Mkuu wa Jeshi la Polisi Mstaafu Said Mwema
JESHI LA POLISI WAZINGATIE MAADILI
WARUDHISHE IMANI YA WANANCHI
Novemba
04, 2007 Mtanzania Jumapili
Na
Elias Mhegera
Siku
ya Jumamosi tarehe 20 Oktoba mwaka huu wananchi wa kijiji cha Ilongero mkoani
Singida walijichukulia sheria mikononi, wakavunja kituo cha polisi kwa lengo la
kumsulubu mtuhumiwa wa ubakaji na mauaji aitwaye Mile ambaye hatimaye wananchi
hao walimuua.
Mkuu
wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Inspekta Jenerali wa Polisi Said Mwema ametoa
tamko kali kukemea kitendo hicho cha wananchi hao, nami nimeona ni muhimu
kulizungumzia suala hilo.
Katika
vipindi vingi vya matukio katika redio zetu na hata katika habari zitolewazo
magazetini matukio ya ukatili yamekuwa yakijitokeza kwa kiwango kikubwa na cha
kutisha.
Mara
kadhaa kumekuwapo na ripoti zenye kuleta simanzi kwa sababu ya watu kufanyiana
vitendo viovu vya ukatili, kuuana na mambo kadhaa yasiyopendeza ili mradi kila
jambo baya la aina hiyo hutokana na utovu wa maaadili kwa namna moja au
nyingine.
Nimeshawishika
kuandika makala hii ili nitoe mchango wangu mdogo katika jamii katika
kuimarisha amani na utulivu.
Kwa
namna yoyote ile katika dunia ya waungwana tunayojitahidi kuijenga hatuwezi
kuruhusu kitendo kama kile cha wananchi wa Ilongero.
Lakini
kwa upande mwingine napenda kutanabahisha kwamba tukio la Ilongero linaonyesha
kwamba kulikuwa na mazingira ya uzembe kwa mamlaka husika ambayo hatimaye
yalisababisha wananchi wakaamua kujichukulia sheria mikononi mwao kwani mhusika
alikuwa amewahi kufikishwa kituoni hapo mara kadhaa na kuachiliwa huru katika
mazingira ambayo yaliwatatiza wananchi wa kijiji hicho.
Lakini
tukio la Ilongero linaashiria kwamba kama mamlaka husika hazitachukua hatua
madhubuti katika muda muafaka ipo hatari ya wananchi kuendelea kujichukulia
sheria mikononi.
Ni
mara kadhaa wananchi wamekuwa wakitoa malalamiko kwamba wapo baadhi ya wahalifu
ambao mara wafikishwapo katika vyombo vya dola kama vile Jeshi la Polisi na
mahakamani huachiliwa huru kwa madai kwamba hapakuwa na ushahidi wa kutosha
kuweza kuwaweka hatiani watuhumiwa hao.
Athari
za muda mrefu ni kwamba watu hao hurudi mitaani wakaendeleza uovu wao na hata
wakati mwingine huwatambia wananchi kwamba wao kamwe hawawezi kuguswa na dola.
Nashawishika
kuamini kwamba upo ufa mkubwa katika utendaji wa vyombo vyetu vya dola ambao
usipozibwa matukio kama hilo la Ilongero yataendelea kujitokeza mara kwa mara.
Sehemu
kubwa ya matukio ya namna ile yamechangiwa na utovu wa maadili si kwa wanajamii
pekee bali hata kwa watendaji katika vyombo vya dola ambao hukubali kupokea
hongo na kuwaachia huru wahalifu.
Yapo
masuala kadhaa yanayolalamikiwa mara kwa mara na wananchi kuhusiana na
kukengeuka kwa maadili ya kitaaluma kwa baadhi ya askari katika Jeshi la Polisi
kwa mfano tukio la hivi karibuni la askari polisi kumuibia mwenzake silaha
akiwa lindoni, ama hata baadhi ya askari polisi kuwafichiua watoa habari
(whistleblowers), haya ni mambo yanayolivunjia heshima jeshi hilo katika jamii.
