hatuwezi kuruhusu kitendo kama kile cha wananchi wa Ilongero.

Lakini kwa upande mwingine napenda kutanabahisha kwamba tukio la Ilongero linaonyesha kwamba kulikuwa na mazingira ya uzembe kwa mamlaka husika ambayo hatimaye yalisababisha wananchi wakaamua kujichukulia sheria mikononi mwao kwani mhusika alikuwa amewahi kufikishwa kituoni hapo mara kadhaa na kuachiliwa huru katika mazingira ambayo yaliwatatiza wananchi wa kijiji hicho.

Lakini tukio la Ilongero linaashiria kwamba kama mamlaka husika hazitachukua hatua madhubuti katika muda muafaka ipo hatari ya wananchi kuendelea kujichukulia sheria mikononi.

Ni mara kadhaa wananchi wamekuwa wakitoa malalamiko kwamba wapo baadhi ya wahalifu ambao mara wafikishwapo katika vyombo vya dola kama vile Jeshi la Polisi na mahakamani huachiliwa huru kwa madai kwamba hapakuwa na ushahidi wa kutosha kuweza kuwaweka hatiani watuhumiwa hao.

Athari za muda mrefu ni kwamba watu hao hurudi mitaani wakaendeleza uovu wao na hata wakati mwingine huwatambia wananchi kwamba wao kamwe hawawezi kuguswa na dola.

Nashawishika kuamini kwamba upo ufa mkubwa katika utendaji wa vyombo vyetu vya dola ambao usipozibwa matukio kama hilo la Ilongero yataendelea kujitokeza mara kwa mara.

Sehemu kubwa ya matukio ya namna ile yamechangiwa na utovu wa maadili si kwa wanajamii pekee bali hata kwa watendaji katika vyombo vya dola ambao hukubali kupokea hongo na kuwaachia huru wahalifu.

Yapo masuala kadhaa yanayolalamikiwa mara kwa mara na wananchi kuhusiana na kukengeuka kwa maadili ya kitaaluma kwa baadhi ya askari katika Jeshi la Polisi kwa mfano tukio la hivi karibuni la askari polisi kumuibia mwenzake silaha akiwa lindoni, ama hata baadhi ya askari polisi kuwafichiua watoa habari (whistleblowers), haya ni mambo yanayolivunjia heshima jeshi hilo katika jamii.

Kwa hali yoyote ile iwapo Jeshi la Polisi au hata mahakama zetu hazitarekebisha baadhi ya mienendo na kukidhi matakwa na mahitaji basi tutaendelea kushuhudia vitendo vya uvunjaji wa sheria kwa wananchi kujichukulia sheria mikononi kama walivyofanya wananchi wa Ilongero hivi karibuni. Lakini tukio hilo ni muendelezo tu wa matukio ya aina hiyo ambapo mara kadhaa wananchi hujichukulia sheria mikononi na kuwachoma watu moto kwa kuwavalisha watu matairi na baadaye kuwachoma moto kwa kutumia petrol mafuta ya taa n.k. 

Ndiyo maana katika makala zangu kadhaa nimekuwea nikisisitiza kwamba iwapo mamlaka halali zitashindwa kutimiza wajibu wao basi walizi wa maadili watajitokeza na kuifanya kazi hiyo.

Walinzi hao wa maadili ninaowazungumzia hawaishi katika ombwe (vacuum) bali ni sisi wenyewe pale inapofikia kwamba tumechoshwa na uovu tukaamua kuirudisha jamii katika mstari unaostahili. Siku zote wanadamu wanapofikia hatua hiyo ni kwa sababu wanakuwa wamekatishwa tamaa na mifumo halali inayotakiwa kushughulikia masuala hayo.

Mtuhumiwa aliyeuawa aliyefahamika kwa jina la Mile alikuwa na uzoefu wa uhalifu. Kulingana na maelezo ya wananchi wa Ilongero waliyoyatoa kwa Mbunge wa Jimbo la Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu mtuhumiwa huyo aliwahi kufikishwha kituoni hapo mara tatu kwa tuhuma mbalimbali na mara ya mwisho alitoroka baada ya kuvunja dirisha kituoni hapo.

Wananchi hao walidai kwamba mtuhumiwa Mile amewahi kuhusika katika vitendo vya ubakaji kwa zaidi ya wanawake sita kijijini akiwemo mama yake mzazi! Kabla ya kuwabaka watoto wa familia moja hadi kuwaua. Inadaiwa pia mtuhumiwa huyo wa ubakaji pia alimbaka mwalimu wa wanafunzi hao katika shule ya msingi Mlama.

Ilidaiwa kwamba akina mama waliobakwa waliogopa kutoa taarifa kwa kuona kwamba jambo hilo lingewafedhehesha katika jamii yao. Ukimya wa akina mama hao ndio uliompa kiburi mtuhumiwa huyo wa ubakaji akashirikiana na mtuhumiwa mwenzake aitwaye Hamisi Juma na wakatenda tendo hilo la kinyama tarehe 14 ya mwezi Oktoba hadi kusababisha vifo vya mabinti hao.

Hasira na uchungu wa kupoteza watoto wao wapendwa viliwafanya wananchi hao wa Ilongero wapoteze subira na hatimaye wakaamua kuikamilisha kazi ambayo tayari waliona isingefanywa katika kiwango walichoona wao kinastahili kwa wauaji hao.

Kwa sasa baadhi wa wanakijiji hao akiwemo mwenyekiti wao Issa Swedy wameshikiliwa na dola kutokana na kujichukulia sheria mikononi mwao na kuwaua watuhumiwa wao.

Hata hivyo mbunge wao Nyalandu ameliomba Jeshi la Polisi pamoja na kuwakamata wanakijiji hao nalo kwa upande wake liwajibike kwa kutoa maelezo ya kina juu ya kutoroka na kuachiwa mara kwa mara kwa mtuhumiwa huyo. Ni dhahiri hapo kuna tatizo kubwa ambalo sisi kama wanajamii inatubidi tukune vichwa na kuangalia namna ya kuyazuia matukio ya namna ile yasije tokea tena katika jamii zetu.

Labda tunaweza kuanza kwa kujifanyia tathmini ya viwango vyetu vya maadili na kutafuta jinsi ya kurekebisha mapungufu tuliyonayo.

Maadili ni mfumo wa uhalalishaji wa matendo mema na kwa upande mwingine kuyakataa matendo yote mabaya. Kwa kifupi maadili ni dhana pana inayohusu uchanganuaji wa mema na mabaya.

Labda tatizo lililopo ni kudhania kwamba maadili ni yale tu yaliyoandikwa katika vitabu vya kigeni na kwamba sisi waafrika hatuna maadili yetu au labda hatujawahi kuwa nayo isipokuwa yale yaliyoletwa na wakoloni, wamisionari wafanyabiashara wa kiarabu walioleta uislamu Afrika na mambo kama hayo.

Ni muhimu tukafahamu kwamba nasi tuna maadili yetu ambayo yamejikita katika mila, desturi na tamaduni zetu. Kwa mfano kile kinachoitwa miiko ni msingi thabiti wa maadili ya muafrika, kwa maana hiyo kwa sababu miiko imekuwepo siku zote katika jamii zetu, basi kumbe inadhihirisha kwamba maadili yetu yamekuwepo pia tokea enzi za mababu zetu.

