Jumapili, 6 Julai 2014

UDINI TANZANIA NI KWA MANUFAA YA NANI?

\
Kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Tanzania Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo 



Muft Mkuu Shekhe Shaban Simba 


28/11/2013 | Elias Mhegera
KATIKATI ya Novemba mwaka huu viongozi wa kiroho na wawakilishi kutoka taasisi za dini walikutana katikati ya Jiji la Dar es Salaam katika Hoteli ya Accomondia kujadili mustakabali wa amani.
Viongozi hao kutoka Zanzibar na makao makuu ya Baraza la Madhehebu ya Dini kwa Ajili ya Amani Tanzania (IRCPT) walikutanishwa chini ya ushirikiano na asasi ya Konrad Adenaeur Stiftung (KAS) kutoka nchini Ujerumani.
Mjadala juu ya vyanzo vya chokochoko za udini kama ilivyotarajiwa tokea awali haukuwa mwepesi kutokana na kila upande kati ya Waislamu na Wakristu kujitetea au kujisafisha kila ulipoguswa.
“Mnalo jukumu kubwa la kuhakikisha kwamba Tanzania inaendelea kuwa nchi ya amani kwa sababu waamini katika taasisi zenu za dini wana imani kubwa na nyinyi,” anasema Stefan Reith, Mkurugenzi Mkazi wa KAS.
Reith anasema taasisi yake imekuwa ikiandaa mikutano mingine kama huo wa siku hiyo na yote imekuwa na mafanikio makubwa. Alikuwa na mategemeo kwamba mkutano huo utakuwa na mafanikio kama ile iliyotangulia.
Naye Jaji mstaafu, Raymond Mwaikasu, aliwaomba washiriki katika warsha hiyo kuwa huru katika kutoa mawazo yao kwa sababu kwa kufanya hivyo ndipo watapata kuyaondoa madukuduku yao ili yafanyiwe kazi vizuri.
Naye Sheikh Haji Mussa kutoka Wakf and Trust, Zanzibar anashukuru kwamba sasa walau kuna utulivu visiwani Zanzibar kwani kwa miaka kadhaa kumekuwa na hali tete ya kiusalama inayosababishwa na mambo ya udini.
Wahudhuriaji walipata mwanya wa kukumbushana jinsi ambavyo wazo lao lilisababisha kuanzishwa kwa Benki za Wanavijiji (Vicoba), lengo likiwa ni kuwasaidia watu wenye kipato cha chini hususan wajasiriamali.
Kutoka katika Kituo cha Uhusiano Mwema wa Imani Zanzibar alikuwapo Mratibu wake, Daniel Madsen, aliyesema kwamba uhusiano mzuri wa watu wa imani tofauti ni jambo linalotakiwa kujengwa tokea watu wanapokuwa katika umri mdogo.
Anasema kwamba kituo chake kimekuwa kikitimiza azima hiyo kwa njia ya vitendo kwa kuendesha kampeni mbalimbali ikiwamo michezo kwa watoto. Akizungumzia historia ya kituo chake anasema kilianzishwa mwezi Aprili mwaka 2009 na kujiweka sawa zaidi kiutekelezaji mnamo mwaka 2010.

“Tunajivuna kwamba leo kituo chetu kimekuwa ni kimbilio kwa wengi wanaotaka kupata taarifa mbalimbali kwa kusoma nyaraka, kujifunza kompyuta,  kujifunza lugha ya Kiingereza na hata kwa ajili ya utafiti,” anasisitiza.
Padri wa Kanisa la Kianglikana, Emmanuel Masoud, ambye pia ni katibu msaidizi katika Kamati ya Maridhiano ya Dini Zanzibar anasema visiwa hivyo vilijijengea umaarufu mkubwa kutokana na ukarimu wa watu wake na hata watalii wengi wakaja visiwani humo na wengine kwa ajili ya mashindano ya uvuvi.
Anasema leo hali imebadilika kidogo na watu hawana tena uhakika wa usalama wao moja kwa moja bali katika hali ya mashaka mashaka. Anasema hali hiyo ndiyo imesababisha leo Zanzibar kuwa kituo kikuu cha wauzaji wa dawa za kulevya na hata biashara ya pembe za ndovu ingawaje Zanzibar hakuna hata tembo mmoja.
Anasema vitabu vyote vitakatifu kwa Wakristu na Waislamu vina sisitiza juu ya amani lakini leo ni kinyume chake na ana wasuta wanasiasa kwamba wamechangia katika uhasama wa kidini visiwani humo.
Anayataja matukio yaliyoleta sintofahamu visiwani humo kuwa ni pamoja na mauaji ya Padri Evarist Mushi wa Kanisa Katoliki pamoja na kushambuliwa viongozi wengine wakiwamo Sheikh Fadhili Soraga aliyemwagiwa tindikali.
Anasema matukio yote haya pamoja na uchomaji wa makanisa si utamaduni wa Wazanzibari bali wa watu wabaya wenye lengo la kuondoa amani na kuchafua jina zuri la nchi hiyo.
Pia alitumia muda huo kuzishukuru taasisi zote ambazo zimekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kwamba kuna maridhiano ya watu wa dini tofauti nchini Tanzania Visiwani hususan; KAS na taasisi ya Norwegian Church Aid.
Naye Katibu Mtendaji wa IRCPT, Mch. Thomas Godda, alisema maridhiano ya dhati kati ya watu wa imani tofauti yatapatikana tu kwa viongozi wa taasisi husika kupitia BAKWATA, TEC, CCT, HINDU, BAAHAI na PCT   kukaa pamoja na kutafuta ufumbuzi wa matatizo yaliyopo.
Naye Julian Laurent, mtumishi katika Tume ya Haki za Binadamu (CHRAGG) na mjumbe wa Kamati ya Taifa ya Kuzuia Mauaji ya Kimbari (NCPG), alishauri kwamba njia nzuri ya kuzuia chokochoko za dini ni kwa viongozi wa madhehebu mbalimbali kuhubiri amani kwa waamini wao.

“Kamati yetu inaamini kwamba viongozi wa kiroho wana mchango mkubwa sana katika kuzuia majanga ya vita na wakimbizi, tunaomba mshirikiane na vyombo vya habari katika kufanikisha hilo,” anashauri.
Naye George Bagomwa kutoka IRCPT alishangaa kuona kwamba Jeshi la Polisi katika siku za hivi karibuni limeshindwa kuwanasa wale wote wanaochoma makanisa na hata kuwamwagia watu tindikali kama ilivyotokea Zanzibar.
Lakini Ditrick Rutashobya kutoka Kitengo cha Vijana cha IRCPT anasema kwamba matukio ya kuharibiwa mali za Wakristu ikiwamo kuchomwa kwa makanisa ni matokeo ya propaganda hasi za wanasiasa zilizotumika katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.
“Madai kwamba Dk. Willibrod Slaa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) alikuwa anagombea ili kuwakilisha masilahi ya Kanisa Katoliki kwa sababu yeye alipata kuwa padri, dhidi ya Jakaya Kikwete wa CCM ambaye ni Mwislamu zimeacha makovu yasiyotibika, kampeni za aina hiyo hazifai na wala zisije zikarudiwa tena,” alionya.
Naye Mratibu wa Miradi wa Chama cha Waislamu Wanataaluma (TAMPRO), Said Ngolola, anadai kwamba Waislamu wana dukuduku kwa sababu serikali imekuwa ikizisaidia fedha taasisi za Wakristu na kuzibagua za Kiislamu.
Alikwenda mbele zaidi na kudai kwamba sasa hivi baadhi ya wanavyuo Waislamu wameamua kususia mikopo inayotolewa na Bodi ya Mikopo  kwa Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) kwa sababu imeambatana na malipo yenye riba, jambo ambalo halikubaliki katika Uislamu.
Hoja hiyo ilionekana kumgusa Pd. Damas Mtoi wa Kanisa Katoliki Zanzibar ambaye alisema watu wasiongozwe na hisia katika kutoa michango yao kwa sababu serikali imekuwa ikizifadhili taasisi zinazotoa huduma kwa umma zikiwamo hospitali na vyuo vikuu na wala si kwa sababu ni mali za Wakristu.
Ngolola alipata faraja mara baada ya mjumbe wa bodi ya IRCPT Mama Hindu Lila kudai kwamba serikali imekalia madai 19 ya Waislamu ambayo  wameyalalamikia katika awamu zote za uongozi wa nchi.
Anasema kwamba mnamo mwaka 1999 Waislamu walikutana na Rais wa Awamu ya Tatu Benjamin Mkapa na wakamfahamisha madai yao lakini hayajafanyiwa kazi mpaka leo ingawaje kiongozi huyo wa nchi aliahidi kufanya hivyo.
Naye Mama Shamim Khan, aliyepata kuwa mbunge na naibu waziri alisema kwamba Waislamu na Wakristu wamekuwa na mahusiano ya karibu kwa muda mrefu lakini ghafla tu umezuka uhasama, jambo ambalo linaashiria kwamba kuna uchochezi umefanyika.

Hoja ya kwamba Wakristu wanapendelewa na serikali ilionekana kuzua mjadala mkali kwa kiwango chake huku Wakristu wakidai kwamba watu wasitawaliwe na hisia bali wachimbe ili kupata ukweli zaidi juu ya jambo hilo. Ndipo Madsen kutoka Zanzibar akaonyesha uhusiano uliopo kati ya dhana, hisia na tabia.
Huku akitumia mchoro wa pembe tatu, alionyesha kwamba dhana ikijengeka na ikaungwa mkono na hisia inaweza kusababisha matendo mabaya. Japo hakuwa muwazi sana lakini yaelekea alitaka kuonyesha kwamba mashambulizi dhidi ya taasisi za Kikristu yametokana na mzingo huo wa mawazo.
Mhariri mkongwe, Lawrence Kilimwiko, hakumng’unya maneno aliposema kwamba baadhi ya wanasiasa hutafuta kuungwa mkono na wafuasi wa dini zao pale wanapokuwa wameshindwa kukidhi matarajio fulani.
Naye mhariri mwingine mkongwe, Mboneko Munyanga, alionya kwamba wale wanaodhania kwamba wanaweza kuondoa amani ya Tanzania kwa kupenyeza udini wamechelewa, kwa sababu kuna miingiliano mingi ya kifamilia kati ya Waislamu na Wakristu.
Paul Shemshanga kutoka (PCT) alionya juu ya kuwapo lindi kubwa la wahubiri ambao japo hawajapata mafunzo yoyote darasani lakini wanaushawishi mkubwa kwa sababu wamezaliwa na nguvu fulani za kiroho.
Dk. William Kopwe kutoka CCT anashauri kwamba kuwepo na uratibu mzuri wa watu wote wanaoendesha shughuli za kiimani ikiwamo mihadhara ili kuzuia baadhi ya watu wenye nia ovu kufanikisha mambo yao.
Naye Mwendesha Mkutano huo, Salim Zagar, akisoma majumuisho ya michango alisema kwamba wazo la viongozi wa kiroho kukutana na Rais Kikwete limeonekana ni la muhimu sana.
Pia alisoma maoni kwamba mali za umma zisitumike kwa manufaa ya dini yoyote kwa njia za kibaguzi. Na kwamba wajumbe waliona kuna umuhimu wa masuala ya amani kwa watu wa dini tofauti yawe katika mitaala ya elimu ya sekondari.
Wajumbe walikemea vikali tabia za uchochezi wa kidini kutoka kwa wanasiasa, na propaganda zote zenye kuchochea udini ikiwamo hata katika nyumba za ibada.
Kulikuwa na pendekezo kwamba serikali iitambue rasmi IRCPT kama chombo halali cha kushughulikia maridhiano ya dini kwa watu wa imani tofauti.

Kulitolewa ushauri kwa serikali kuangalia upya suala la elimu na kuondoa umaskini kwa sababu mambo haya yanachangia kwa kiwango kikubwa watu kushawishiwa kwa kudanganywa au hata kwa kupewa fedha kidogo.
Viongozi wa kiroho walionyesha nia ya kuitisha  mkutano wa hadhara kwa watu wa madhehebu yote kwa lengo la kuzungumzia amani. Hasa kwa kuzingatia kwamba Tanzania inaelekea katika uchaguzi wa serikali za mitaa 2014, na Uchaguzi Mkuu 2015.
Imeshauriwa kwamba wadau wengine kama vile asasi za kiraia, wasomi, na vyombo vya habari vitoe mchango katika kuzungumzia masuala ya amani na kupinga uchochezi wa kiimani.
Kuanzia sasa iwe ni marufuku kwa mtu yeyote kuhubiri dini yake huku akiwa ameshikilia kitabu cha imani tofauti. Kanda za redio na video zenye kuchochea udini zipigwe vita mahali pote ikiwamo katika nyumba za ibada.
Naye kiongozi mwandamizi kutoka KAS,  Richard Shaba anasema ili Tanznaia iendelee kuwa na amani watu wabadilike na kuanza kuifikiria amani bila kujali tofauti za dini, hisia na hata ufuasi wa dini zao.
Tuwasiliane: mhegera@gmail.com Simu-0754-826227


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni