Ijumaa, 18 Julai 2014

CHISSANO NA TUZO YA MO IBRAHIM JE KUNA SIASA NYUMA YAKE?

Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili Msumbiji Mzee Joachim Chissano 


Makala hii ilitumika katika gazeti la Mtanzania Jumapili mnamo tarehe 11 Novemba mwaka 2007

Na Elias Mhegera,
Baada ya Rais Mstaafu wa Msumbiji Joachim Alberto Chissano (68), kutangazwa kwamba ndiye mshindi wa kwanza wa tuzo ya Mo Ibrahim ya uongozi bora zimezuka hoja kadhaa miongoni mwa watanzania na labda hata nje ya nchi yetu.

Baadhi ya wale wanaohoji ni ambao hawaoni umuhimu wa tuzo yenyewe na pia lipo kundi ambalo linashindwa kuelewa vigezo vilivyotumika kumpatia tuzo hiyo kiongozi huyo mstaafu, hiyo ndiyo mada ya makala haya.

Chissano amejinyakulia kitita cha Dola milioni 5 za kimarekani labda niwe wazi kwamba dhamira yangu si kujikita katika mjadala wa tuzo yenyewe bali zaidi kuangalia umuhimu wa tuzo hiyo kama upo na kama kweli Chissano alistahili au labda aliyestahili kupata tuzo hiyo ni Mkapa kama baadhi ya watanzania walivyotarajia.
Kwanza nasema tuzo hiyo ni muafaka kwa lengo la kujenga demokrasia, haki za binadamu na utawala bora kwa ujumla.

Vile vile napenda tujadili juu ya uhalali wa Chissano kupokea tuzo hiyo na kwa nini Mkapa hakuipata, tuwaweke katika mizani na kuangalia kama vigezo vilivyotumika ni sahihi bila kusahau nguvu ya ushawishi ya wale waliokuwa katika jopo la uteuzi.

Kabla hatujawalinganisha viongozi hao wawili yaani Mkapa na Chissano ni vyema tukajadili japo kwa uchache kuhusu hoja mbali mbali zilizotolewa kuhusiana na tuzo yenyewe.

Alfajiri ya Alhamisi tarehe 25, Oktoba 2007 nilisikiliza mjadala ulioendeshwa kati ya BBC na Dkt. Azaveri Lwaitama wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuhusiana na tuzo hiyo.

Dkt. Lwaitama alitoa changamoto kwamba tuzo hiyo ilitakiwa ibadilishwe mfumo wake ili wahusika watokane na viongozi wote waliopata kuongoza Afrika kuanzia enzi ya akina Julius Nyerere, Kwame Nkrumah, Kenneth Kaunda, hadi waliostaafu hivi karibuni kama Mzee Nelson Mandela.

Kwa mtazamo wake walengwa wa tuzo hiyo walikuwa hawakidhi viwango na kwa maana hiyo Chissano alikuwa bora miongoni mwa hao ‘bora viongozi’ na wala siyo viongozi bora.

Kama hiyo haitoshi Dkt. Lwaitama alisema lengo lisingekuwa kuwapatia mamilioni ya pesa viongozi hao ambao tayari wanazo pesa nyingi na badala yake pesa hizo zingeelekezwa kwenye taasisi zao ili kuwasaidia wenye mahitaji kama vile ‘scholarship’, huduma za kijamii n.k.

Sipingani na mawazo hayo ya Dkt. Lwaitama lakini napenda kumkumbusha kwamba waingereza wanayo methali isemayo ‘amlipaye mpiga zumari ndiye huchagua wimbo’ –‘He who pays the piper, calls the tune’.

Kwa maana hiyo mtoaji wa tuzo hiyo ndiye alikuwa na kauli ya mwisho kwamba tuzo hiyo iwalenge watu wa aina gani. Kwa hiyo kama huo ndio ulikuwa utaratibu, na viongozi 13 wastaafu wa kiafrika wakaingizwa katika kinyang’anyiro hicho basi ni muhimu tukawajadili hawa wawili kwa sababu wanatuhusu zaidi.

Chissano ni kwa sababu tayari amefungua njia kwa kupokea tuzo hiyo, na Mkapa ni kwa sababu alikuwa rais wetu watanzania.

Lakini pia ni muhimu tuwafahamu baadhi ya viongozi waliongizwa katika kapu hilo la marais wastaafu 13 waAfrika: Ukiwaondoa Mkapa na Chissano wengine ni pamoja na Kumba Yala wa Guinea Bissau, Maaouiya Ould Sid Ahmed Taya wa Mauritania, na Mathew Karekou wa Benin.

Wengine ni Albert Rene wa Seychelles, Gnasingbe Eyadema wa Togo, Bakili Muluzi wa Malawi miongoni mwao watano waliingia madarakani kwa njia ya mapinduzi ya kijeshi. Eyadema amewahi kupindua serikali mara mbili na pia inadaiwa kwamba alihusika katika mauaji ya Sylvanus Olyimpio rais wa kwanza wa Togo.

Baada ya kuizungumzia tuzo yenyewe; ni vyema tuwazungumzie pia wahusika katika jopo la uteuzi. Walengwa wangu katika hili ni Katibu Mkuu Mstaafu wa Umoja wa Mataifa. Kofi Annan na Katibu Mkuu Mstaafu wa Umoja wa Nchi za Afrika (OAU/AU), Dkt. Salim Ahmed Salim.

Wengine ni Rais Mstaafu wa Ireland Mary Robinson, Rais Mstaafu wa Finland Martti Ahtisaari, Waziri wa zamani wa Uchumi wa Nigeria Ngozi Okonjo Iweala.

Kabla sijawazungumzia Chissano na Mkapa napenda tumchambue Kofi Annan Katibu Mkuu Mstaafu wa Umoja wa Mataifa. Kupatikana kwake katika nafasi hiyo kulikuja baada ya shinikizo kubwa la Marekani la kumzuia Dkt. Boutros Boutros Ghali asigombee ukatibu huo kwa mara ya pili.

Nchi kadhaa za kiafrika zilishinikiza kwamba arejee tena lakini jitihada hizo ziligonga mwamba na ndipo akaenguliwa na nafasi hiyo ikachukuliwa na Dkt. Kofi Annan mwaka 1996.

Shinikizo la kumuondoa Dkt. Boutros Ghali na kuingizwa kwa Kofi Annan kwa mchunguzi yeyote makini kunaonekana kulipangwa na wamarekani labda kwa kudhania kwamba muda wote Annan angeendelea kuwa mtiifu kwao japo katika utendaji wake kuna nyakati hakusita kuwakemea wamarekani kwa kuugeuza umoja huo kama mhuri tu wa kutimiza haja zao…
Kofi Annan alikuwa mfanyakazi wa Umoja wa Mataifa wa muda mrefu lakini hakuwa mwakilishi wa nchi yake, Ghana, bali alikuwa mwajiriwa wa kawaida (civil servant) ndani ya umoja huo kwa kujitafutia ajira hiyo yeye mwenyewe binafsi.

 Uteuzi wake uliambatana na minong’ono kutoka kwa baadhi ya viongozi wa kiafrika kwamba walikuwa wamesalitiwa kwani walimuona Annan alikuwa ‘mkimbizi’ aliyeliasi bara lake la Afrika akaoa ugenini na kuyahamishia makao yake ya kudumu Amerika na akalisahau bara lake la Afrika, walimuona ni mtu aliyekwisha hamishika kifikra (uprooted).

Tukiachana na Annan tumzungumzie Dkt. Salim Ahmed Salim huyo ni Mtanzania kutoka Pemba mahali ambako ndiko kumeathirika zaidi na mtafaruku wa Zanzibar ambao Mkapa rais wetu mstaafu alishindwa kuutatua.

Salimu pia anashikilia rekodi ya katibu mkuu wa OAU/AU aliyekaa kwa muda mrefu zaidi katika utumishi wake. Katika nafasi hiyo Salim Ahmed Salim alikaa katika wadhifa huo kwa kipindi cha miaka 12 akiwa anakaribiwa kwa karibu kwa rekodi hiyo na katibu mkuu wa kwanza wa umoja huo marehemu Diallo Telli raia wa Guinea aliyekaa katika kiti hicho kwa kipindi cha miaka kumi kati ya 1963 hadi 73.

Jarida la Mambo toleo la Agosti 1994 katika uchambuzi wake wa nani alistahili kuwa rais katika uchaguzi wa mwaka 1995, lilimwagia sifa nyingi Dkt. Salim hali ambayo imekuwa tofauti kidogo katika uchaguzi uliopita wa mwaka 2005.

Nitanukuu maneno mchache ya gazeti hilo kuhusiana na Dkt. Salim. ‘Salim hana matatizo na watu wa bara. Mama yake ni Mnyamwezi na ukoo wake haujatoweka Tabora. Alipokuwa waziri mkuu (1985) alitekeleza suala la kuruhusu mitumba ambayo ilisaidia wananchi wa kawaida katika kipindi hicho kutokana na hali ngumu ya maisha iliyokuwepo’.

Ikumbukwe kwamba kipindi hicho Mwalimu Nyerere alikuwa bado yungali hai, na ndipo rais wa awamu ya pili Mzee Ali Hassan Mwinyi alikuwa anamalizia kipindi chake Mwalimu Nyerere aliuchukia sana ubaguzi wa rangi, na Mzee Mwinyi alikuwa akitokea Zanzibar, mazingira yote hayo yalikuwa na faida nyingi kwake (Dkt Salim).Mchakato wa kumpata mgombea urais kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), mwaka 2005 ulikuwa na mazingira magumu kwa Dkt. Salim.

Baadhi ya makombora yaliyoelekezwa kwake ni ‘Uarabu’ wake na kwamba baadhi ya ndugu zake walikuwa na nafasi kubwa serikalini na jeshini katika nchi za uarabuni.

Yote hayo yalifanyika wakati Mkapa akiwa na nyadhifa zote mbili, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na pia mwenyekiti wa chama tawala CCM.

Kwa kuyazungmzia hayo simaanishi kwamba Dkt. Salim ameitumia nafasi yake katika jopo la uteuzi kwa lengo la kulipiza kisasi bali nataka kuonyesha kwamba yeye akiwa ni muathirika wa ubaguzi wetu na akiwa binadamu mwenye hisia kama sisi wengine tulivyo alikuwa ana haki pia ya kujiuliza mara mbilimbili utoaji wa tuzo ya kiongozi bora kwa Mkapa.

Tukiachana na hao viongozi wawili mahiri waliohusika katika jopo la uteuzi. Sasa tuwageukie viongozi wetu ambao wamezua mijadala mingi hapa Tanzania yaani Joachim Chissano na Benjamin Mkapa. Wapo walioona tuzo hiyo ilistahili kumwendea Mkapa badala ya Chissano wapo pia wanaoona Chissano alistahili kuipata tuzo hiyo.

Mijadala hiyo ndiyo imenifanya niwaweke viongozi hao wawili wastaafu katika mizani ili baadaye tufikie muafaka kwamba ni nani kati yao alistahili kupata tuzo hiyo. Lakini ni muhimu kwanza tujiridhishe kwamba ni kwa nini Chissano ameipata tuzo hiyo badala ya Mkapa.

Joachim Alberto Chissano alikuwa ni miongoni mwa vigogo wa juu kabisa ndani ya chama cha FRELIMO baada ya kifo cha Samora Machel mwezi Oktoba mwaka 1986. Awali ya hapo Samora alisaini mkataba wa maelewano na serikali ya makaburu (Nkomati Accord) tarehe 16 Machi 1984.

Lakini hakuna msukumo wa nguvu unaonishawishi niamini kwamba ni yeye pekee alistahili kumrithi Samora najua hilo linaweza kukutana na upinzani lakini wafuatiliaji wa mambo yalivyokuwa Msumbiji kwa wakati ule watakubaliana nami kwamba waliostahili kumrithi Samora ni aliyekuwa Katibu Mkuu wa FRELIMO Marcelino Dos Santos vinginevyo angekuwa mjane wa Samora Machel Graca Machel.

Marcelino Dos Santos msomi mwenye kiwango cha shahada ya udaktari, mwenye uwezo wa kuzungumza lugha mbalimbali za kimataifa na pia mshairi mahiri alirushiwa makombora kwamba ni chotara wa kireno!

Graca Machel alitupwa nje ya mfumo kwa muda na baadaye alirudishwa lakini pia kukiwa na minon’gono kwamba yeye aliwahi kuwa katika timu ya watu waliotaka kuendesha mapinduzi dhidi ya serikali ya Jochim Chisssano.

Wapo wanaodai kwamba kifo cha Samora kilikuwa ni muendelezo wa mauaji ya wakomunisti kama ilivyojitokeza kwa Amilcar Cabral, Patrice Lumumba, Ernesto ‘che’ Guavara, Walter Rodney na wengineo hasa katika nchi za Latini Amerika.

Rejea habari za The New Nation Septemba 4, 1992, na madai ya aliyekuwa rais wa Russia marehemu Boris Yeltsin. Yeye alidai mauaji ya Samora yalikuwa mauaji dhidi ya ukomunisti na alikuwa tayari kugharimia uchunguzi huru juu ya ajali iliyochukua uhai wa Samora.

Mojawapo ya sifa anazopewa Chissano kwamba zimechangia kupewa tuzo hiyo ni kuibadilisha nchi hiyo kutoka katika ukomunisti kwa hiyo tuamini kwamba yawezekana hiyo ni zawadi maalumu kwake kwa kufanikisha kuua ukomunisti barani Afrika?

Hoja hiyo inawiana na madai kwamba wapo viongozi ndani ya FRELIMO waliohusika na mauaji ya Samora kwa ajali ya kupangwa kama ilivyofanyika Pakistan kwa Jenerali Zia Ul Hug ambaye alimpindua na baadaye kumuua Zulfikar Ali Bhutto waziri mkuu aliyekuwa kipenzi cha ‘walalahoi’ wa Pakistan

Hoja hiyo inaweza kuwa na maelezo ya ziada ya kisayansi kwamba licha ya ukomunisti hata ule uamuzi wake wa ghafla wa kugeuza mwelekeo bila kuwashirikisha wenzake ilikuwa ni sababu tosha ya wenzake kumuangamiza.

Historia inayo mifano mingi inayowahusu wote waliopata kuchukua maamuzi ya namna hiyo (U-turn decisions), katika kusaini mikataba bila kuwashirikisha wenzao kikamilifu au hata kwa kuonekana wameisaliti misimamo yao ya awali.

Watetezi wa hoja hiyo wanadai kwamba viongozi wote waliopata kufanya maamuzi ya namna hiyo baadaye waliuawa kwa kuhujumiwa na wenzao ndani ya mfumo,mifano michache inayotolewa ni ule wa Camp David wa tarehe 17 Septemba 1978 kati ya waziri mkuu wa Israeli kwa wakati ule Menachem Begin na Rais Anwar Al Sadat wa Misri.

Kitendo hicho kilihesabiwa na baadhi ya waarabu wenzake kwamba ni cha kisaliti na hivyo Sadat aliuawa kwa kumiminiwa risasi tarehe 6 Oktoba 1981.

Jambo kama hili liliwarudia waisraeli pale waziri mkuu wao Yitzhak Rabin aliposaini mkataba wa maelewano na kiongozi wa mamlaka ya wapalestina Yasser Arafat kwanza kwa maelewano na wapalestina ya tarehe 20 Agosti 1993 (Oslo Accords) na baadaye tarehe 13 Septemba 1993 katika kile kilichoitwa ‘Declaration of Principles’ au kwa jina jingine Gaza-Jericho Washington Peace Agreement.
Kwa baadhi ya waisraeli Rabin alionekana ni msaliti kwani maelewano hayo yalihusu kuachia baadhi ya maeneo yanayokaliwa na waisraeli kwa wapalestina hivyo naye aliuawa tarehe 4 Novemba 1995 kwa kupigwa risasi.

Tukirudi kwa suala la Msumbiji ni vipi basi makaburu waliendelea kumuunga mkono Alfonso Dhlakama wakati tayari kulikuwa na maelewano ya Nkomati?

Maelezo ya hilo ni kwamba kuingia kwa Chissano si kwamba kuliondoa tu ukomunisti Msumbiji lakini pia hakukutekeleza maelewano ya Nkomati ndiyo maana makaburu waliendelea kukifadhiri kikundi cha RENAMO hadi muafaka ulipofikiwa mwaka 1992 na kikundi hicho kikatambuliwa kama chama cha siasa.

Lakini pia suala la kumalizika kwa vita kati ya FRELIMO na RENAMO linafaa liangaliwe katika mtazamo wa kihistoria kwamba kusambaratika kwa Soviet Union ya zamani ndiko kulichangia kuwapo kwa mabadiliko kadhaa duniani.

Kwa mfano kuachiliwa kwa Mzee Nelson Mandela, ambako kulihitimisha utawala wa makaburu kisiasa lakini kumewanufaisha zaidi kiuchumi “Makaburu” kwani sasa wanamtandao mkubwa wa uwekezaji wakizidi kupanda kaskazini mwa bara la Afrika.

Maelezo yangu marefu ambayo kwa msomaji mwingine anaweza kuona kwamba hayawiani na uteuzi wa Chissano ni katika kujenga hoja kwamba inawezekana kwamba japo wenye ushawishi mkubwa zaidi katika uteuzi wa Chissano ni waafrika wenzetu lakini pia upo uwezekano kwamba kulikuwa na ushawishi wa nje katika uteuzi huo.

Maana yangu ni kwamba kumalizika kwa mgogoro wa FRELIMO na RENAMO hakukutokana tu na busara za Chissano lakini pia ni kwa sababu yeye pia aliusambaratisha ukomunisti nchini mwake.

Sababu nyingine ni ukweli pia kwamba Chissano hajawahi kutuhumiwa kwa udikteta nchini mwake na vyombo vya habari vya ndani na nje ya Msumbiji tofauti na viongozi wengine wa kiafrika kama ilivyokuwa kwa Mugabe au hata kwa ukiukwaji wa haki za binadamu kama ilivyokuwa kwa Mkapa kama nitakavyoeleza hapo baadaye.
Licha ya hayo ni jinsi ambavyo Chissano amefanikisha zoezi la mpito kutoka kwenye serikali yake hadi kwa serikali iliyopo sasa ya ‘Comrade’ Armando Emilio Guebuza kwa njia ya amani, na katika uchaguzi ambao haukuleta malalamiko makubwa kama ilivyo katika chaguzi za nchi nyingine.

Tusisahau pia kwamba wakati Rais Mugabe alipoamua kunyakua mashamba ya walowezi waliopo nchini mwake na kuyakabidhi kwa wazalendo, Chissano aliwakaribisha walowezi hao nchini mwake ambapo wamenunua ardhi bikira (virgin land) ambayo inarutuba na haijawahi kulimwa kabisa.

 Kilichofanyika ni kuyategua mabomu yaliyokuwa kwenye ardhi hiyo ambayo yalitegwa wakati wa vita ya wenyewe kwa wenyewe ya muda mrefu.

Lakini siyo kwamba Chissano hakupata upinzani wa hapa na pale kutoka kwa wanajopo waliohitimisha kwa kumpatia tuzo hiyo.Kwa mfano baadhi ya wanajopo walidai yeye hajawahi kukemea vitendo vinavyofanywa na jirani yake Mugabe.
Pia tuhuma zinazomhusu mtoto wake kwamba alihusika na mauaji ya mwandishi wa habari Carlos Cardoso tayari Chissano amewahi kutoa ruhusa kwa mamlaka husika kama vile polisi na mahakama kuchukua hatua bila kujali kwamba mhusika ni mwanae kwani tayari huyo ni mtu mzima.

Doa kubwa la Mkapa ni suala la mgogoro wa Zanzibar ambalo alionekana kulifumbia macho, au kushindwa kuchukua hatua madhubuti ambazo zingeweza kuleta ufumbuzi wa kudumu. Sasa kwa sababu mojawapo ya sifa kuu iliyompatia tuzo Chissano ni uwezo wake wa kutatua mgogoro wa chama chake na RENAMO.

 Hata kama ulikuwa umechochewa kutoka nje lakini kushindwa kwa Mkapa kutatua mgogogoro wa Zanzibar kati ya CCM na CUF mahali ambapo mmoja wa wanajopo anatoka yaani Dkt. Salim ni sababau tosha ya kumnyima sifa ya kupata tuzo hiyo.

Lakini kwa upande mwingine doa jingine kubwa kwa utawala wa Mkapa ni mauaji yaliyotokea Zanzibar Januari 26 na 27 mwaka 2001. Ambapo zaidi ya wafuasi 20 wa chama cha upinzani CUF waliuawa na polisi.

Hilo lilikuwa ni doa kwake kwa sababu Zanzibar ni sehemu ya Tanzania kufuatia Muungano wa mwaka 1964. Pia Mkapa anatuhumiwa kwa kuvigandamiza vyama vya upinzani pamoja na uchanga wa vyama hivyo. Kwa mfano matumizi ya rasilimali kubwa katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Sengerema mwaka 1998.

Matukio mengine ni kushindwa kwake kuwalinda raia wake kama vile kupigwa kwa makamu mwenyekiti wa chama cha upinzani cha UDP, Dkt Fortunatus Masha mwezi Oktoba, 2000.

Matukio mengine ni pamoja na kukamatwa kwa mwenyekiti wa chama cha TLP, Augustine Mrema na Rais wa Chama cha Wanasheria za Mazingira (LEAT) Nshala Rugemeleza baada ya kutoa madai kwamba wachimbaji wadogo walifukiwa na kufa huko Bulyanhulu mwaka 1996.

Pamoja na hayo ni hizi tuhuma za ufisadi ambazo bado zinaendelea kufumuliwa dhidi ya serikali ya Mkapa. Kwa hiyo ukiwaweka katika mizani Chissano na Mkapa kwa kuzingatia vithibitisho  hivyo vichache tulivyonavyo ni dhahiri tuzo hiyo inastahili kwenda kwa Chissano na wala siyo kwa Mkapa.

Lakini kukosa tuzo hiyo pekee hakuondoi mazuri ambayo Mkapa kama kiongozi amewaachia Watanzania kama vile mfumo mzuri wa miundo mbinu, sekondari za kata, majengo mapya ya serikali, uwanja wa kisasa wa mpira, pia ameshughulikia kwa kiwango kikubwa matatizo ya wakimbizi kutoka katika nchi za jirani zilizokumbwa na machafuko.

Mwandishi wa makala haya anapatikana kwa simu 0754 826 272
Na kwa barua pepe: mhegeraelias@yahoo.com






Hakuna maoni:

Chapisha Maoni