Matukio ya watu kuuana wakigombea mwanamke, au kufumaniana ugoni, kuchomeana ndani ya nyumba, kuwaadhibu wasiostahili, kwenda kinyume cha taratibu za jamii, visasi kuwekeana vikwazo, ubaguzi wa rangi, unyanyapaa, kuathiriana kisaikolojia, kughushi malipo, kuwaingiza wenzetu katika mikataba ya uongo, kutumia madaraka vibaya yote haya ni utovu wa maadili ambao huchangia katika matukio ya kudhuriana kila uchao.

Lakini matukio yote yaliyotajwa hapo juu yanaweza kuzuilika iwapo tutazingatia maadili ambayo tunarithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kabla hata ya kufikiria kwenda darasani kwa ajili ya somo la maadili.

Katika mila zetu za kiafrika maadili yalitokana na umoja wa kifamilia kwa sababu koo mbalimbali ziliishi katika eneo moja katika mfumo wa ukoo, koo kadhaa na hatimaye kijiji. Kwa maana hiyo kijiji kimoja au vijiji kadhaa vilitokana na koo zenye kushabihiana katika lugha (kabila), mila na desturi, na kwa maana hiyo maadili yao yalifanana.

Maadili yenyewe yalirithishwa kwa njia ya imani, sherehe za kimila, nyimbo hadithi na simulizi mbalimbali. Kwa ujumla maadili yaliyokuwepo yalitegemeana sana na tafsiri ya mazingira na matukio yaliyojitokeza katika jamii husika. Kwa mfano kuzaliwa kwa mtoto, maradhi, vifo, mazishi, n.k.

Kila jamii ililinda maadili yake kutegemeana na shughuli zilizoizunguka jamii hiyo kama vile kilimo, ufugaji, uvuvi, uhunzi n.k. Kwa maana hiyo hata miungu walioabudiwa walitokana na mazingira husika. Kwa maana hiyo kulikuwa na miungu wa mvua, mavuno, tiba, amani, n.k.

Maadili hayo ya kiafrika ndiyo yaliyowatuma waafrika wachague mlo wa aina fulani, makazi yao, mavazi, namna ya kufunga ndoa kuwapokea watoto wanaozaliwa, kuzikana na namna ya kukabiliana na majanga mbalimbali katika jamii husika.

Kimsingi katika maadili ya kiafrika hakuna eneo lililokuwa limetelekezwa kwani kila jambo lilikuwa na majibu yake tayari tayari. Kwa maana hiyo watu walikuwa wamejiwekea tayari utaratibu wa kukabiliana na majanga yoyote ambayo yangejitokeza mbele yao.

Kulikuwepo na taratibu za kurekebisha ndoa, mahusiano ya kawaida katika jamii namna ya kukabiliana na misukosuko mbalimbali ya kimaisha, kuvumbua dawa, matumizi ya ardhi, matumizi ya alama na ishara mbalimbali, masuala ya posa na utoaji wa mahari n.k. Mambo yote hayo yalilenga katika utoaji wa maamuzi sahihi mara yanapojitokeza mapungufu fulani.

Lakini pia ni katika maadili hayo hayo ndipo ulipopatikana mgawanyo wa majukumu mbalimbali ya kijamii na kazi. Kulikuwepo na misemo mbalimbali na tungo zenye ujumbe murua katika kila tukio husika.

Kwa bahati mbaya imani za kishirikina pia zilitawala sana katika jamii zetu na ndiyo maana kila jamii ilikuwa na madawa kwa ajili ya kujilinda na maadui zao.

Kinachojitokeza katika matukio ya sasa ambayo yanaripotiwa na vyombo vya habari kila siku ni kupotea dira au muelekeo wa maadili yetu ambako kumechangiwa kwa kiwango fulani na kuhama hama kwa ajili ya kutafuta maslahi.

Kuja kwa ukoloni na dini za kigeni ambazo zote zimeyakandamiza maadili yetu kwamba ni ya kishenzi na kwa maana hiyo mvurugiko huo ndiyo unaochangia katika matukio mabaya yanayosababisha watu wachinjane kama kuku kila uchao.

Kwa hiyo ni lazima tufahamu kwamba kuna ombwe (vacuum) kati ya maadili yetu na yale ya kigeni au wakati mwingine ni kwa sababu watu wa makabila mbalimbali wanafunga ndoa au hata kuingiliana kijamii bila kufahamiana vizuri kwanza.

Kwa hiyo kuna umuhimu wa kuwianisha maadili yetu (dialogue) ili kuondoa migogoro isiyokwisha na pia ili tupate dira moja inayokidhi mahitaji yetu sote kwa pamoja.

Si lengo la makala hii kuzungumzia maadili katika kila taaluma au kuingia kwa undani sana juu ya dhana ya uadilifu, bali lengo ni kuyazungumzia maadili katika ujumla wake na kuangalia vyanzo vya matatizo katika jamii zetu na hatimaye kutoa ushauri wa nini kifanyike ili kurekebisha hali iliyopo kwa sasa, yaani kilio cha utovu wa maadili.

Ni vyema basi tukagusia maadili kama yanavyotazamwa na wenzetu wageni: wao wameyagawa katika sehemu kuu tatu; metaethics, normative ethics, na applied ethics. Makala hii imelenga katika kuyachanganua maadili haya kama yanavyotazamwa na wenzetu na kutoa tafsiri yake katika mazingira yetu.

Metaethics ni dhana ya kimaadili inayo chunguza vyanzo vya maadili, maana zake, dhana ya ukweli na utashi wa Mungu katika yale tuyatendayo. Normative ethics ni dhana inayozungumzia matendo zaidi na pia namna ya kurekebisha matendo hayo na kutoa mwelekeo mzuri zaidi.

Kwa upande mwingine applied ethics ni dhana inayozungumzia au kuangalia, kuchunguza, au kupima matendo yasiyo ya kawaida katika maisha ya jamii zetu. Kwa mfano utoaji wa mimba, ushoga, na usagaji, masuala ya mazingira kama vile ukataji wa miti ovyo, kuchoma misitu, adhabu ya kifo n.k.

Baada ya kujadili maadili ni nini, na kuwianisha maadili yetu ya kiafrika na yale ya kigeni, ni vyema sasa tukajadili ni kwa nini hutokea watu wakakiuka maadili japo wakati mwingine wanayafahamu, na pia wanazijua fika athari za kukiuka maadili hayo.

MAZINGIRA YA MAAMUZI

Japo hakuna dhambi inayohalalishwa kwa namna yoyote ile lakini hujitokeza kwamba binadamu akayumbishwa kisaikolojia na kujikuta katika mazingira yanayoweza kumfanya akiuke maadili. Tukio la mauaji la Ilongero linaweza kuhusishwa na suala la mazingira ya maamuzi yaani uchungu wa kupoteza watoto na hasira kali ya wananchi

Kwa mfano binti aliyemaliza darasa la saba akajikuta haendelezwi kwa njia yoyote ile, hapati taaluma, wala ajira rasmi ni rahisi sana kwake kuhalalisha kujiingiza katika biashara mbaya ya ukahaba. Japo binti huyo anaweza asifurahishwe sana na uamuzi wake huo lakini anaweza kuwa na kisingizio kwamba hakuwa na njia nyingine mbadala ya kujikimu katiaka maisha yake.