Kwa
hali yoyote ile iwapo Jeshi la Polisi au hata mahakama zetu hazitarekebisha
baadhi ya mienendo na kukidhi matakwa na mahitaji basi tutaendelea kushuhudia
vitendo vya uvunjaji wa sheria kwa wananchi kujichukulia sheria mikononi kama walivyofanya
wananchi wa Ilongero hivi karibuni. Lakini tukio hilo ni muendelezo tu wa
matukio ya aina hiyo ambapo mara kadhaa wananchi hujichukulia sheria mikononi na
kuwachoma watu moto kwa kuwavalisha watu matairi na baadaye kuwachoma moto kwa
kutumia petrol mafuta ya taa n.k.
Ndiyo maana katika makala zangu kadhaa nimekuwea
nikisisitiza kwamba iwapo mamlaka halali zitashindwa kutimiza wajibu wao basi walizi
wa maadili watajitokeza na kuifanya kazi hiyo.
Walinzi hao wa maadili ninaowazungumzia hawaishi katika
ombwe (vacuum) bali ni sisi wenyewe pale inapofikia kwamba tumechoshwa na uovu
tukaamua kuirudisha jamii katika mstari unaostahili. Siku zote wanadamu
wanapofikia hatua hiyo ni kwa sababu wanakuwa wamekatishwa tamaa na mifumo
halali inayotakiwa kushughulikia masuala hayo.
Mtuhumiwa
aliyeuawa aliyefahamika kwa jina la Mile alikuwa na uzoefu wa uhalifu.
Kulingana na maelezo ya wananchi wa Ilongero waliyoyatoa kwa Mbunge wa Jimbo la
Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu mtuhumiwa huyo aliwahi kufikishwha kituoni
hapo mara tatu kwa tuhuma mbalimbali na mara ya mwisho alitoroka baada ya
kuvunja dirisha kituoni hapo.
Wananchi
hao walidai kwamba mtuhumiwa Mile amewahi kuhusika katika vitendo vya ubakaji
kwa zaidi ya wanawake sita kijijini akiwemo mama yake mzazi! Kabla ya kuwabaka
watoto wa familia moja hadi kuwaua. Inadaiwa pia mtuhumiwa huyo wa ubakaji pia
alimbaka mwalimu wa wanafunzi hao katika shule ya msingi Mlama.
Ilidaiwa
kwamba akina mama waliobakwa waliogopa kutoa taarifa kwa kuona kwamba jambo
hilo lingewafedhehesha katika jamii yao. Ukimya wa akina mama hao ndio uliompa
kiburi mtuhumiwa huyo wa ubakaji akashirikiana na mtuhumiwa mwenzake aitwaye
Hamisi Juma na wakatenda tendo hilo la kinyama tarehe 14 ya mwezi Oktoba hadi
kusababisha vifo vya mabinti hao.
Hasira
na uchungu wa kupoteza watoto wao wapendwa viliwafanya wananchi hao wa Ilongero
wapoteze subira na hatimaye wakaamua kuikamilisha kazi ambayo tayari waliona
isingefanywa katika kiwango walichoona wao kinastahili kwa wauaji hao.
Kwa
sasa baadhi wa wanakijiji hao akiwemo mwenyekiti wao Issa Swedy wameshikiliwa na
dola kutokana na kujichukulia sheria mikononi mwao na kuwaua watuhumiwa wao.
Hata
hivyo mbunge wao Nyalandu ameliomba Jeshi la Polisi pamoja na kuwakamata
wanakijiji hao nalo kwa upande wake liwajibike kwa kutoa maelezo ya kina juu ya
kutoroka na kuachiwa mara kwa mara kwa mtuhumiwa huyo. Ni dhahiri hapo kuna
tatizo kubwa ambalo sisi kama wanajamii inatubidi tukune vichwa na kuangalia
namna ya kuyazuia matukio ya namna ile yasije tokea tena katika jamii zetu.
Labda
tunaweza kuanza kwa kujifanyia tathmini ya viwango vyetu vya maadili na kutafuta
jinsi ya kurekebisha mapungufu tuliyonayo.
Maadili
ni mfumo wa uhalalishaji wa matendo mema na kwa upande mwingine kuyakataa
matendo yote mabaya. Kwa kifupi maadili ni dhana pana inayohusu uchanganuaji wa
mema na mabaya.
