Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu Mzee Benjamin Mkapa
NB:
Makala hii ilitumika katika gazeti la Majira
Jumapili May 02, 2008
Na
Elias Mhegera
Ufisadi
ni tunda la kukengeuka kimaadili, hali hiyo inajitokeza mara kwa mara kwa
viongozi wetu, kwa hiyo ni lazima tujiulize mara mbili mbili ni wapi
tumepotoka.
Pia
tutafakari ni kwa jinsi gani tunaweza kuondokana na hali hiyo. Ufisadi ndiyo
unaochangia katika kuongezeka kwa udikteka katika nchi za Kiafrika kwani
viongozi waliopo madarakani huogopa kwamba wanaweza kufunguliwa mashitaka mara
waondokapo madarakani.
Ni
katika mazingira hayo tulishuhudia nchi kama Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo
ikiitwa Zaire chini ya Mobutu Seseko ikigeuzwa kuwa kisima cha wendawazimu kuchota utajiri wa nchi hiyo bila huruma huku
wakiiacha nchi na mashimo matupu baada ya kuchota hazina kubwa ya madini
iliyomo nchini humo.
Leo
hii DRC ni nchi maskini kama zilivyo nchi nyingi za kiafrika bila kujali ina
hazina kiasi gani ya utajiri.Ufisadi ni maradhi mabaya ambayo Watanzania hatuna
haja ya kukumbushwa kwa sababu tayari madhara yake tumeyaona.
Mikataba
mibovu katika upatikanaji wa tenda mbalimbali kama vile zile za umeme za IPTL,
Richmond, Songas, ni mifano michache ya jinsi ambavyo hazina ya taifa inaweza
kuchotwa na waroho wachache kwa manufaa yao, na kuwaacha wananchi walio wengi
wakiwa wanaumia kwa kukosa huduma muhimu.
Tunapozungumzia
tuhuma za ufisadi hatuna maana kwamba watuhumiwa au hata wahusika wanyongwe,
wakatwe mikono au wafanyiwe mambo kama hayo bali tunawashawishi tu wapendwa
wetu hao warudi kundini ili tuishi tena maisha ya amani na utulivu kama ilivyo
utamaduni wetu Watanzania.
Ni
imani yangu kwamba hakuna mtu mwenye busara atakayechukia hizi kelele
zinazopigwa dhidi ya ufisadi.Ni ukweli usiopingika kwamba hata kama ufisadi
unamnufaisha kwa namna gani mtu mmoja na familia yake lakini bado kuna ndugu
zake wengi wanaathirika kutokana na ufisadi huo huo.
Leo
kuna tuhuma kadhaa ambazo nyingine zipo mahakamani. Kimsingi ni kwamba bado
watuhumiwa wanaweza kushinda katika kesi hizo, lakini hiyo haiondoi ukweli
kwamba watu hao wamehujumu mali ya umma.
Ni
dhahiri katika nchi ambayo viongozi wake wakuu wengi wamekengeuka kimaadili
basi hata mifumo mingine inayotakiwa kuunga mkono mifumo hiyo nayo itaathirika
kwa kiwango kikubwa.
Uoza
katika jamii huanza kwa kiwango kidogo lakini baadaye husambaa katika maeneo
makubwa kama vile ugonjwa.
Kwa
vile Mzee Mkapa amestaafu kwa heshima zote, nadhani ni vizuri tukamuacha
apumzike, lakini na yeye pia atutendee uungwana kwa haya yafuatayo; akiri
kwamba ametenda ndivyo sivyo.
Watanzania
walimuamini na kumpatia dhamana ya uongozi kwa vipindi viwili vya miaka mitano
mitano, hivyo awatambue wakosoaji wake kwamba si maadui zake bali ni watu wenye
mapenzi mema na nchi yao. Kuna mazuri mengi lakini kuna mapungufu kadhaa pia
aliyoyacha.
Alirudisha
heshima ya watumishi wa umma ambao kwa miaka kadhaa walikuwa wanadharaulika
kama watu wa chini wasio na kipato baada ya walanguzi kujimilikisha uchumi hasa
katika awamu ya pili ya Mzee Ali Hassan Mwinyi.
Katika
hilo alipandisha mishahara ya watumishi wa umma na akaanzisha utaratibu wa
kujenga majengo mapya kwa ajili ya makazi na ofisi kadhaa za watumishi hali
ambayo hakuwapo katika awamu zote zilizomtangulia.
Ni
Mkapa huyo huyo aliyehjitahidi kuongeza udahili wa wanafunzzi katika vyuo
vikuu, ikiwa ni pamoja na kutoa majengo kadhaa ya serikali kwa baadhi ya vyuo
kama vile Chuo Kikuu cha Tumaini, Chuo Kikuu cha Mt. Agostino, Chuo Kikuu cha
Kiislamu Morogoro, n.k.