UBINAFSI
Wapo watu wengi katika jamii zetu waliotawaliwa na ubinafsi bila kufahamu kwamba kufanya hivyo ni kukiuka maadili. Hii ni kwa sababu mara nyingi watu wa aina hii hujitahidi kukwamisha mambo ya wenzao kila wanapoona kuna dalili za mafanikio fulani, watu wa aina hii hudhania kwamba ni wao pekee wanaostahili kupata. 
  
Kama hiyo haitoshi kundi la watu wa aina hii husumbuliwa sana na ghiliba na roho za kwa nini kwa wale wenye upeo mkubwa au wenye tabia ya kujihangaisha katika kutafuta maendeleo (aggressive). Watu wa aina hii hawakawii kuwadhuru wenzao pale wanapoona kuna dalili njema mbele yao.

Katika kundi la watu wenye tabia kama hizi ndiyo tunasikia vifo vya mara kwa mara kutokana na kutaka kuzibiana ridhiki. Yapo mambo kadhaa yanayoambatana na ubinafsi kama vile kuchongeana na hata kulishana sumu. Mambo ya aina hii hutokea sana kwa wafanyabiashara, wanasiasa na viongozi katika taasisi mbalimbali wanaotaka kutukuzwa.

HASIRA NA PAPARA
Kuna nyakati ambapo watu hukiuka maadili kwa sababu ya kulipiza visasi, na maamuzi ya pupa. Kwa mfano wapo akina mama ambao huamua kuanzisha mahusiano na rafiki za waume zao pale wanapojiona kwamba hawakutendewa haki lakini mara nyingi maamuzi kama hayo huwashushia heshima zao mbele ya jamii badala ya kutatua tatizo linalowakabili.
Hali ya visasi vya namna hiyo inaweza pia kufanywa na mwanaume dhidi ya mke wake au hata kwa wachumba ambao bado hawajafunga ndoa. Wakati mwingine visasi vya namna hii huchangiwa sana na  wazazi, mawifi mashemeji na marafiki wa karibu wa wapenzi hao kwa kuanzisha chokochoko zisizokuwa na maana yoyote wala tija kwa wapendanao.

Wakati mwingine watu hujiingiza katika utovu wa maadili baada ya jamii kuwatolea hukumu isiyostahili kwa mfano binti aliye masomoni apatapo mimba husutwa na kuitwa majina mabaya ambayo yanaweza kumvunja moyo na kumfanya ajitumbukize katika vitendo viovu.

Hiyo utokea baada ya kuona kwamba jamii haikumtendea haki. Mambo kama haya pia huwakuta watu wenye ugumba ambao huhukumiwa na jamii katika namna inayowaumiza sana na kuwaelekeza katika vitendo viovu katika namna ya kujiliwaza.

ULAZIMISHAJI
Japo hali ya ulazimishaji wa ndoa imepungua kwa kiwango kikubwa lakini bado kuna watu ambao wana tabia za kuwalazimisha watoto wao wa kike na wakiume kuingia katika ndoa bila hiari zao na matokeo yake ni kusababisha misuguano isiyoisha, uzinzi, visasi kushambuliana n.k.

MALEZI DUNI NA KUTOWAJIBIKA
Malezi duni ndiyo chimbuko la maovu mengi tunayoyashuhudia katika jamii zetu, iwapo tunaajiri watu wenye malezi duni toka nyumbani tunajenga mazingira ya kuwa na watumishi waovu.

 Malezi duni huanzia katika familia moja moja lakini baadaye huathiri taasisi, mashirika na mwisho wa yote ni ubadhirifu wa mali ya umma ukatili, unyama, fitina na majungu. Labda hapo ndipo tunapoona umuhimu wa dini katika kujenga maadili mema kwa familia zetu.

Kuwajibika kwa mtu yeyote kunatokana na mambo kadhaa, kwa mfano nidhamu binafsi ya maisha, majukumu aliyokabidhiwa katika jamii kulingana na wakati husika lakini mara nyingi suala la kuwajibika linamhusu zaidi mtu mmoja mmoja yeye na nafsi yake.

Kwa mfano ni vipi mtu anawajibika kwa wazazi wake, kwa jamii yake, kwa taifa lake, kwa dini yake, kwa familia yake, au hata kwa nafsi yake mwenyewe. Kutowajibika ndicho chanzo kikubwa cha utovu wa maadili na katika hilo wahusika wanaweza kuwa wataalamu kama vile waalimu madaktari, waandishi wa habari, wachungaji, askari polisi n.k.

UDHALILISHAJI
Udhalilishaji upo wa aina nyingi kwa mfano kutowatambua watu wenye vipaji maalumu husababisha wakate tamaa na wakati mwingine wajiingize katika vitendo viovu kama njia ya kujiliwaza kama vile ulevi wa kupindukia, udhalilishaji ni pamoja na kuwanyima nafasi za kujiendeleza watumishi ambao wameonyesha dhamira hiyo na pia kukwamisha bahati zao fulani fulani.

Udhalilishaji ni pamoja na kuwabagua wenzetu katika misingi ya dini, rangi, kabila, kutotimiza ahadi zetu kwao, ikiwa ni pamoja na kuwanyima haki zao za kimsingi. Kwa mfano muajiri anayedai rushwa ya ngono kwa binti au mwanamke hiyo ni aina mojawapo ya udhalilishaji. Wakati mwingine hujitokeza watu wakakwamisha biashara za wenzao katika misingi hiyo hiyo ya chuki na udhalilishaji.

NINI BASI KIFANYIKE ILI KUREKEBISHA HALI HIYO?
Jambo la muhimu sana ni kuwa wakweli katika kila jambo tulitendalo, yaani kuwe na uwazi, bila kificho chochote. Tujue kutubu na kuwaomba radhi wenzetu mara tuwakoseapo.

Ni jambo jema hata kulipa fidia pale unapoona umemuathiri mwenzako kwa njia moja au nyingine. Kwa lugha nyingine haitoshi kwa (IGP), kuonyesha tu kwamba Jeshi la Polisi linao uwezo hata wa kuua pale linapokwamishwha katika kutimiza majukumu yake bali pia aonyeshe ni kwa jinsi gaini jeshi hilo litarudisha imani ya wananchi kwa jeshi hilo.

Tujenge utamaduni wa kuwa na shukrani na fadhila kwa wenzetu, kwa mfano mtu asiyetambua umuhimu wa kuwashukuru waliomsaidia katika jambo fulani huwavunja moyo watu hao na kusababisha wasitoe misaada kama hiyo kwa wengine.

Kwa upande mwingine tusitegemee kupewa shukrani kila tunapotenda wema kwani inaweza kujitokeza kwamba mara unapomtendea wema mtu utalipwa kwa njia nyingine na mtu tofauti kabisa na wakati mwingine mahali usipopategemea kabisa.

Mwisho kabisa tujenge tabia ya kuheshimu misingi iliyowekwa na jamii kama vile kushiriki katika misiba ya wenzetu, sherehe mbalimbali, kama vile arusi, kuwatembelea wagonjwa, tuheshimu sheria na taratibu za nchi tukiyazigatia yote haya matukio maovu ya watu kuuana na kudhuriana ya tatokomea mara moja.