Labda
tatizo lililopo ni kudhania kwamba maadili ni yale tu yaliyoandikwa katika
vitabu vya kigeni na kwamba sisi waafrika hatuna maadili yetu au labda
hatujawahi kuwa nayo isipokuwa yale yaliyoletwa na wakoloni, wamisionari
wafanyabiashara wa kiarabu walioleta uislamu Afrika na mambo kama hayo.
Ni
muhimu tukafahamu kwamba nasi tuna maadili yetu ambayo yamejikita katika mila,
desturi na tamaduni zetu. Kwa mfano kile kinachoitwa miiko ni msingi thabiti wa
maadili ya muafrika, kwa maana hiyo kwa sababu miiko imekuwepo siku zote katika
jamii zetu, basi kumbe inadhihirisha kwamba maadili yetu yamekuwepo pia tokea
enzi za mababu zetu.
Matukio
ya watu kuuana wakigombea mwanamke, au kufumaniana ugoni, kuchomeana ndani ya
nyumba, kuwaadhibu wasiostahili, kwenda kinyume cha taratibu za jamii, visasi
kuwekeana vikwazo, ubaguzi wa rangi, unyanyapaa, kuathiriana kisaikolojia,
kughushi malipo, kuwaingiza wenzetu katika mikataba ya uongo, kutumia madaraka
vibaya yote haya ni utovu wa maadili ambao huchangia katika matukio ya
kudhuriana kila uchao.
Lakini
matukio yote yaliyotajwa hapo juu yanaweza kuzuilika iwapo tutazingatia maadili
ambayo tunarithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kabla hata ya kufikiria
kwenda darasani kwa ajili ya somo la maadili.
Katika
mila zetu za kiafrika maadili yalitokana na umoja wa kifamilia kwa sababu koo
mbalimbali ziliishi katika eneo moja katika mfumo wa ukoo, koo kadhaa na
hatimaye kijiji. Kwa maana hiyo kijiji kimoja au vijiji kadhaa vilitokana na
koo zenye kushabihiana katika lugha (kabila), mila na desturi, na kwa maana
hiyo maadili yao yalifanana.
Maadili
yenyewe yalirithishwa kwa njia ya imani, sherehe za kimila, nyimbo hadithi na
simulizi mbalimbali. Kwa ujumla maadili yaliyokuwepo yalitegemeana sana na
tafsiri ya mazingira na matukio yaliyojitokeza katika jamii husika. Kwa mfano
kuzaliwa kwa mtoto, maradhi, vifo, mazishi, n.k.
Kila
jamii ililinda maadili yake kutegemeana na shughuli zilizoizunguka jamii hiyo
kama vile kilimo, ufugaji, uvuvi, uhunzi n.k. Kwa maana hiyo hata miungu
walioabudiwa walitokana na mazingira husika. Kwa maana hiyo kulikuwa na miungu
wa mvua, mavuno, tiba, amani, n.k.
Maadili
hayo ya kiafrika ndiyo yaliyowatuma waafrika wachague mlo wa aina fulani,
makazi yao, mavazi, namna ya kufunga ndoa kuwapokea watoto wanaozaliwa, kuzikana
na namna ya kukabiliana na majanga mbalimbali katika jamii husika.
Kimsingi
katika maadili ya kiafrika hakuna eneo lililokuwa limetelekezwa kwani kila
jambo lilikuwa na majibu yake tayari tayari. Kwa maana hiyo watu walikuwa
wamejiwekea tayari utaratibu wa kukabiliana na majanga yoyote ambayo
yangejitokeza mbele yao.
Kulikuwepo
na taratibu za kurekebisha ndoa, mahusiano ya kawaida katika jamii namna ya
kukabiliana na misukosuko mbalimbali ya kimaisha, kuvumbua dawa, matumizi ya
ardhi, matumizi ya alama na ishara mbalimbali, masuala ya posa na utoaji wa
mahari n.k. Mambo yote hayo yalilenga katika utoaji wa maamuzi sahihi mara
yanapojitokeza mapungufu fulani.
Lakini
pia ni katika maadili hayo hayo ndipo ulipopatikana mgawanyo wa majukumu
mbalimbali ya kijamii na kazi. Kulikuwepo na misemo mbalimbali na tungo zenye
ujumbe murua katika kila tukio husika.