Itoshe
tu hapa kuonyesha kwamba wakati tunapotafakari juu ya hatma ya Mkapa tukumbuke
pia kwamba yapo mazuri aliyoyafanya.
Lakini
kwa upande mwingine ipo historia kivuli ambayo kwa miaka kadhaa
haitashahauliuka kwa Watanzania na hasa kwa kuzingatia imani waliyokuwa nayo
katika uongozi wake.
Ndiyo
maana nimesema lengo la makala hii ni kutaka viongozi wengine wajifunze na
kutanabahisha ni kwa nini mtu huyo aliyeanza kwa kupewa sifa zote za usafi
ameondoka madarakani na kugubikwa na tuhuma nyingi za ufisadi.
Katika
mambo mawili ambayo hata mimi binafsi sikuyategemea kutoka kwa mwanadiplomasia
mahili kama yeye ni ‘ukatili’ dhidi ya wapinzani, na hili la kula bila kunawa
mikono, yaani ufisadi wa kupindukia.
Ni
hapo ndipo ninaona maanguko makuu ambayo yameizika historia nzuri ya utumishi
uliotukuka kwa miaka kadhaa. Nitaeleza kwa kifupi juu ya hoja zangu hizo.
Ni
imani yangu kwamba si matajiri wote wanaoipenda CCM kwa mapenzi ya dhati bali
wamejifunza kutoka kwa wenzao ambao walijiunga na kambi ya upinzania na mambo
yao kibiashara yakaharibika kwa kiwango
kikubwa.
Mifano
ipo mingi lakini nataka tujikumbushe yale yaliyompata mwandishi mwandamizi
Jenerali Ulimwengu ambaye alivuliwa uraia katika misingi ambayo ilijionyesha
dhahiri kwamba ni ya kisiasa kutokana na kuikosoa vilivyo serikali ya Mkapa.
Katika
mantiki hiyo hiyo tunawaangalia watu kama vile Dkt. Masumbuko Lamwai ambao
walijiunga na upinzani.
Dkt.
Masumbuko Lamwai alikuwa mwiba mkali pale alipojiunga na NCCR-Mageuzi na kuunda
ngome imara ya upinzani akishirikiana na Mabere Marando, Mzee Ndimara
Tegambwage, Mch. Kamara Kusupa na wengine kadhaa.
Upinzani
wake ulisababisha apoteze wadhifa wake wa uhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam, akafungiwa uwakili Bara , akapoteza udiwani Manzese na hatimaye
akabakia mtu wa kuwawaya.
Wapo
wengi waliodhurika kutokana na mfumo mbaya wa kisiasa ambao aliujenga Mkapa
miongoni mwao ni pamoja na Mwenyekiti wa sasa wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam,
John John Guninita ambaye alikihama chama hicho na kujiunga na CHADEMA.
Mazingira
magumu aliyokumbana nayo katika kambi ya upinzani yalimrejesha ‘kikondoo’
katika chama tawala na leo amekumbukwa na kupata wadhifu huo.
Ni
Mkapa huyo huyo aliyeshinikiza Karume
awe mgombea wa urais Zanzibar mwaka 2000 wakati alikuwa wa tano katika mchujo
wa kura za maoni akitanguliwa na wenzake Dkt. Gharibu Bilali, Marehemu Hassan
Diria, Amina Salum Ali na Abdisalam Issa Khatib.
Kwa
hali yoyote Mkapa alitakiwa awaachie Wazanzibari waamue nani anayewafaa badala
ya kumpitisha kimabavu mtu ambaye labda wao walimuona kwamba hana uwezo wa
kuwaongoza.
Mifano
mingine michache ni ubabe uliofanywa kwa kupigwa virungu kwa Dkt. Fortunatus
Masha katika uchaguzi mkuu wa 2000 huko Sengerema, Mwanza. Tusisahau pia vipigo
vya polisi dhidi ya wafuasi wa TLP, dhidi ya mwenyekiti wa CUF, Ibrahim
Lipumba, n.k.
Tukirejea
nyuma kidogo, mara Mzee Ruksa alipoyumba na ikabidi Mwalimu Nyerere aingilie
kati, hakusita kusema kwamba Mwinyi binafsi hakuwa mtu mbaya isipokuwa alikuwa
na kundi la watu wabaya lilokuwa limemzunguka, je leo mwalimu angewasema akina
nani hao?
Tuwasiliane:
mhegera@gmail.com, Na: 0754-826272

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni