Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere alikaa Ikulu kwa zaidi ya miaka 20 na kuaondoka akiwa na mali za kawaida kabisa, leo Ikulu ni mahali pa watu kujitajirisha!
Oktoba 28, 2007 Mtanzania Jumapili
Na
Elias Mhegera
Kila
mfuatiliaji wa masuala ya kijamii katika vyombo vya habari nchini Tanzania
atakubaliana nami kwamba miongoni mwa habari ambazo zimegonga vichwa vya habari
vingi hususani katika magazeti katika siku za hivi karibuni ni tuhuma za
ufisadi zinazoelekezwa kwa rais mstaafu wa awamu ya tatu Benjamini Mkapa.
Nimeshawishika
kuchangia mawili matatu katika mjadala huo muhimu kwa maslahi ya taifa letu.
Labda
kabla hata sijaenda mbali katika mjadala huu naomba nieleweke wazi kwamba simo
katika kundi la wale wanaotaka iundwe tume kuchunguza tuhuma hizo za ufisadi
wake, sababu zangu ni kwamba ni dhahiri kufanya hivyo hakutatuletea tija yoyote
na badala yake tutaliingiza taifa katika gharama kubwa na mwisho wa siku
tutaambiwa hakuna ushahidi wowote kuhusiana na tuhuma hizo.
Lakini
pia naomba kutanabahisha kwamba mnamo mwaka 1995 Mkapa alipotajwa kwamba ni mtu
msafi ‘Mr. clean’ nilikuwa na wasiwasi mkubwa juu ya usafi huo. Hofu yangu
ilitokana na imani yangu kwamba kama kweli Mkapa alikuwa msafi basi alikuwa ni
mtu wa kipekee kwani mazingira ya wakati ule yalitoa mwanya mkubwa kwa viongozi
wengi kujilimbikizia mali kwa kile kilichoitwa kupunguza ‘ukali wa maisha’
Hofu
niliyokuwa nayo wakati ule ndiyo hiyo hiyo inayonitatiza juu ya uwezekano wa
kuundwa kwa tume huru inayoweza kuja na majibu ya uhakika na yanayoweza kukidhi
matarajio ya watanzania wengi juu ya tuhuma hizo ambazo zinafumuliwa kila
uchao.
Kwa
hiyo naona kuna uwezekano kwamba siasa za makundi zilizoibuka hivi karibuni
katika nchi yetu ndizo zinazochangia kufumuliwa kwa tuhuma hizo na inawezekana
wanaofanya hivyo hawana usafi wowote pia ni watu waliokuwa ndani ya mfumo huo
huo.
Naomba
nisieleweke kwamba namtetea Mkapa kwa namna yoyote ile isipokuwa nataka
kutanabahisha kwamba matatizo ya Mkapa ni matatizo ya mifumo tawala yote
isiyotaka kuachia madaraka (rigid systems) ambayo imesambaa takribani katika
bara letu zima la Afrika.
Kwa
lugha nyingine ni kwamba mfumo alioupokea na ule aliofanya nao kazi na baadaye
kukabidhi madaraka katika mfumo mpya lakini wa chama kile kile ni mazingira yanayoweza
kusababisha kwa mtu yeyote awaye kukengeuka kimaadili hata kama aliingia
madarakani akiwa msafi.
Kutokana
na kukaa madarakani kwa muda mrefu kwa chama kimoja lazima kuwepo na madhara ya
aina fulani kisiasa kama tunavyoshuhudia sasa hapa nchini mwetu.
Lakini
pia chama pekee si tatizo bali tatizo linakuja pale chama tawala kinapokosa
vyombo mahususi vya ukosoaji kama vile asasi za kiraia, vyombo huru vya habari
vyama vya dhati vya upinzani na mambo kadhaa yanayoweza kuweka mazingira ya
utendaji halali wa serikali iliyopo madarakani (legitimacy).
Ile
dhana kwamba huyu ni mwenzetu ambayo ilikuwa inatumiwa mara kadhaa na wanasiasa
wa chama tawala ilikuwa na mwangwi mbaya kwa sababu ilionyesha kwamba chama
kilikuwa tayari kulinda hata waovu kisa tu ni ‘wenzetu’siasa iligeuzwa kuwa
ajira ya kudumu badala ya kuthaminiwa kwamba utumishi wa umma ni jambo la
kujitolea tena kwa watu wasafi na wenye dhamira njema pekee na wala si kwa kila
awaye
Ni
hofu hiyo ndiyo ilinishawihi niamini kwamba kama kuna dhana ya huyo ni mwenzetu
maana yake kulikuwa na mazingira ya kuwalinda wale waliokuwa na hofu ya
kukabiliwa na mashtaka ya ufisadi kwa hiyo labda walimuona Mkapa kwamba ni mtu
ambaye asingediriki kuhatarisha maslahi ya watu wa aina hiyo.
Kwa
lugha nyingine mfumo wa awamu ya pili ndiyo hasa ulikuwa chimbuko lililojenga
mazingira ya ufisadi wa baadhi ya viongozi wetu, mazingira ambayo hayakuwepo
katika awamu ya kwanza ya Hayati Mwalimu Nyerere.
Kwa
kusema hivyo simaanishi kwamba ufisadi haukuwepo kabisa katika awamu ya kwanza
isipokuwa ulijengewa mazingira magumu ya kushamiri. Wenye nacho walijengewa
mazingira magumu ya kuonyesha ukwasi wao (extravagancy).
Hivyo
basi yawezekana kabisa kwamba viongozi wetu walianza kujichumia mali taratibu,
kimya kimya katika awamu ya kwanza lakini wakaonyesha kucha zao katika awamu
iliyofuata kutokana na ukweli kwamba mazingira yaliwaruhusu kufanya hivyo.
Kwa
maana hiyo kile kilichoitwa usafi wa Mkapa yawezekana kilitokana na ukweli
kwamba yeye binafsi kamwe hakuwahi kujidhihirisha kwamba alikuwa muathirika wa
ukwasi wa viongozi wa awamu ya pili jambo ambalo lilichangia kuanguka kwa
umaarufu wa kisiasa wa Mzee Ali Hassan Mwinyi.
Upo
pia uwezekano kwamba Mkapa alikuwa mtu msafi hadi wakati ule lakini aliharibiwa
na mfumo alioukuta kwa sababu hakuweza kufanya mabadiliko ya dhati kuwaondoa
viongozi ambao usafi wao kimaadili ulikuwa unatia mashaka.
Historia
inatuonyesha kwamba wapo viongozi ambao wamepata kuharibiwa na mifumo japokuwa
walikuwa na dhamira safi kabla ya kutekwa nyara na mafisadi na watu wenye
dhamira za kufanikisha mambo yao binafsi.La kushangaza ni kwamba historia
inatueleza kwamba hata watu kama Adolf Hitler ambao baadaye wamekuja kingizwa
katika safu ya madikteta wabaya kabisa waliopata kutokea hapa duniani nao
walianza kama watu wenye dhamira njema hadi pale walipotekwa nyara na watu
wenye maslahi binafsi.
Hadi
pale alipotoa kitabu chake ‘Mein Kempf’ (1925) yaani mapambano yangu bado
Hitler alikuwa bado ni mtu mwenye dhamira safi kabisa. Lakini dhamira hiyo safi
ya kuwatumikia wanyonge aliyokuwa nayo Hitler iliotekwa nyara na mabepari
waliohofia kutaifishwa mali zao iwapo utawala wa kikomunisti ungeingia
madarakani kwa hiyo mabepari hao ndiyo waliomteka nyara Hitler wakamgeza kuwa
chombo cha kulinda maslahi yao hususani mali na viwanda vyao.
Kuungwa
mkono huko kwa Hitler hakukuja kama bahati mbaya bali kulitokana na fundisho
walilopata kutoka kwa wenzao wa Urusi baada ya mapinduzi ya kikomunisti yaliyoendeshwa
na V.I. Lenini Oktoba 1917.