Kwa
bahati mbaya imani za kishirikina pia zilitawala sana katika jamii zetu na ndiyo
maana kila jamii ilikuwa na madawa kwa ajili ya kujilinda na maadui zao.
Kinachojitokeza
katika matukio ya sasa ambayo yanaripotiwa na vyombo vya habari kila siku ni
kupotea dira au muelekeo wa maadili yetu ambako kumechangiwa kwa kiwango fulani
na kuhama hama kwa ajili ya kutafuta maslahi.
Kuja
kwa ukoloni na dini za kigeni ambazo zote zimeyakandamiza maadili yetu kwamba
ni ya kishenzi na kwa maana hiyo mvurugiko huo ndiyo unaochangia katika matukio
mabaya yanayosababisha watu wachinjane kama kuku kila uchao.
Kwa
hiyo ni lazima tufahamu kwamba kuna ombwe (vacuum) kati ya maadili yetu na yale
ya kigeni au wakati mwingine ni kwa sababu watu wa makabila mbalimbali wanafunga
ndoa au hata kuingiliana kijamii bila kufahamiana vizuri kwanza.
Kwa
hiyo kuna umuhimu wa kuwianisha maadili yetu (dialogue) ili kuondoa migogoro
isiyokwisha na pia ili tupate dira moja inayokidhi mahitaji yetu sote kwa
pamoja.
Si
lengo la makala hii kuzungumzia maadili katika kila taaluma au kuingia kwa
undani sana juu ya dhana ya uadilifu, bali lengo ni kuyazungumzia maadili
katika ujumla wake na kuangalia vyanzo vya matatizo katika jamii zetu na
hatimaye kutoa ushauri wa nini kifanyike ili kurekebisha hali iliyopo kwa sasa,
yaani kilio cha utovu wa maadili.
Ni
vyema basi tukagusia maadili kama yanavyotazamwa na wenzetu wageni: wao
wameyagawa katika sehemu kuu tatu; metaethics,
normative ethics, na applied ethics.
Makala hii imelenga katika kuyachanganua maadili haya kama yanavyotazamwa na
wenzetu na kutoa tafsiri yake katika mazingira yetu.
Metaethics ni dhana ya kimaadili inayo chunguza vyanzo vya
maadili, maana zake, dhana ya ukweli na utashi wa Mungu katika yale
tuyatendayo. Normative ethics ni
dhana inayozungumzia matendo zaidi na pia namna ya kurekebisha matendo hayo na
kutoa mwelekeo mzuri zaidi.
Kwa
upande mwingine applied ethics ni dhana
inayozungumzia au kuangalia, kuchunguza, au kupima matendo yasiyo ya kawaida
katika maisha ya jamii zetu. Kwa mfano utoaji wa mimba, ushoga, na usagaji,
masuala ya mazingira kama vile ukataji wa miti ovyo, kuchoma misitu, adhabu ya
kifo n.k.
Baada
ya kujadili maadili ni nini, na kuwianisha maadili yetu ya kiafrika na yale ya
kigeni, ni vyema sasa tukajadili ni kwa nini hutokea watu wakakiuka maadili
japo wakati mwingine wanayafahamu, na pia wanazijua fika athari za kukiuka
maadili hayo.
MAZINGIRA YA
MAAMUZI
Japo
hakuna dhambi inayohalalishwa kwa namna yoyote ile lakini hujitokeza kwamba
binadamu akayumbishwa kisaikolojia na kujikuta katika mazingira yanayoweza
kumfanya akiuke maadili. Tukio la mauaji la Ilongero linaweza kuhusishwa na
suala la mazingira ya maamuzi yaani uchungu wa kupoteza watoto na hasira kali
ya wananchi
Kwa
mfano binti aliyemaliza darasa la saba akajikuta haendelezwi kwa njia yoyote
ile, hapati taaluma, wala ajira rasmi ni rahisi sana kwake kuhalalisha
kujiingiza katika biashara mbaya ya ukahaba. Japo binti huyo anaweza
asifurahishwe sana na uamuzi wake huo lakini anaweza kuwa na kisingizio kwamba
hakuwa na njia nyingine mbadala ya kujikimu katiaka maisha yake.
UBINAFSI
Wapo
watu wengi katika jamii zetu waliotawaliwa na ubinafsi bila kufahamu kwamba
kufanya hivyo ni kukiuka maadili. Hii ni kwa sababu mara nyingi watu wa aina
hii hujitahidi kukwamisha mambo ya wenzao kila wanapoona kuna dalili za
mafanikio fulani, watu wa aina hii hudhania kwamba ni wao pekee wanaostahili
kupata.
Kama
hiyo haitoshi kundi la watu wa aina hii husumbuliwa sana na ghiliba na roho za
kwa nini kwa wale wenye upeo mkubwa au wenye tabia ya kujihangaisha katika
kutafuta maendeleo (aggressive). Watu wa aina hii hawakawii kuwadhuru wenzao
pale wanapoona kuna dalili njema mbele yao.
Katika
kundi la watu wenye tabia kama hizi ndiyo tunasikia vifo vya mara kwa mara
kutokana na kutaka kuzibiana ridhiki. Yapo mambo kadhaa yanayoambatana na
ubinafsi kama vile kuchongeana na hata kulishana sumu. Mambo ya aina hii hutokea
sana kwa wafanyabiashara, wanasiasa na viongozi katika taasisi mbalimbali
wanaotaka kutukuzwa.
HASIRA NA PAPARA
Kuna
nyakati ambapo watu hukiuka maadili kwa sababu ya kulipiza visasi, na maamuzi
ya pupa. Kwa mfano wapo akina mama ambao huamua kuanzisha mahusiano na rafiki
za waume zao pale wanapojiona kwamba hawakutendewa haki lakini mara nyingi
maamuzi kama hayo huwashushia heshima zao mbele ya jamii badala ya kutatua
tatizo linalowakabili.
Hali
ya visasi vya namna hiyo inaweza pia kufanywa na mwanaume dhidi ya mke wake au
hata kwa wachumba ambao bado hawajafunga ndoa. Wakati mwingine visasi vya namna
hii huchangiwa sana na wazazi, mawifi
mashemeji na marafiki wa karibu wa wapenzi hao kwa kuanzisha chokochoko
zisizokuwa na maana yoyote wala tija kwa wapendanao.
Wakati
mwingine watu hujiingiza katika utovu wa maadili baada ya jamii kuwatolea
hukumu isiyostahili kwa mfano binti aliye masomoni apatapo mimba husutwa na
kuitwa majina mabaya ambayo yanaweza kumvunja moyo na kumfanya ajitumbukize
katika vitendo viovu.
Hiyo
utokea baada ya kuona kwamba jamii haikumtendea haki. Mambo kama haya pia
huwakuta watu wenye ugumba ambao huhukumiwa na jamii katika namna inayowaumiza
sana na kuwaelekeza katika vitendo viovu katika namna ya kujiliwaza.
ULAZIMISHAJI
Japo
hali ya ulazimishaji wa ndoa imepungua kwa kiwango kikubwa lakini bado kuna
watu ambao wana tabia za kuwalazimisha watoto wao wa kike na wakiume kuingia
katika ndoa bila hiari zao na matokeo yake ni kusababisha misuguano isiyoisha,
uzinzi, visasi kushambuliana n.k.
MALEZI DUNI NA KUTOWAJIBIKA
Malezi
duni ndiyo chimbuko la maovu mengi tunayoyashuhudia katika jamii zetu, iwapo
tunaajiri watu wenye malezi duni toka nyumbani tunajenga mazingira ya kuwa na
watumishi waovu.
Malezi duni huanzia katika familia moja moja
lakini baadaye huathiri taasisi, mashirika na mwisho wa yote ni ubadhirifu wa
mali ya umma ukatili, unyama, fitina na majungu. Labda hapo ndipo tunapoona
umuhimu wa dini katika kujenga maadili mema kwa familia zetu.
Kuwajibika
kwa mtu yeyote kunatokana na mambo kadhaa, kwa mfano nidhamu binafsi ya maisha,
majukumu aliyokabidhiwa katika jamii kulingana na wakati husika lakini mara
nyingi suala la kuwajibika linamhusu zaidi mtu mmoja mmoja yeye na nafsi yake.
Kwa
mfano ni vipi mtu anawajibika kwa wazazi wake, kwa jamii yake, kwa taifa lake,
kwa dini yake, kwa familia yake, au hata kwa nafsi yake mwenyewe. Kutowajibika
ndicho chanzo kikubwa cha utovu wa maadili na katika hilo wahusika wanaweza
kuwa wataalamu kama vile waalimu madaktari, waandishi wa habari, wachungaji,
askari polisi n.k.
UDHALILISHAJI
Udhalilishaji
upo wa aina nyingi kwa mfano kutowatambua watu wenye vipaji maalumu husababisha
wakate tamaa na wakati mwingine wajiingize katika vitendo viovu kama njia ya
kujiliwaza kama vile ulevi wa kupindukia, udhalilishaji ni pamoja na kuwanyima
nafasi za kujiendeleza watumishi ambao wameonyesha dhamira hiyo na pia
kukwamisha bahati zao fulani fulani.
Udhalilishaji
ni pamoja na kuwabagua wenzetu katika misingi ya dini, rangi, kabila, kutotimiza
ahadi zetu kwao, ikiwa ni pamoja na kuwanyima haki zao za kimsingi. Kwa mfano
muajiri anayedai rushwa ya ngono kwa binti au mwanamke hiyo ni aina mojawapo ya
udhalilishaji. Wakati mwingine hujitokeza watu wakakwamisha biashara za wenzao
katika misingi hiyo hiyo ya chuki na udhalilishaji.
NINI BASI KIFANYIKE ILI KUREKEBISHA HALI
HIYO?
Jambo
la muhimu sana ni kuwa wakweli katika kila jambo tulitendalo, yaani kuwe na
uwazi, bila kificho chochote. Tujue kutubu na kuwaomba radhi wenzetu mara
tuwakoseapo.
Ni
jambo jema hata kulipa fidia pale unapoona umemuathiri mwenzako kwa njia moja
au nyingine. Kwa lugha nyingine haitoshi kwa (IGP), kuonyesha tu kwamba Jeshi
la Polisi linao uwezo hata wa kuua pale linapokwamishwha katika kutimiza
majukumu yake bali pia aonyeshe ni kwa jinsi gaini jeshi hilo litarudisha imani
ya wananchi kwa jeshi hilo.
Tujenge
utamaduni wa kuwa na shukrani na fadhila kwa wenzetu, kwa mfano mtu asiyetambua
umuhimu wa kuwashukuru waliomsaidia katika jambo fulani huwavunja moyo watu hao
na kusababisha wasitoe misaada kama hiyo kwa wengine.
Kwa
upande mwingine tusitegemee kupewa shukrani kila tunapotenda wema kwani inaweza
kujitokeza kwamba mara unapomtendea wema mtu utalipwa kwa njia nyingine na mtu
tofauti kabisa na wakati mwingine mahali usipopategemea kabisa.
Mwisho
kabisa tujenge tabia ya kuheshimu misingi iliyowekwa na jamii kama vile
kushiriki katika misiba ya wenzetu, sherehe mbalimbali, kama vile arusi,
kuwatembelea wagonjwa, tuheshimu sheria na taratibu za nchi tukiyazigatia yote
haya matukio maovu ya watu kuuana na kudhuriana ya tatokomea mara moja.
Wakati
tukiwa bado na kumbukumbu ya tukio la Ilongero ni muhimu pia tujiulize
mtuhumiwa wa ubakaji alikuwa ni mtovu wa maadili wa kawaida au upo uwezekano
alikuwa ameathirika pia kisaikolojia (psychopathy).
Vitendo
vya mtuhumiwa huyo vinaashiria kwamba kuna uwezekana kwamba alikuwa na matatizo
ya kisaikolojia labda kutokana na ukatili aliofanyiwa na wanadamu wenzake siku
za nyuma ndipo naye akaamua kulipiza kisasi kwa njia hiyo aliyoitumia?
Nakaribisha mawazo yenu
Mwandishi
wa makala hii anapatikana kwa simu: 0754 826 272
Na
kwa barua pepe: mhegeraelias@yahoo.com


