Jumapili, 6 Julai 2014

NANI KADANDIA FARASI WA HURUMA CCM AU UKAWA?





Na Elias Mhegera
Hivi karibuni nilichangia hoja katika mada iliyokuwa ikiendelea kati ya mwanasiasa kijana na mwandishi wa mmoja wa kike. Katika hitimisho langu juu ya mzozo huo nilisema kwamba mwandishi huyo alikuwa amedandia farasi wa huruma kwa kusema kwamba mpinzani wake mwanasiasa kijana anadharau waandishi wanawake.
Ni  pia nikasema kwamba mwanasiasa huyo hakumkosoa mwandishi wa kike kwa sababu ni mwanamke bali kwa kuangalia udhaifu wa hoja zake. Baadaye hoja hiyo ilimfurahisha mhariri mmoja wa gazeti la Mawio kuipenda hoja yangu.
Mhariri huyo akaniomba niingalie hoja yangu katika muktadha wa mvutano kati ya CCM na UKAWA ni nani alikuwa anadandia farasi wa huruma katika kupata katiba mpya?
Kama tunavyofahamu wabunge wa vyama vilivyounda Umoja wa Katiba ya Wanachi (UKAWA) waliamua kuondoka bungeni baada ya CCM kuanza kuyagandamiza mapendekezo ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mpya iliyokuwa chini ya jaji  Joseph Warioba ambaye pia ni waziri mkuu mstaafu.
Kwa kweli swali hilo lilikuwa ni la mtego kidogo ingawaje jibu lake lipo wazi kabisa. Nami nikaaanza kwa kujibu kwamba mtu wa kwanza kujibu hilo siyo mimi bali Mzee Jenerali Ulimwengu na tena katika miaka ya mwanzo kabisa ya 90.
Mzee Ulimwengu alipata kuandika makala katika miaka ile akisema kwamba baadhi ya wanasiasa wa CCM wa leo ni wanafiki na akaitetea hoja yake akitoa ushahidi wa “makasri” kama alivyoyaita yeye akimaanisha majengo makubwa makubwa ambayo ndiyo kwanza yalikuwa yameanza kuchipuka kama uyoga huko Mikocheni na Masaki.
Ulimwengu alisema kwamba wanasiasa hao wa CCM walikuwa wameficha mamilioni ya pesa ambayo baada ya Mwalimu Nyerere kustaafu sasa walianza kuyatumia kwa kuporomosha maghorofa kibao na hata dhana yenyewe ya uwekezaji wa ndani ilianzia hapo hapo kukawa na miradi iliyofumuka kila siku na kukabidhiwa kwa watu ambao siku chache zilizotangulia walikuwa ni mafukara wa kutupwa.
Lakini baada ya “Mzee Ruksa” kusema watu kufungua “vijimiradi vya kuku wa mayai”siyo mbaya wao wakaanza kukabidhi biashara zao kwa ndugu zao na hapo yakaanza kununuliwa mabasi ya kisasa na kulihujumu shirika la reli ili lisiharibu biashara za mabasi yao.
Hali ikaendelea hivyo mpaka baadaye mawaziri wakaanza kumiliki mashirika ya ndege wengine wakipitia migongoni mwa watu binafsi na wengine wakiyamiliki mashirika ya ndege moja kwa moja na hapo ndipo Air Tanzania ikaingiwa na virusi vilivyoanza kufifisha afya yake.
Cha ajabu ni kwamba hao wana CCM mamilionea eti nao bado wanadai wanafuata nyayo za “Baba wa Taifa” na kuwaambia Watanzania wakiacha kuipigia CCM maana yake ni kwamba wanamsaliti Mwalimu Nyerere na waasisi wenzake wa TANU akina Marehemu Rashid Kawawa na baadaye Mzee Abeid Amani Karume katika muungano wake na ASP na kuunda CCM (chini ya Mzee Aboud Jumbe).
Kwa hiyo kwa falsafa hiyo mtu yeyote akihama kutoka CCM na kujiunga na chama chochote cha upinzani basi huyo ni msaliti wa waasisi wa taifa hili.  Na kinyume chake mtu yeyote akifanya ufisadi na bado akabakia ndani ya CCM basi huyo anamuenzi Mwalimu na waasisi wenzake.
Hapo ndipo pananitatiza juu ya kumuenzi Mwl. Nyerere. Nakumbuka Mwl katika kujiandaa kustaafu alimuweka katika nafasi ya uwaziri mkuu mtu mahiri kabisa Marehemu Edward Moringe Sokoine ili apambane na ufisadi lakini mtu huyo akafa kifo chenye maswali mengi kuliko majibu mwaka 1984 ikiwa ni mwaka mmoja tu kabla ya kustaafu kwa Mwalimu Nyerere.
Kuhusu hatua alizochukua Sokoine kupambana na ufisadi watu wengi wenye rika kama langu la miaka 50 na zaidi wanayo kumbukumbu nzuri.
Mimi mwenyewe nikiwa mwanafunzi Seminari ndogo ya Nyegezi nilikuwa mmoja wa watu waliokwenda kuokota biskuti na madebe ya sukari yaliyotupwa na wafanyabiashara wengi wakiwa ni wenye asili ya kiasia waliotupa vitu vyao maeneo ya Nyegezi fisheries wakiogopa kukamatwa katika ile saka saka hatari ya wahujumu uchumi.
Mimi mwenyewe pia niliingia kwa kujipenyeza katika mkutano pale Liberty Cinema Mwanza mwaka 1984 wakati wananchi wa Mwanza walipokuwa “wakimcha chana live” mkuu wa mkoa Marehemu Abdulnoor Suleiman na Mkurugenzi wa Mkoa Bw. Issaya Kasera Gungu.
wakitaka wavuliwe madaraka kwa sababu wanaendesha biashara ya magendo ndani ya Ziwa Victoria. Baada ya kurejea Dar Mwalimu hakusubiri cha Tume ya Bunge wala cha TAKUKURU iwavyo kwa jina lolote lile, bali aliwafutilia mbali watu hao.
Je tunakumbuka ya mwaka 1982 chini ya uongozi wa Mwl Nyerere yalivyowakumba waziri Augustine Mwingira na Meneja Mkuu wa ATC Bw. Lawrence Mmasi chini ya kashfa na hao walitimuliwa mara moja (kwa sasa wote hao ni marehemu).

Watendaji hao walikodi ndege mbili chakavu zilizokuwa zikifanya safari kati ya Ulaya na India zikimilikiwa na raia wa Lebanon Bw. George Hallack leo tunaambiwa CAG, TAKUKURU, Kamati ya Bunge, Mahakama n.k. na wakati mwingine taasisi zote hizo zinakosa ushahidi wa kuwatia hatiani mafisadi hao.
Kwa hiyo kwa muktadha wa mjadala huu aliyedandia farasi wa huruma ni CCM na tena amefanya hivyo kwa miaka mingi. Vikundi vya walafi wanaofikiria kujitajirisha leo wanasema eti wanamuenzi Mwalimu Nyerere je wanafanya hivyo kivipi? kwa kupora mashamba na ardhi ya wanyonge?
Je ni kwa kuendesha biashara kubwa ya mahoteli? kwa kumiliki malori na vituo vya mafuta? kwa mikataba mibovu katika  madini? huko ndiko kumuenzi Mwalimu? je yeye aliacha malori mangapi? aliacha mahoteli mangapi? baada ya kuwa amekaa madarakani kwa zaidi ya miaka 20? nadhani nimeeleweka vyema.
UKAWA ni mojawapo ya jitihada kutoka kwa wale wasioridhishwa na hali ya kisiasa nchini, jitihada hizo zimekuwa nyingi na pia katika majina tofauti tofauti kuanzia lile kundi la wabunge 55 yaani G-55 lililokuwa likiongozwa na Mzee Njelu Kasaka, Philp Marmo, Jeneral Ulimwengu na wenzao.
Baadaye alikuja mama ambaye sauti yake imezimika ghafla hatujui kulikoni? (Anne Kilango) Lumambo Seleli, James Lembeli n.k. labda tofauti ya hii UKAWA ya sasa imetokana na vyama vya upinzani.
Kwa hiyo UKAWA ni zaidi ya katiba mpya, bali ni njozi ya matumaini iliyorejea baada ya wapinzani kuanza kupata busara baada ya kuwa wakisutana wao kwa wao  miaka nenda rudi.
Miaka iliyotangulia ilionekana Tanganyika ikirejea kutakuwa na muamko wa kisiasa lakini leo hoja ya kukataa serikali tatu kwa CCM ni hofu ya kushindwa, kwani Muungano kwa jinsi ulivyo sasa unawapatia wao manufaa ya kuendelea kubakia madarakani.
Elias Mhegera-Tel: 0754-826272



Maoni 1 :

  1. wamemshambulia vikali kwamba ni msaliti kisha wakampatia tuzo ya uzalendo, wapi na wapi?

    JibuFuta