Wakati tukiwa bado na kumbukumbu ya tukio la Ilongero ni muhimu pia tujiulize mtuhumiwa wa ubakaji alikuwa ni mtovu wa maadili wa kawaida au upo uwezekano alikuwa ameathirika pia kisaikolojia (psychopathy).

Vitendo vya mtuhumiwa huyo vinaashiria kwamba kuna uwezekana kwamba alikuwa na matatizo ya kisaikolojia labda kutokana na ukatili aliofanyiwa na wanadamu wenzake siku za nyuma ndipo naye akaamua kulipiza kisasi kwa njia hiyo aliyoitumia? Nakaribisha mawazo yenu

Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0754 826 272
Na kwa barua pepe: mhegeraelias@yahoo.com




Kiongozi wa Kanisa Katoliki Tanzania Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo 
TUHESHIMU DINI ZETU LAKINI PIA TUSIBEZE UTAMADUNI WETU

Novemba 25, 2007 Mtanzania Jumapili

Na Elias Mhegera
Kutokana na vuguvugu la kutaka kuanzishwa kwa mahakama ya kadhi hapa nchini tayari baadhi ya Watanzania wameanza kuwa na hofu kwamba  nchi yetu inaweza kuingia katika malumbano ambayo yanaweza kuondoa amani na utulivu mambo ambayo yamedumu kwa muda mrefu hapa nchini.

Lakini pia kuna hofu kwamba mivutano ya sasa inaweza kusababisha mambo ambayo yaliwahi kujitokeza huko nyuma kuhusiana na mivutano ya kidini makala haya yanajadili hofu hiyo.

Labda tuanze na kile kilichoandikwa na mwandishi mahiri nchini Joseph Mihangwa katika gazeti la Raia Mwema, toleo la Novemba 14-20, 2007.mada ya udini inajadiliwa katika Nasaha za Mihangwa na makala yake yenye kichwa cha habari ‘Nalilia utamaduni wangu, nimechoshwa na udini’

Kimsingi Mwandishi Joseph Mihangwa ametoa duku duku lake kulingana na hofu iliyoibuka kwamba mjadala wa Mahakama ya Kadhi unaweza kuleta mitafaruku nchini. Nami naungana mkono naye katika hilo japo napenda pia kuonyesha tofauti zangu kuhusiana na mustakabali wa hizi dini ambazo yeye ameziita ni za mapokeo.

Tofauti yangu na Mihangwa ni kwamba ni vigumu kwa sasa kusema tunaweza kuziondosha hizi dini ‘za kigeni’ yaani Uislamu na Ukristu kwa sababu tayari zimeishajikita ndani ya damu na roho zetu, lakini pia ni kwa vizazi na vizazi kwa hiyo zoezi la kuziondoa linaweza kuwa gumu.

Jambo la msingi ninaloona linaweza kutusaidia ni kutafuta maelewano ili kuheshimiana na kuweza kuishi bila migongano (dialogue).

Hata vile kwa sababu huo ulikuwa ni mtazamo wake binafsi Mihangwa anayo haki hiyo kwa sababu katika nchi yetu suala la imani ni suala binafsi na kila mtu amepewa uhuru wa kuchagua dini anayopenda ili mradi havunji sheria za nchi. Kwa mtazamo huo ni haki yake ya msingi kama ameamua kurudi katika dini yake ya mizimu.

Miaka kadhaa iliyopita nilisoma makala ya Mihangwa mmoja wa waandishi ninaowaheshimu sana kutokana na misimamo yao isiyoyumba. Makala hiyo ilikuwa inaiomba Tume ya  Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kumuunga mkono ‘Dkt’Matunge kutokana na uvumbuzi wake wa usafiri wa ungo.

Sielewi Mihangwa alimaanisha nini katika makala ile, au labda alilenga kutoa burudani tu kwa wasomaji wake. Ndiyo maana hata sasa ninakuwa na wasi wasi huo kwa sababu siamini kwamba anachokisema Mihangwa ni jambo linalowezekana katika mazingira ya sasa (feasible).

Hofu yangu hiyo inatokana na ukweli kwamba hata huo usafiri wa ungo sijawahi kuamini kwamba upo au ipo siku utakuwapo.

Lakini naomba nisieleweke kwamba mimi ni mmoja katika wale wanaomini kwamba mambo mengi hayawezekani, au yapo kwa malengo yasiyodhahiri (ploys), na kwa maana hiyo nisiwekwe katika kundi hilo la watu wenye hofu kila wakati (cynics).

Mataifa kadhaa yanao watu wasiofuata uislamu wala ukristu, kwa mfano Uchina, Japan na Korea kuna wafuasi wengi wa dhehebu la Confuscianism, Iran napo kuna wafuasi wa Baha’i madhehebu yote niliyoyataja hayafuati Uislam wala Ukristu. 

Hofu yangu ni kwamba iwapo tutakubaliana kimsingi kwamba tuziondoe hizo dini ‘za kigeni’ basi tusitarajie kwamba moja kwa moja tutakuwa tumetoa nafsi ya kukua kwa tamaduni zetu za kiasili maana hata dini zetu ambazo zilikandamizwa na ujio wa wageni. Sana sana matokeo yake kutakuwa na ombwe (vacuum) ambalo linaweza kuleta matatizo makubwa katika jamii.

Japo mimi banafsi nimelelewa katika malezi ya Kanisa Katoliki, lakini pia ninayo mengi ninayokubaliana na Mihangwa na wala sitaki nionekane kwamba ni muasi wa dini yangu isipokuwa kwamba naongozwa na mambo mawili makubwa kwamba kama tunavyofundishwa na historia.

Na pia taaluma ya uandishi wa habari naongozwa na misingi ya kitaaluma ambayo inatanguliza ukweli kwa sababu ukweli siku zote ndio unaotuweka huru.

Kwa mfano ni ukweli usiopingika kwamba wamisionari wa kwanza walichangia sana kuingia kwa ukoloni kwa sababu walipeleka nyumbani taarifa juu ya mambo mazuri waliyoyakuta Afrika (prelude) hali iliyowafanya mabepari wa kikoloni waje kuwekeza na kunyonya raslimali za bara letu.

Lakini ukiachana na hao wamisionari kuna upande wa pili wa shilingi ambapo Waarabu walifika na kuwakamata mababu zetu na kuwauza kwa wazungu tayari kwa kupelekwa utumwani.Huo ndiyo ukweli ambao hatuwezi kuufuta katika historia kuhusu kuingia kwa Ukristo na Uislamu katika bara la Afrika.

Pamoja na kwamba Waarabu walikaa katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu wakitafuta pembe za tembo na watumwa lakini ni katika maeneo hayo hayo ambako Uislamu ulishamiri.

Anzia Ujiji Kigoma, uje Tabora ambako kulikuwa na kambi ya mapumziko ya watumwa nenda Bagamoyo, na Dar es Salaam tayari kuingizwa katika mashua tayari kwa kusafirishwa kwenda Amerika ambako mpaka leo tuna kizazi cha watu weusi (African Diaspora).

Ninachomaanisha hapa ni kwamba hoja ya Mihangwa inagusa mazingira hayo ya kuingia kwa dini hizo na sasa zinataka kugeuka kuwa vyanzo vya vurugu badala kujenga umoja ambao unatokana na utamaduni wetu wa Afrika.

Yawezekana wale wanaotaka kutumia dini kutugawanya hawana kumbukumbu hiyo au vinginevyo wameamua kusamehe yale yaliyofanywa na wamisionari na Waarabu wakati wa kuingia kwao  barani Afrika.

Hivi karibuni wakati akitawazwa kuwa kiongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Alex Malasusa alionya juu ya tabia ya viongozi wa dini kujaribu kuitumia dini kwa manufaa ya kisisa.

Japo hakutaja jina la mtu lakini imani yangu kubwa ni kwamba alimlenga Mchungaji Mtikila ambaye amekuwa katika mzozo na serikali akipinga hiyo mahakama ya kadhi. Wakati akiachiliwa kwa dhamana Mchungaji Mtikila alipokelewa na viongozi wengine wa dini wenye mtazamo kama wake.

Ni dhahiri kwamba jambo hilo linatoa taswira kwamba hoja hii ya Mahakama ya Kadhi inao wapinzani wengi na wala si Mtikila pekee.Kwa hiyo huo ni ujumbe tosha kwa serikali kwamba jambo lolote ambalo linakutana na upinzani katika baadhi ya makundi ya jamii yetu basi lipewe uzito unaostahili hata kama lengo la jambo hilo nia yake ni njema (bonafide).

Ukweli wa hilo unatokana na ukweli kwamba kwa miaka kadhaa serikali yetu imedhamiria kujenga jamii yenye usawa na isiyokuwa na ubaguzi wa namna yoyote ile, sasa kama leo tutaanza kuyumbishana ina maana tutakuwa tumeondoa ile dhana kwamba serikali yetu haina dini isipokuwa watu wake ndiyo wenye dini (secularism).

Kwa lengo la kuondoa manung’uniko yasiyo na tija kwa ujenzi wa jamii yetu jambo la Mahakama ya Kadhi linaweza kufanywa kwamba ni jambo la ndani la dini husika na wala lisifike mahali likaonyesha kwamba dini fulani ni nyeti (unique) kuliko dini nyingine hali hiyo ikiendekezwa inaweza kuleta athari za udini (bigotry), tukifikia hapo basi hiyo ndiyo safari kuelekea kwenye machafuko.

Ikumbukwe kwamba hata neno ruksa kwa mara ya kwanza Mzee Ali Hassan Mwinyi alilitumia alipokuwa akihalalisha watu kula aina yoyote ya chakula bila kuingiliwa katika maamuzi yao. Akasema anayetaka kula chura ruksa, anayetaka kula nyoka ruksa. Hiyo ilifuatia kikundi cha Waislamu wenye ‘itikadi kali’ kuvamia bucha ya nguruwe ‘kiti moto’na kuvunja bucha hiyoya Mbokomu maeneo ya mwembechai.

Tukiyafanyia mzaha mambo ya dini yanaweza kuwasha moto ambao baadaye tutashindwa kuuzima. Mwaka 1966 nchini Nigeria yalizuka machafuko makubwa kutokana na mivutano ya kidini kati ya waislamu na wakristu.Chanzo cha mgogoro huo ni tabia ya wa Ibo ambao wengi wao au takribani wote ni wakristu kujiamulia mambo yao kinyume na serikali kuu ambayo ilionekana kulalia upande wa uislamu.

Kwa mfano katika mgogoro wa Waisraeli na Wapalestina wa Ibo walikuwa wanawaunga mkono Waisraeli wakati ambapo serikali kuu ilikuwa inawaunga mkono Wapalestina. Jambo hilo liliilazimisha serikali kuu kutunga sheria ambapo watu wote walilazimika kuzifuata nchini humo.

Kwa upande wao wa Ibo hawakuridhishwa na baadhi ya sheria zilizokuwa zimelalia katika misindi ya dini ya kiislamu (shariah)  na hapo ndipo wa Ibo wakiongozwa na Ezekiah Odumwegu Ojukwu wakatangaza kujitenga kwa Jimbo la Biafra kwa lengo la kuunda serikali yao kamili mpango ambao ulisababisha machafuko na vifo vya watu kadhaa.

Tatizo la Biafra lilichukua sura ya kimataifa ambapo Mwalimu Nyerere pia alimuunga mkono Ojukwu, na mataifa mengine yaliiunga mkono serikali kuu. Haishangazi Ojukwu alikuwa mmojawapo wa Wanaigeria walioambatana na Rais Mstaafu wa Nigeria Olusegen Obasanjo katika Mazishi ya Mwalimu Nyerere mwezi Oktoba 1999.

Kwa hapa Tanzania ukiachana na suala la mabucha ya Mbokomu kumekuwapo na matatizo ya mara kwa mara katika msikiti wa Mwembechai . Vurugu hizo zimewahi kusababisha kuvunjwa vunjwa kwa vioo vya magari ya serikali na hata kuuawa kwa kuchomwa visu kwa askari polisi katika machafuko ya aina hiyo wafuasi wawili madhehebu ya Kiislamu wamewahi kuuawa.

Labda katika harakati za ‘kumtafuta mchawi’ chama cha upinzani CUF kilituhumiwa kwamba ndicho kilihusika na uchochezi wa vurugu hizo.Chama hicho kwa upande wake kilikanusha vikali tuhuma hizo. Vyovyote iwavyo lakini lazima tufahamu kwamba kuuzima moto unaotokana na uhasama wa kidini si jambo jepesi kwani hayo ni masuala yanayohusu imani za watu.

Kwa ujumla tunaweza kukubaliana kwamba kuna nyakati uchochezi wa udini unafanywa na watu wa nje na wala huwezi kusema kwamba hiyo ni chokochoko ya wakorofi wachache tu ndani ya nchi.

Matukio ya Bosnia, Serbia, na Poland kwa kiwango kikubwa yalichochewa kutoka nje.Hali kama hiyo imejitokeza hivi karibuni nchini Somalia ambapo kulikuwa na mapambano makali kati ya wanamgambo wa mahakama za kiislamu na majeshi ya Ethiopia.

Upo ushahidi kwamba makundi ya wanamgambo wa mahakanma za kiislamu walielekea kuizidia nguvu serikali ya Somalia kwa sababu walikuwa wanapewa msaada kutoka Irani, ndipo kwa upande mwingine Marekani ilipojitokeza na kutoa zana za kivita ambapo majeshi ya Ethiopia yaliweza kuwasambaratisha wanamgambo wa kiislamu.

Kwa upande wa Poland nchi ambayo Hayati Papa John Paul II alikuwa anatoka hakukubaliana na utawala wa kikomunisti wa serikali ya Jenerali Jaruzeski na hatimaye papa huyo alikiunga mkono chama cha wafanyakazi cha Solidarity kikiongozwa na Lech Walesa ambacho hatimaye kilifanikiwa kuungusha utawala wa kikomunisti nchini humo.

Yote haya yanatufundisha kwamba ushawishi wa dini ni mkubwa sana katika siasa kwa hiyo viongozi wa dini wanatakiwa kuwa makini katika uendeshaji wa mambo yao ili isifikie mahali wao ndiyo wakawa vyanzo vya machafuko kama ilivyokuwa kwa Sudani, Chechnya, Afghanstan n.k.

Miaka ya nyuma kiongozi wa Italia Benito Mussolini aliona umuhimu wa kufanya maelewano na viongozi wa Kanisa Katoliki na baadaye walisaini mkataba wa maelewano (The Lateran Treaty , 1929)ambao hatimaye uliitambua Vatican kama mamlaka kamili ndani ya Italia. Huo ni mfano tosha wa jinsi ambavyo serikali zinatakiwa kushughulikia masuala ya dini kulingana na mazingira halisi.

Mvutano uliopo sasa kimataifa ni kile kinachoitwa ubeberu wa kimarekani kupitia katika utandawazi. Haishangazi kwamba Waislamu wa Nigeria walipinga mashindano ya urembo yasifanyikie nchini mwao na badala yake yalihamishiwa Sanya nchini China.

Yote hiyo ni katika kuonyesha kwamba pande hizo mbili zimeshindwa kufikia muafaka (dialogue) kuhusuana na tofauti zilizopo ambazo zinaweza kupata ufumbuzi na kuondoa mivutano isiyo na tija.

Kwa upande wa nchi za magharibi nazo hazijachoka kutoa nafasi kwa wakosoaji wa Uislamu kama vile mwanamama Ayaan Hirsi Ali mkimbizi kutoka Somalia ambaye ameishi nchini Uholanzi kuanzia mwaka 1992 akipinga ndoa ya lazima aliyopangiwa nchini mwake.

Kwa sasa mwanamke huyo anaandika mengi ambayo anayaona ni ukandamizaji wa dhahiri wa mwanamke unaofanywa na dini ya kiislamu, mama huyo kwa sasa ni mbunge nchini Uholanzi. Wapo wengine wanaomuunga mkono kama vile Naghem Khadhim wa Iraq na Homa Arjomand wa Irani.

Kwa hapa Tanzania mvutano uliopo si kwamba ni wa Waislamu na Wakristu pekee lakini hata Wasabato ambao mara kadhaa wamekuwa wakilalalamika kwamba siku yao haiheshimiwi, labda tatizo lililo dhahiri hapo ni kwamba ipo siku hata Waislamu watadai kwamba Ijumaa iwe siku ya mapumziko kama ilivyo kwa Jumamaosi na Jumapili sijui mwisho wa yote hayo utakuwa ni upi.

Kwa hakika tunahitaji kukaa na kufanya maelewano ya kidini ili kupunguza mizozo isiyo na manufaa vinginevyo tutafikia mahali pa kuanzisha vikundi vya kuziondoa dini za kigeni (nihilistic movements), hapo ndipo tutakuwa tumefikia mwisho wa amani yetu. Chonde chonde Watanzania tusifikie huko!

Lakini kwa Mihangwa kama ameamua kurudi alikotoka na tumtakie safari njema, wasalimie Mlungu na Kubeh!

Mwandishi wa makala haya anapatikana kwa simu 0754 826 272, na Barua pepe: mhegeraelias@yahoo.com





WASTAAFU WAJISAFISHE ILI WAHESHIMIWE!

Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere alikaa Ikulu kwa zaidi ya miaka 20 na kuaondoka akiwa na mali za kawaida kabisa, leo Ikulu ni mahali pa watu kujitajirisha!

Oktoba 28, 2007 Mtanzania Jumapili

Na Elias Mhegera
Kila mfuatiliaji wa masuala ya kijamii katika vyombo vya habari nchini Tanzania atakubaliana nami kwamba miongoni mwa habari ambazo zimegonga vichwa vya habari vingi hususani katika magazeti katika siku za hivi karibuni ni tuhuma za ufisadi zinazoelekezwa kwa rais mstaafu wa awamu ya tatu Benjamini Mkapa.

Nimeshawishika kuchangia mawili matatu katika mjadala huo muhimu kwa maslahi ya taifa letu.

Labda kabla hata sijaenda mbali katika mjadala huu naomba nieleweke wazi kwamba simo katika kundi la wale wanaotaka iundwe tume kuchunguza tuhuma hizo za ufisadi wake, sababu zangu ni kwamba ni dhahiri kufanya hivyo hakutatuletea tija yoyote na badala yake tutaliingiza taifa katika gharama kubwa na mwisho wa siku tutaambiwa hakuna ushahidi wowote kuhusiana na tuhuma hizo.

Lakini pia naomba kutanabahisha kwamba mnamo mwaka 1995 Mkapa alipotajwa kwamba ni mtu msafi ‘Mr. clean’ nilikuwa na wasiwasi mkubwa juu ya usafi huo. Hofu yangu ilitokana na imani yangu kwamba kama kweli Mkapa alikuwa msafi basi alikuwa ni mtu wa kipekee kwani mazingira ya wakati ule yalitoa mwanya mkubwa kwa viongozi wengi kujilimbikizia mali kwa kile kilichoitwa kupunguza ‘ukali wa maisha’

Hofu niliyokuwa nayo wakati ule ndiyo hiyo hiyo inayonitatiza juu ya uwezekano wa kuundwa kwa tume huru inayoweza kuja na majibu ya uhakika na yanayoweza kukidhi matarajio ya watanzania wengi juu ya tuhuma hizo ambazo zinafumuliwa kila uchao.

Kwa hiyo naona kuna uwezekano kwamba siasa za makundi zilizoibuka hivi karibuni katika nchi yetu ndizo zinazochangia kufumuliwa kwa tuhuma hizo na inawezekana wanaofanya hivyo hawana usafi wowote pia ni watu waliokuwa ndani ya mfumo huo huo.

Naomba nisieleweke kwamba namtetea Mkapa kwa namna yoyote ile isipokuwa nataka kutanabahisha kwamba matatizo ya Mkapa ni matatizo ya mifumo tawala yote isiyotaka kuachia madaraka (rigid systems) ambayo imesambaa takribani katika bara letu zima la Afrika.

Kwa lugha nyingine ni kwamba mfumo alioupokea na ule aliofanya nao kazi na baadaye kukabidhi madaraka katika mfumo mpya lakini wa chama kile kile ni mazingira yanayoweza kusababisha kwa mtu yeyote awaye kukengeuka kimaadili hata kama aliingia madarakani akiwa msafi.

Kutokana na kukaa madarakani kwa muda mrefu kwa chama kimoja lazima kuwepo na madhara ya aina fulani kisiasa kama tunavyoshuhudia sasa hapa nchini mwetu.

Lakini pia chama pekee si tatizo bali tatizo linakuja pale chama tawala kinapokosa vyombo mahususi vya ukosoaji kama vile asasi za kiraia, vyombo huru vya habari vyama vya dhati vya upinzani na mambo kadhaa yanayoweza kuweka mazingira ya utendaji halali wa serikali iliyopo madarakani (legitimacy).

Ile dhana kwamba huyu ni mwenzetu ambayo ilikuwa inatumiwa mara kadhaa na wanasiasa wa chama tawala ilikuwa na mwangwi mbaya kwa sababu ilionyesha kwamba chama kilikuwa tayari kulinda hata waovu kisa tu ni ‘wenzetu’siasa iligeuzwa kuwa ajira ya kudumu badala ya kuthaminiwa kwamba utumishi wa umma ni jambo la kujitolea tena kwa watu wasafi na wenye dhamira njema pekee na wala si kwa kila awaye 

Ni hofu hiyo ndiyo ilinishawihi niamini kwamba kama kuna dhana ya huyo ni mwenzetu maana yake kulikuwa na mazingira ya kuwalinda wale waliokuwa na hofu ya kukabiliwa na mashtaka ya ufisadi kwa hiyo labda walimuona Mkapa kwamba ni mtu ambaye asingediriki kuhatarisha maslahi ya watu wa aina hiyo.

Kwa lugha nyingine mfumo wa awamu ya pili ndiyo hasa ulikuwa chimbuko lililojenga mazingira ya ufisadi wa baadhi ya viongozi wetu, mazingira ambayo hayakuwepo katika awamu ya kwanza ya Hayati Mwalimu Nyerere.

Kwa kusema hivyo simaanishi kwamba ufisadi haukuwepo kabisa katika awamu ya kwanza isipokuwa ulijengewa mazingira magumu ya kushamiri. Wenye nacho walijengewa mazingira magumu ya kuonyesha ukwasi wao (extravagancy).

Hivyo basi yawezekana kabisa kwamba viongozi wetu walianza kujichumia mali taratibu, kimya kimya katika awamu ya kwanza lakini wakaonyesha kucha zao katika awamu iliyofuata kutokana na ukweli kwamba mazingira yaliwaruhusu kufanya hivyo.

Kwa maana hiyo kile kilichoitwa usafi wa Mkapa yawezekana kilitokana na ukweli kwamba yeye binafsi kamwe hakuwahi kujidhihirisha kwamba alikuwa muathirika wa ukwasi wa viongozi wa awamu ya pili jambo ambalo lilichangia kuanguka kwa umaarufu wa kisiasa wa Mzee Ali Hassan Mwinyi.

Upo pia uwezekano kwamba Mkapa alikuwa mtu msafi hadi wakati ule lakini aliharibiwa na mfumo alioukuta kwa sababu hakuweza kufanya mabadiliko ya dhati kuwaondoa viongozi ambao usafi wao kimaadili ulikuwa unatia mashaka.

Historia inatuonyesha kwamba wapo viongozi ambao wamepata kuharibiwa na mifumo japokuwa walikuwa na dhamira safi kabla ya kutekwa nyara na mafisadi na watu wenye dhamira za kufanikisha mambo yao binafsi.La kushangaza ni kwamba historia inatueleza kwamba hata watu kama Adolf Hitler ambao baadaye wamekuja kingizwa katika safu ya madikteta wabaya kabisa waliopata kutokea hapa duniani nao walianza kama watu wenye dhamira njema hadi pale walipotekwa nyara na watu wenye maslahi binafsi.

Hadi pale alipotoa kitabu chake ‘Mein Kempf’ (1925) yaani mapambano yangu bado Hitler alikuwa bado ni mtu mwenye dhamira safi kabisa. Lakini dhamira hiyo safi ya kuwatumikia wanyonge aliyokuwa nayo Hitler iliotekwa nyara na mabepari waliohofia kutaifishwa mali zao iwapo utawala wa kikomunisti ungeingia madarakani kwa hiyo mabepari hao ndiyo waliomteka nyara Hitler wakamgeza kuwa chombo cha kulinda maslahi yao hususani mali na viwanda vyao.

Kuungwa mkono huko kwa Hitler hakukuja kama bahati mbaya bali kulitokana na fundisho walilopata kutoka kwa wenzao wa Urusi baada ya mapinduzi ya kikomunisti yaliyoendeshwa na V.I. Lenini Oktoba 1917.
Katika mazingira hiyo mabepari wa Ujerumani walikuwa na haki ya kulinda mali zao ili zisije taifishwa na kuwekwa mikononi mwa umma kama ilivyojitokeza huko Urusi. Hata hivyo Hitler huyo huyo baadaye aligeuaka na kuwa shubiri kwa kila mpenda amani duniani yaliyofuata baada ya hapo ni historia ambayo inafahamika na takribani na kila mmoja wetu.

Kwa mantiki hiyo ndiyo maana nasema upo uwezekano kwamba Mkapa alikuwa mtu msafi kabisa lakini alitekwa nyara katikati ya safari yake na kundi fulani la watu ambao walikuwa wametanguliza maslahi yao binafsi.
Ni kundi hilo ambalo limesababisha sasa aandamwe an tuhuma nyingi ambazo hata hivyo hajawahi kuzikanusha kwa ukamilifu bali amekuwa akizizungumzia kijuujuu tu.

Kwa hiyo kama tunajiaminisha kwamba mkapa alikuwa mtu msafi basi lazima tukubali kwamba lipo kundi la watanzania wenzetu ambalo lilimpaka mawaa likamvuta katika ufisadi, akajikuta ameangukia huko bila kutarajia.

Kwa upande mwingine naweza kusema kwamba hatuna uhakika kama kundi hilo bado limo ndani ya mfumo unaotawala sasa au la kwa sababu chama ni kile kile japo yamefanyika mabadiliko hapa na pale.

Lakini upo uwezekano pia kwamba kama kweli tuhuma zinazoelekezwa kwa Mkapa zina ukweli basi labda msukumo ulitoka nje.  Kwa upande huo napenda niunge mkono hoja iliyotolewa na mwandishi mwandamizi Lawrence Kilimwiko katika makala yake: Afrika Bado Haijawa Huru, Mwananchi, toleo namba. 02634 jumatano Agosti 29, 2007.

Hoja ya Kilimwiko  katika makala yake ni kwamba viongozi wetu wanaangukia katika ufisadi kwa sababu ya kukubali kutumiwa kama maajenti wa maslahi ya nje.

Jambo hilo linafanyika  kwa lengo la kulinda mikataba inayolinyonya bara letu au hata kwa lengo la kuanzisha mikataba mipya ya aina hiyo. Kilimwiko anatahadharisha kwamba hicho ni chanzo kimojawapo cha kushidikana kwa wazo la kuwa na serikali moja ya bara la Afrika.

Kwa hiyo kama kuna ukweli juu ya tuhuma zinazoelekezwa kwa Mkapa basi tuziangalie katika mtindo huo kwamba yawezekana amepotoshwa na kundi la mafisadi wa ndani, wa nje au hata kwa ujumuisho wa makundi yote haya mawili la ndani na lile la nje.

Hapo ndipo kuna swali muhimu kwetu kwamba tupo tayari kuikabili na kuitokomeza mifumo yote hiyo miwili ama tunataka tuishie kwa Mkapa peke yake?

Katika kitabu chao Governance and Politics in Africa (1992) waandishi Goran Hyden na Michael Bratton wansema tatizo lililopo Afrika ni ile hali ya kupokea na kuanzisha siasa za ushindani ambazo kwa kweli zimeonyesha kwamba bara letu lilikuwa bado halijaandaliwa vya kutosha kwa siasa za aina hiyo. Matokeo yake ni kwamba vyama tawala vimeamua kuwabagua wapinzani hata katika mambo ambayo ni ya kimsingi kabisa na yanatija kwa watu wote bila kujali itikadi zao.

Mifumo tawala ndiyo inajipa ukiranja wa usimamizi na ugawaji wa raslimali za taifa hali ambayo imechangia kuwapo kwa mikanganyiko mingi na ufisadi.

Ni katika mazingira hayo sasa tunaweza kutoa hukumu ya haki kwa Mkapa, kwa kuzingatia suala la mifumo na misukukumo ya ndani na nje na wala siyo kwa kumunyooshea kidole yeye binafsi, kwa hiyo tuanze na mifumo ndipo tumalize na watu binafsi kama kweli tumedhamiria kupata ufanisi wa kudumu.

Ndiyo maana mimi binafsi kama mwandishi sina sababu ya kumtetea Mkapa lakini pia sioni sababu ya kundwa kwa tume ya kumchunguza kwa sababu kufanya hivyo ni kuliingiza taifa katika gharama kubwa na mwisho wa yote hakuna lolote la maana litakaloletwa na tume hiyo kama kweli itaundwa.

Sababu nyingine ni kwamba lazima tuangalie kwamba serikali iliyopo madarakani ni ile ile ya CCM. Kwa namna yoyote ile tuhuma zinazomhusu Mkapa (kama kweli zipo) lazima zitawagusa pia baadhi ya watendaji wakubwa wa serikali iliyopo madarakani kwa sasa jambo hilo linaweza kujenga mazingira ya kulindana.

Lakini la muhimu zaidi ni kwamba pamoja na mapungufu yake rais huyo mstaafu ameacha mambo kadhaa ya kimaendelo ambayo kwa sasa inaelekea yanasusua, hasa suala la ujenzi wa barabara ambao ulikwenda kwa kasi nzuri ya kuvutia katika kipindi cha uongozi wake.

Kwa hiyo ni lazima tufahamu kwamba pamoja na mapungufu yake zikiwemo tuhuma za kufanya biashara akiwa Ikulu, tuhuma nyingi si kwamba zinamgusa yeye pekee bali zinaugusa mfumo mzima uliokuwepo madarakani katika kipindi chake wakiwemo baadhi ya mawaziri ambao wamo katika awamu iliyopo madarakani kwa sasa.

Kama vile hiyo haitoshi tushukuru pia kwamba mfumo wa Mkapa ulikuwa na uwazi na uliruhusu kukosolewa jambo ambalo ni la muhimu katika ujenzi wa demokrasia na ndiyo maana waandishi wa habari walikuwa na uhuru wa kukosoa kila walipojisikia kufanya hivyo.
Kipindi cha utawala wake Mkapa hakuwa na kikundi cha waandishi wa kumtetea bali alijibu mapigo yeye binafsi kwa kadri alivyoona inafaa.

Ipo haja ya rais wa sasa kuchota yale machache anayoona kwamba yatamfaa katika uendeshaji wa serikali yake ya sasa. Kwa mfano ipo haja ya kupunguza ukubwa wa serikali nikiwa na maana ya kwamba baraza la mawaziri ni kubwa kuliko mahitaji halisi na uwezo wa nchi yetu kumudu gharama za mawaziri hao

Kinachojitokeza sasa kinanifanya nikumbuke dhana zilizojengwa na mwanafalsafa wa kiitaliano kwa jina Antonio Gramsci aliyeishi 1891-1937. Gramsci anayo machapisho mengi lakini yanayokumbukwa zaidi ni yale aliyoandika alipokuwa gerezani kati ya mwaka 1925-35.kutokana na kupinga ukandamizaji nchini mwake.

Mwanafalsafa huyo anazungumzia dhana nzima ya ukiritimba wa vyama kuhodhi madaraka kwa muda mrefu kwa kuhakikisha kwamba wapinzani wote wenye nguvu wanamezwa ndani ya vyama hivyo (co-optation), au vinginevyo wawe tayari kuangamizwa.

Anasema mfumo tawala uliokaa madarakani kwa muda mrefu hufikia mahali ukachoka na kushindwa kuleta mambo mapya lakini hubakia madarakani kwa kazi hiyo ya kujenga himaya ya kisiasa (hegemony). Kwa hiyo kubakia madarakani ni zoezi linalopewa kipaumbele kuliko mambo mengine yenye tija zaidi.

Mifumo tawala hulazimisha makundi yote yenye nguvu kuunga mkono mfumo tawala kwa njia mbali mbali ikiwemo kuunda tume na vyombo au itikadi zisizo na maana yoyote zaidi ya kuwapofusha watawaliwa.

Katika kutimiza hilo mfumo tawala hujenga mazingira ya kuungwa mkono kwa kila jambo, hata asasi za kiraia, wasomi, viongozi wa dini waandishi wa habari wote huvutwa ndani ya mfumo tawala kwa kutumia mbinu mbalimbali ili waunge mkono matakwa ya watawala.

Kwa bahati mbaya pale inapofikia kwamba makundi yote hayo yakagundua kwamba kuna hadaa nyingi kuliko utendaji ndipo mapambano ya dhati huanza na mwishowe ni kuzaa udikteta na ukandamizaji wa hali ya juu dhidi ya wote wanaotaka kujitoa katika “himaya” hiyo.

Yawezekana falsafa hiyo ya Gramsci ilitokana na kufungwa na utawala mbovu nchini mwake lakini mawazo yake yanatupatia fundisho kwamba si jambo jema kwa kiongozi kusifiwa sana au hata kumiliki madaraka makubwa kupita kiasi.Kama hatutaanza sasa kurekebisha mambo tusishangae kuona hali hiyo ikijitokeza hata hapa kwetu Tanzania.

Kinachonipa hofu hiyo ni ukweli kwamba tumejenga mazingira magumu sana kwa rais aliyepo madarakani kwa sasa kukosolewa. Takribani kila kundi kubwa limemezwa ndani ya ‘mtandao’ uliofanikisha zoezi la kumuingiza madarakani Rais Kikwete. Hali hiyo si ishara nzuri katika ujenzi wa demokrasia.

Tunaona kwamba makundi mbalimbali yameguswa katika teuzi mbalimbali baada ya uchaguzi mkuu uliopita. Viongozi wa taasisi, madaktari, waandishi wa habari, wahadhiri wa vyuo vikuu, wasanii, n.k. wote wamemezwa ndani ya mfumo tawala.

Mazingira tuliyonayo ambapo kila inapojitokeza mwandishi mmoja akaukosoa mfumo tawala basi hushambuliwa vilivyo na kundi jingine  la waandishi ambao kwa haraka haraka huzima hoja yoyote ile isiyoufurahisha mfumo tawala. Hii si njia muafaka katika ujenzi wa demokrasia.

Waandishi hao wenye kuwashambulia wenzao wananifanya niamini kwamba Rais Mstaafu Mkapa alikuwa sahihi zaidi kwa kuruhusu kukosolewa na kujibu mapigo yeye mwenyewe pale alipoona inastahili kufanya hivyo.

Nadhani sasa ni muda muafaka kila amtakiaye rais wetu mema afanye hivyo kwa kuzingatia pande zote mbili yaani kupongeza pale inapostahili na pia kukosoa inapobidi kufanya hivyo.

Ni dhahiri kwamba kama tutaendeleza tabia ya kumpamba rais kila uchao badala ya kumsahihisha pale tunapohitajika kufanya hivyo kwa njia ya kumkosoa basi tutakuwa tunambomoa badala ya kumjenga.Vyombo vya habari ni viunganishi kati ya watawala na watawaliwa tuache vitimize jukumu hilo.

Naungana mkono hoja ya wale wanaosema Mkapa aachwe apumzike kwa sababu utamaduni wetu wa kisiasa hauonyeshi kama kweli kuna jambo lenye manufaa litakalopatikana baada ya kumchunguza zaidi ya kupoteza bure pesa za walipa kodi, na tumuache Mkapa apumzike aliyotutendea yanatosha aliyotukosea basi tumsamehe.

Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu 0754 826 272