Katika
mazingira hiyo mabepari wa Ujerumani walikuwa na haki ya kulinda mali zao ili
zisije taifishwa na kuwekwa mikononi mwa umma kama ilivyojitokeza huko Urusi.
Hata hivyo Hitler huyo huyo baadaye aligeuaka na kuwa shubiri kwa kila mpenda
amani duniani yaliyofuata baada ya hapo ni historia ambayo inafahamika na
takribani na kila mmoja wetu.
Kwa
mantiki hiyo ndiyo maana nasema upo uwezekano kwamba Mkapa alikuwa mtu msafi kabisa
lakini alitekwa nyara katikati ya safari yake na kundi fulani la watu ambao
walikuwa wametanguliza maslahi yao binafsi.
Ni
kundi hilo ambalo limesababisha sasa aandamwe an tuhuma nyingi ambazo hata hivyo
hajawahi kuzikanusha kwa ukamilifu bali amekuwa akizizungumzia kijuujuu tu.
Kwa
hiyo kama tunajiaminisha kwamba mkapa alikuwa mtu msafi basi lazima tukubali
kwamba lipo kundi la watanzania wenzetu ambalo lilimpaka mawaa likamvuta katika
ufisadi, akajikuta ameangukia huko bila kutarajia.
Kwa
upande mwingine naweza kusema kwamba hatuna uhakika kama kundi hilo bado limo
ndani ya mfumo unaotawala sasa au la kwa sababu chama ni kile kile japo
yamefanyika mabadiliko hapa na pale.
Lakini
upo uwezekano pia kwamba kama kweli tuhuma zinazoelekezwa kwa Mkapa zina ukweli
basi labda msukumo ulitoka nje. Kwa
upande huo napenda niunge mkono hoja iliyotolewa na mwandishi mwandamizi
Lawrence Kilimwiko katika makala yake: Afrika Bado Haijawa Huru, Mwananchi, toleo namba. 02634 jumatano
Agosti 29, 2007.
Hoja
ya Kilimwiko katika makala yake ni
kwamba viongozi wetu wanaangukia katika ufisadi kwa sababu ya kukubali kutumiwa
kama maajenti wa maslahi ya nje.
Jambo
hilo linafanyika kwa lengo la kulinda
mikataba inayolinyonya bara letu au hata kwa lengo la kuanzisha mikataba mipya
ya aina hiyo. Kilimwiko anatahadharisha kwamba hicho ni chanzo kimojawapo cha
kushidikana kwa wazo la kuwa na serikali moja ya bara la Afrika.
Kwa
hiyo kama kuna ukweli juu ya tuhuma zinazoelekezwa kwa Mkapa basi tuziangalie
katika mtindo huo kwamba yawezekana amepotoshwa na kundi la mafisadi wa ndani,
wa nje au hata kwa ujumuisho wa makundi yote haya mawili la ndani na lile la
nje.
Hapo
ndipo kuna swali muhimu kwetu kwamba tupo tayari kuikabili na kuitokomeza mifumo
yote hiyo miwili ama tunataka tuishie kwa Mkapa peke yake?
Katika
kitabu chao Governance and Politics in
Africa (1992) waandishi Goran Hyden na Michael Bratton wansema tatizo
lililopo Afrika ni ile hali ya kupokea na kuanzisha siasa za ushindani ambazo
kwa kweli zimeonyesha kwamba bara letu lilikuwa bado halijaandaliwa vya kutosha
kwa siasa za aina hiyo. Matokeo yake ni kwamba vyama tawala vimeamua kuwabagua
wapinzani hata katika mambo ambayo ni ya kimsingi kabisa na yanatija kwa watu
wote bila kujali itikadi zao.
Mifumo
tawala ndiyo inajipa ukiranja wa usimamizi na ugawaji wa raslimali za taifa
hali ambayo imechangia kuwapo kwa mikanganyiko mingi na ufisadi.
Ni
katika mazingira hayo sasa tunaweza kutoa hukumu ya haki kwa Mkapa, kwa
kuzingatia suala la mifumo na misukukumo ya ndani na nje na wala siyo kwa
kumunyooshea kidole yeye binafsi, kwa hiyo tuanze na mifumo ndipo tumalize na
watu binafsi kama kweli tumedhamiria kupata ufanisi wa kudumu.
Ndiyo
maana mimi binafsi kama mwandishi sina sababu ya kumtetea Mkapa lakini pia
sioni sababu ya kundwa kwa tume ya kumchunguza kwa sababu kufanya hivyo ni
kuliingiza taifa katika gharama kubwa na mwisho wa yote hakuna lolote la maana
litakaloletwa na tume hiyo kama kweli itaundwa.
Sababu
nyingine ni kwamba lazima tuangalie kwamba serikali iliyopo madarakani ni ile
ile ya CCM. Kwa namna yoyote ile tuhuma zinazomhusu Mkapa (kama kweli zipo)
lazima zitawagusa pia baadhi ya watendaji wakubwa wa serikali iliyopo
madarakani kwa sasa jambo hilo linaweza kujenga mazingira ya kulindana.
Lakini
la muhimu zaidi ni kwamba pamoja na mapungufu yake rais huyo mstaafu ameacha
mambo kadhaa ya kimaendelo ambayo kwa sasa inaelekea yanasusua, hasa suala la
ujenzi wa barabara ambao ulikwenda kwa kasi nzuri ya kuvutia katika kipindi cha
uongozi wake.
Kwa
hiyo ni lazima tufahamu kwamba pamoja na mapungufu yake zikiwemo tuhuma za
kufanya biashara akiwa Ikulu, tuhuma nyingi si kwamba zinamgusa yeye pekee bali
zinaugusa mfumo mzima uliokuwepo madarakani katika kipindi chake wakiwemo
baadhi ya mawaziri ambao wamo katika awamu iliyopo madarakani kwa sasa.
Kama
vile hiyo haitoshi tushukuru pia kwamba mfumo wa Mkapa ulikuwa na uwazi na
uliruhusu kukosolewa jambo ambalo ni la muhimu katika ujenzi wa demokrasia na
ndiyo maana waandishi wa habari walikuwa na uhuru wa kukosoa kila walipojisikia
kufanya hivyo.
Kipindi
cha utawala wake Mkapa hakuwa na kikundi cha waandishi wa kumtetea bali alijibu
mapigo yeye binafsi kwa kadri alivyoona inafaa.
Ipo
haja ya rais wa sasa kuchota yale machache anayoona kwamba yatamfaa katika
uendeshaji wa serikali yake ya sasa. Kwa mfano ipo haja ya kupunguza ukubwa wa
serikali nikiwa na maana ya kwamba baraza la mawaziri ni kubwa kuliko mahitaji
halisi na uwezo wa nchi yetu kumudu gharama za mawaziri hao
Kinachojitokeza
sasa kinanifanya nikumbuke dhana zilizojengwa na mwanafalsafa wa kiitaliano kwa
jina Antonio Gramsci aliyeishi 1891-1937. Gramsci anayo machapisho mengi lakini
yanayokumbukwa zaidi ni yale aliyoandika alipokuwa gerezani kati ya mwaka
1925-35.kutokana na kupinga ukandamizaji nchini mwake.
Mwanafalsafa
huyo anazungumzia dhana nzima ya ukiritimba wa vyama kuhodhi madaraka kwa muda
mrefu kwa kuhakikisha kwamba wapinzani wote wenye nguvu wanamezwa ndani ya
vyama hivyo (co-optation), au vinginevyo wawe tayari kuangamizwa.
Anasema
mfumo tawala uliokaa madarakani kwa muda mrefu hufikia mahali ukachoka na
kushindwa kuleta mambo mapya lakini hubakia madarakani kwa kazi hiyo ya kujenga
himaya ya kisiasa (hegemony). Kwa hiyo kubakia madarakani ni zoezi linalopewa
kipaumbele kuliko mambo mengine yenye tija zaidi.
Mifumo
tawala hulazimisha makundi yote yenye nguvu kuunga mkono mfumo tawala kwa njia
mbali mbali ikiwemo kuunda tume na vyombo au itikadi zisizo na maana yoyote
zaidi ya kuwapofusha watawaliwa.
Katika
kutimiza hilo mfumo tawala hujenga mazingira ya kuungwa mkono kwa kila jambo,
hata asasi za kiraia, wasomi, viongozi wa dini waandishi wa habari wote huvutwa
ndani ya mfumo tawala kwa kutumia mbinu mbalimbali ili waunge mkono matakwa ya
watawala.
Kwa
bahati mbaya pale inapofikia kwamba makundi yote hayo yakagundua kwamba kuna
hadaa nyingi kuliko utendaji ndipo mapambano ya dhati huanza na mwishowe ni
kuzaa udikteta na ukandamizaji wa hali ya juu dhidi ya wote wanaotaka kujitoa
katika “himaya” hiyo.
Yawezekana
falsafa hiyo ya Gramsci ilitokana na kufungwa na utawala mbovu nchini mwake
lakini mawazo yake yanatupatia fundisho kwamba si jambo jema kwa kiongozi
kusifiwa sana au hata kumiliki madaraka makubwa kupita kiasi.Kama hatutaanza
sasa kurekebisha mambo tusishangae kuona hali hiyo ikijitokeza hata hapa kwetu
Tanzania.
Kinachonipa
hofu hiyo ni ukweli kwamba tumejenga mazingira magumu sana kwa rais aliyepo
madarakani kwa sasa kukosolewa. Takribani kila kundi kubwa limemezwa ndani ya ‘mtandao’
uliofanikisha zoezi la kumuingiza madarakani Rais Kikwete. Hali hiyo si ishara
nzuri katika ujenzi wa demokrasia.
Tunaona
kwamba makundi mbalimbali yameguswa katika teuzi mbalimbali baada ya uchaguzi
mkuu uliopita. Viongozi wa taasisi, madaktari, waandishi wa habari, wahadhiri
wa vyuo vikuu, wasanii, n.k. wote wamemezwa ndani ya mfumo tawala.
Mazingira
tuliyonayo ambapo kila inapojitokeza mwandishi mmoja akaukosoa mfumo tawala
basi hushambuliwa vilivyo na kundi jingine la waandishi ambao kwa haraka haraka huzima
hoja yoyote ile isiyoufurahisha mfumo tawala. Hii si njia muafaka katika ujenzi
wa demokrasia.
Waandishi
hao wenye kuwashambulia wenzao wananifanya niamini kwamba Rais Mstaafu Mkapa
alikuwa sahihi zaidi kwa kuruhusu kukosolewa na kujibu mapigo yeye mwenyewe
pale alipoona inastahili kufanya hivyo.
Nadhani
sasa ni muda muafaka kila amtakiaye rais wetu mema afanye hivyo kwa kuzingatia
pande zote mbili yaani kupongeza pale inapostahili na pia kukosoa inapobidi
kufanya hivyo.
Ni
dhahiri kwamba kama tutaendeleza tabia ya kumpamba rais kila uchao badala ya
kumsahihisha pale tunapohitajika kufanya hivyo kwa njia ya kumkosoa basi
tutakuwa tunambomoa badala ya kumjenga.Vyombo vya habari ni viunganishi kati ya
watawala na watawaliwa tuache vitimize jukumu hilo.
Naungana
mkono hoja ya wale wanaosema Mkapa aachwe apumzike kwa sababu utamaduni wetu wa
kisiasa hauonyeshi kama kweli kuna jambo lenye manufaa litakalopatikana baada
ya kumchunguza zaidi ya kupoteza bure pesa za walipa kodi, na tumuache Mkapa
apumzike aliyotutendea yanatosha aliyotukosea basi tumsamehe.
Mwandishi
wa makala hii anapatikana kwa simu 0754 826 272
Barua
pepe: mhegeraelias@yahoo.com

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni