Kiongozi wa Kanisa Katoliki Tanzania Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo
TUHESHIMU DINI ZETU LAKINI PIA TUSIBEZE
UTAMADUNI WETU
Novemba 25, 2007 Mtanzania Jumapili
Na
Elias Mhegera
Kutokana
na vuguvugu la kutaka kuanzishwa kwa mahakama ya kadhi hapa nchini tayari
baadhi ya Watanzania wameanza kuwa na hofu kwamba nchi yetu inaweza kuingia katika malumbano
ambayo yanaweza kuondoa amani na utulivu mambo ambayo yamedumu kwa muda mrefu
hapa nchini.
Lakini
pia kuna hofu kwamba mivutano ya sasa inaweza kusababisha mambo ambayo yaliwahi
kujitokeza huko nyuma kuhusiana na mivutano ya kidini makala haya yanajadili
hofu hiyo.
Labda
tuanze na kile kilichoandikwa na mwandishi mahiri nchini Joseph Mihangwa katika
gazeti la Raia Mwema, toleo la Novemba 14-20, 2007.mada ya udini inajadiliwa
katika Nasaha za Mihangwa na makala yake yenye kichwa cha habari ‘Nalilia
utamaduni wangu, nimechoshwa na udini’
Kimsingi
Mwandishi Joseph Mihangwa ametoa duku duku lake kulingana na hofu iliyoibuka
kwamba mjadala wa Mahakama ya Kadhi unaweza kuleta mitafaruku nchini. Nami
naungana mkono naye katika hilo japo napenda pia kuonyesha tofauti zangu
kuhusiana na mustakabali wa hizi dini ambazo yeye ameziita ni za mapokeo.
Tofauti
yangu na Mihangwa ni kwamba ni vigumu kwa sasa kusema tunaweza kuziondosha hizi
dini ‘za kigeni’ yaani Uislamu na Ukristu kwa sababu tayari zimeishajikita ndani
ya damu na roho zetu, lakini pia ni kwa vizazi na vizazi kwa hiyo zoezi la
kuziondoa linaweza kuwa gumu.
Jambo
la msingi ninaloona linaweza kutusaidia ni kutafuta maelewano ili kuheshimiana
na kuweza kuishi bila migongano (dialogue).
Hata
vile kwa sababu huo ulikuwa ni mtazamo wake binafsi Mihangwa anayo haki hiyo
kwa sababu katika nchi yetu suala la imani ni suala binafsi na kila mtu amepewa
uhuru wa kuchagua dini anayopenda ili mradi havunji sheria za nchi. Kwa mtazamo
huo ni haki yake ya msingi kama ameamua kurudi katika dini yake ya mizimu.
Miaka
kadhaa iliyopita nilisoma makala ya Mihangwa mmoja wa waandishi ninaowaheshimu
sana kutokana na misimamo yao isiyoyumba. Makala hiyo ilikuwa inaiomba Tume
ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH)
kumuunga mkono ‘Dkt’Matunge kutokana na uvumbuzi wake wa usafiri wa ungo.
Sielewi
Mihangwa alimaanisha nini katika makala ile, au labda alilenga kutoa burudani
tu kwa wasomaji wake. Ndiyo maana hata sasa ninakuwa na wasi wasi huo kwa sababu
siamini kwamba anachokisema Mihangwa ni jambo linalowezekana katika mazingira
ya sasa (feasible).
Hofu
yangu hiyo inatokana na ukweli kwamba hata huo usafiri wa ungo sijawahi kuamini
kwamba upo au ipo siku utakuwapo.
Lakini
naomba nisieleweke kwamba mimi ni mmoja katika wale wanaomini kwamba mambo
mengi hayawezekani, au yapo kwa malengo yasiyodhahiri (ploys), na kwa maana
hiyo nisiwekwe katika kundi hilo la watu wenye hofu kila wakati (cynics).
Mataifa
kadhaa yanao watu wasiofuata uislamu wala ukristu, kwa mfano Uchina, Japan na
Korea kuna wafuasi wengi wa dhehebu la Confuscianism, Iran napo kuna wafuasi wa
Baha’i madhehebu yote niliyoyataja hayafuati Uislam wala Ukristu.
Hofu
yangu ni kwamba iwapo tutakubaliana kimsingi kwamba tuziondoe hizo dini ‘za
kigeni’ basi tusitarajie kwamba moja kwa moja tutakuwa tumetoa nafsi ya kukua
kwa tamaduni zetu za kiasili maana hata dini zetu ambazo zilikandamizwa na ujio
wa wageni. Sana sana matokeo yake kutakuwa na ombwe (vacuum) ambalo linaweza
kuleta matatizo makubwa katika jamii.
Japo
mimi banafsi nimelelewa katika malezi ya Kanisa Katoliki, lakini pia ninayo
mengi ninayokubaliana na Mihangwa na wala sitaki nionekane kwamba ni muasi wa
dini yangu isipokuwa kwamba naongozwa na mambo mawili makubwa kwamba kama tunavyofundishwa
na historia.
Na
pia taaluma ya uandishi wa habari naongozwa na misingi ya kitaaluma ambayo
inatanguliza ukweli kwa sababu ukweli siku zote ndio unaotuweka huru.
Kwa
mfano ni ukweli usiopingika kwamba wamisionari wa kwanza walichangia sana
kuingia kwa ukoloni kwa sababu walipeleka nyumbani taarifa juu ya mambo mazuri
waliyoyakuta Afrika (prelude) hali iliyowafanya mabepari wa kikoloni waje
kuwekeza na kunyonya raslimali za bara letu.
Lakini
ukiachana na hao wamisionari kuna upande wa pili wa shilingi ambapo Waarabu
walifika na kuwakamata mababu zetu na kuwauza kwa wazungu tayari kwa kupelekwa
utumwani.Huo ndiyo ukweli ambao hatuwezi kuufuta katika historia kuhusu kuingia
kwa Ukristo na Uislamu katika bara la Afrika.
Pamoja
na kwamba Waarabu walikaa katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu wakitafuta
pembe za tembo na watumwa lakini ni katika maeneo hayo hayo ambako Uislamu
ulishamiri.
Anzia
Ujiji Kigoma, uje Tabora ambako kulikuwa na kambi ya mapumziko ya watumwa nenda
Bagamoyo, na Dar es Salaam tayari kuingizwa katika mashua tayari kwa
kusafirishwa kwenda Amerika ambako mpaka leo tuna kizazi cha watu weusi
(African Diaspora).
Ninachomaanisha
hapa ni kwamba hoja ya Mihangwa inagusa mazingira hayo ya kuingia kwa dini hizo
na sasa zinataka kugeuka kuwa vyanzo vya vurugu badala kujenga umoja ambao
unatokana na utamaduni wetu wa Afrika.
Yawezekana
wale wanaotaka kutumia dini kutugawanya hawana kumbukumbu hiyo au vinginevyo
wameamua kusamehe yale yaliyofanywa na wamisionari na Waarabu wakati wa kuingia
kwao barani Afrika.
Hivi
karibuni wakati akitawazwa kuwa kiongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri
Tanzania (KKKT), Askofu Alex Malasusa alionya juu ya tabia ya viongozi wa dini
kujaribu kuitumia dini kwa manufaa ya kisisa.
Japo
hakutaja jina la mtu lakini imani yangu kubwa ni kwamba alimlenga Mchungaji
Mtikila ambaye amekuwa katika mzozo na serikali akipinga hiyo mahakama ya
kadhi. Wakati akiachiliwa kwa dhamana Mchungaji Mtikila alipokelewa na viongozi
wengine wa dini wenye mtazamo kama wake.
Ni
dhahiri kwamba jambo hilo linatoa taswira kwamba hoja hii ya Mahakama ya Kadhi
inao wapinzani wengi na wala si Mtikila pekee.Kwa hiyo huo ni ujumbe tosha kwa
serikali kwamba jambo lolote ambalo linakutana na upinzani katika baadhi ya
makundi ya jamii yetu basi lipewe uzito unaostahili hata kama lengo la jambo
hilo nia yake ni njema (bonafide).
Ukweli
wa hilo unatokana na ukweli kwamba kwa miaka kadhaa serikali yetu imedhamiria
kujenga jamii yenye usawa na isiyokuwa na ubaguzi wa namna yoyote ile, sasa
kama leo tutaanza kuyumbishana ina maana tutakuwa tumeondoa ile dhana kwamba
serikali yetu haina dini isipokuwa watu wake ndiyo wenye dini (secularism).
Kwa
lengo la kuondoa manung’uniko yasiyo na tija kwa ujenzi wa jamii yetu jambo la
Mahakama ya Kadhi linaweza kufanywa kwamba ni jambo la ndani la dini husika na
wala lisifike mahali likaonyesha kwamba dini fulani ni nyeti (unique) kuliko
dini nyingine hali hiyo ikiendekezwa inaweza kuleta athari za udini (bigotry),
tukifikia hapo basi hiyo ndiyo safari kuelekea kwenye machafuko.
Ikumbukwe
kwamba hata neno ruksa kwa mara ya kwanza Mzee Ali Hassan Mwinyi alilitumia alipokuwa
akihalalisha watu kula aina yoyote ya chakula bila kuingiliwa katika maamuzi
yao. Akasema anayetaka kula chura ruksa, anayetaka kula nyoka ruksa. Hiyo
ilifuatia kikundi cha Waislamu wenye ‘itikadi kali’ kuvamia bucha ya nguruwe
‘kiti moto’na kuvunja bucha hiyoya Mbokomu maeneo ya mwembechai.
Tukiyafanyia
mzaha mambo ya dini yanaweza kuwasha moto ambao baadaye tutashindwa kuuzima.
Mwaka 1966 nchini Nigeria yalizuka machafuko makubwa kutokana na mivutano ya
kidini kati ya waislamu na wakristu.Chanzo cha mgogoro huo ni tabia ya wa Ibo
ambao wengi wao au takribani wote ni wakristu kujiamulia mambo yao kinyume na
serikali kuu ambayo ilionekana kulalia upande wa uislamu.
Kwa
mfano katika mgogoro wa Waisraeli na Wapalestina wa Ibo walikuwa wanawaunga
mkono Waisraeli wakati ambapo serikali kuu ilikuwa inawaunga mkono Wapalestina.
Jambo hilo liliilazimisha serikali kuu kutunga sheria ambapo watu wote walilazimika
kuzifuata nchini humo.
Kwa
upande wao wa Ibo hawakuridhishwa na baadhi ya sheria zilizokuwa zimelalia katika
misindi ya dini ya kiislamu (shariah) na
hapo ndipo wa Ibo wakiongozwa na Ezekiah Odumwegu Ojukwu wakatangaza kujitenga
kwa Jimbo la Biafra kwa lengo la kuunda serikali yao kamili mpango ambao
ulisababisha machafuko na vifo vya watu kadhaa.
Tatizo
la Biafra lilichukua sura ya kimataifa ambapo Mwalimu Nyerere pia alimuunga
mkono Ojukwu, na mataifa mengine yaliiunga mkono serikali kuu. Haishangazi Ojukwu
alikuwa mmojawapo wa Wanaigeria walioambatana na Rais Mstaafu wa Nigeria
Olusegen Obasanjo katika Mazishi ya Mwalimu Nyerere mwezi Oktoba 1999.
Kwa
hapa Tanzania ukiachana na suala la mabucha ya Mbokomu kumekuwapo na matatizo ya
mara kwa mara katika msikiti wa Mwembechai . Vurugu hizo zimewahi kusababisha
kuvunjwa vunjwa kwa vioo vya magari ya serikali na hata kuuawa kwa kuchomwa
visu kwa askari polisi katika machafuko ya aina hiyo wafuasi wawili madhehebu
ya Kiislamu wamewahi kuuawa.
Labda
katika harakati za ‘kumtafuta mchawi’ chama cha upinzani CUF kilituhumiwa
kwamba ndicho kilihusika na uchochezi wa vurugu hizo.Chama hicho kwa upande
wake kilikanusha vikali tuhuma hizo. Vyovyote iwavyo lakini lazima tufahamu
kwamba kuuzima moto unaotokana na uhasama wa kidini si jambo jepesi kwani hayo
ni masuala yanayohusu imani za watu.
Kwa
ujumla tunaweza kukubaliana kwamba kuna nyakati uchochezi wa udini unafanywa na
watu wa nje na wala huwezi kusema kwamba hiyo ni chokochoko ya wakorofi wachache
tu ndani ya nchi.
Matukio
ya Bosnia, Serbia, na Poland kwa kiwango kikubwa yalichochewa kutoka nje.Hali
kama hiyo imejitokeza hivi karibuni nchini Somalia ambapo kulikuwa na mapambano
makali kati ya wanamgambo wa mahakama za kiislamu na majeshi ya Ethiopia.
Upo
ushahidi kwamba makundi ya wanamgambo wa mahakanma za kiislamu walielekea kuizidia
nguvu serikali ya Somalia kwa sababu walikuwa wanapewa msaada kutoka Irani,
ndipo kwa upande mwingine Marekani ilipojitokeza na kutoa zana za kivita ambapo
majeshi ya Ethiopia yaliweza kuwasambaratisha wanamgambo wa kiislamu.
Kwa
upande wa Poland nchi ambayo Hayati Papa John Paul II alikuwa anatoka hakukubaliana
na utawala wa kikomunisti wa serikali ya Jenerali Jaruzeski na hatimaye papa
huyo alikiunga mkono chama cha wafanyakazi cha Solidarity kikiongozwa na Lech
Walesa ambacho hatimaye kilifanikiwa kuungusha utawala wa kikomunisti nchini
humo.
Yote
haya yanatufundisha kwamba ushawishi wa dini ni mkubwa sana katika siasa kwa
hiyo viongozi wa dini wanatakiwa kuwa makini katika uendeshaji wa mambo yao ili
isifikie mahali wao ndiyo wakawa vyanzo vya machafuko kama ilivyokuwa kwa
Sudani, Chechnya, Afghanstan n.k.
Miaka
ya nyuma kiongozi wa Italia Benito Mussolini aliona umuhimu wa kufanya
maelewano na viongozi wa Kanisa Katoliki na baadaye walisaini mkataba wa
maelewano (The Lateran Treaty , 1929)ambao hatimaye uliitambua Vatican kama mamlaka
kamili ndani ya Italia. Huo ni mfano tosha wa jinsi ambavyo serikali zinatakiwa
kushughulikia masuala ya dini kulingana na mazingira halisi.
Mvutano
uliopo sasa kimataifa ni kile kinachoitwa ubeberu wa kimarekani kupitia katika
utandawazi. Haishangazi kwamba Waislamu wa Nigeria walipinga mashindano ya
urembo yasifanyikie nchini mwao na badala yake yalihamishiwa Sanya nchini
China.
Yote
hiyo ni katika kuonyesha kwamba pande hizo mbili zimeshindwa kufikia muafaka
(dialogue) kuhusuana na tofauti zilizopo ambazo zinaweza kupata ufumbuzi na
kuondoa mivutano isiyo na tija.
Kwa
upande wa nchi za magharibi nazo hazijachoka kutoa nafasi kwa wakosoaji wa Uislamu
kama vile mwanamama Ayaan Hirsi Ali mkimbizi kutoka Somalia ambaye ameishi
nchini Uholanzi kuanzia mwaka 1992 akipinga ndoa ya lazima aliyopangiwa nchini
mwake.
Kwa
sasa mwanamke huyo anaandika mengi ambayo anayaona ni ukandamizaji wa dhahiri
wa mwanamke unaofanywa na dini ya kiislamu, mama huyo kwa sasa ni mbunge nchini
Uholanzi. Wapo wengine wanaomuunga mkono kama vile Naghem Khadhim wa Iraq na
Homa Arjomand wa Irani.
Kwa
hapa Tanzania mvutano uliopo si kwamba ni wa Waislamu na Wakristu pekee lakini
hata Wasabato ambao mara kadhaa wamekuwa wakilalalamika kwamba siku yao
haiheshimiwi, labda tatizo lililo dhahiri hapo ni kwamba ipo siku hata Waislamu
watadai kwamba Ijumaa iwe siku ya mapumziko kama ilivyo kwa Jumamaosi na Jumapili
sijui mwisho wa yote hayo utakuwa ni upi.
Kwa
hakika tunahitaji kukaa na kufanya maelewano ya kidini ili kupunguza mizozo
isiyo na manufaa vinginevyo tutafikia mahali pa kuanzisha vikundi vya kuziondoa
dini za kigeni (nihilistic movements), hapo ndipo tutakuwa tumefikia mwisho wa
amani yetu. Chonde chonde Watanzania tusifikie huko!
Lakini
kwa Mihangwa kama ameamua kurudi alikotoka na tumtakie safari njema, wasalimie
Mlungu na Kubeh!
Mwandishi
wa makala haya anapatikana kwa simu 0754 826 272, na Barua pepe: mhegeraelias@yahoo.com

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni