Mkulima wa kijiji cha Makaani Gama, Kata ya Magomeni, Wilaya ya Bagamoyo akililia ardhi yake ambayo imeporwa kwa njia za kifisadi na kukabidhiwa kwa "investor?"
Na Elias Mhegera/Januari 20/2014
Iwapo kuna jambo linaweza kusababisha vita ya wenyewe kwa wenyewe
nchini Tanzania kwa hali inayojionyesha sasa basi vita hiyo itasababishwa na
migogoro ya ardhi kama ilivyodhihirika Bagamoyo hivi karibuni.
Mgogoro wa kugombea ardhi Bagamoyo katika kijiji cha Makaani
Gama ni wa muda mrefu na wenye mtiririko wa mambo mengi ya ajabu. Siku ya
Jumapili tarehe 19, Januari (juzi) Kamishina wa ardhi Bw Gapser Luanda
alilazimika kuambatana na timu ya watendaji wake kwenda kijijini hapo ili
kusikiliza malalamiko ya wakulima.
Mgogoro huo ambao mpaka sasa umefunguliwa kesi katika
Mahakama Kuu Kitengo cha Ardhi Kesi Na: 162/2012 umekuwa ukichukua sura tofauti
tofauti kulingana na maslahi yanayokinzana ndani yake.
Awali serikali ilitoa ardhi ya Ranchi ya Zanzibar iliyotolewa
na Mwalimu Julius Nyerere kwa serikali ya Zanzibar chini ya utawala wa Mzee
Abdu Jumbe mwaka 1984. Hata hivyo baada kugawiwa ardhi mwekezaji amejitanua
katika vijiji vya jirani kama vile Makaani Gama, Fukayosi na Matipwiri na hivyo
kusababisha migogoro ya kugombea ardhi.
Moto uliowashwa hivi karibuni umetokana na jaribio la mwekezaji
kupitia kampuni ya Eco-Energy kujaribu kuandaa taratibu za kuwalipa fidia
wakazi wa maeneo hayo ili wapishe na kuachia eneo hilo kabla hata kesi ya
msingi iliyopo mahakamani ikiwa haijakamilika.
Uchunguzi wa mfafanuzi.blogspot.com
umebaini kwamba kulikuwa na mbinu ya mwekezaji au ya kigogo anayetuhumiwa
kujificha nyuma ya mwekezaji kutaka kuwagawa wamiliki wa mashamba hayo
yanayogombewa.
Mchezo uliotumika ulikuwa na wa kuwaahidi nyumba wanavijiji
waliomo katika mashamba kwa sasa ambapo inadaiwa mtoto wa kigogo aliwaahidi
wanavijiji kwamba watajengewa nyumba za kisasa na kisha kukabidhiwa funguo za
nyumba zilizokamilika.
Mbinu hiyo ilionekena kuleta mafanikio kwa kiwango chake kwa
upande wa “mwekezaji” kwani baadhi ya wanavijiji walikuwa tayari kupisha katika
eneo hilo kwa ahadi ya kujengewa nyumba hizo.
Hata hivyo mpango huo ulikutana na pingamizi kubwa kutoka kwa
wamiliki wa mashamba ambao wanaishi jijini Dar es Salaam na baadhi ya wale wa
kijiji Makaani Gama. Kwa upande wao
wanadai wapo tayari kushirikiana na mwekezaji wa Eco-Energy katika kilimo cha
miwa kwa ajili ya sukari lakini bila kuachilia ardhi yao.
Kwa upande mwingine jitihada za serikali kupitia kwa
watendaji kadhaa wa wizara ya ardhi Wilayani Bagamoyo na hata makao makuu ya
Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi akiwamo Waziri Prof. Anna Tibaijuka na Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Ahmed Kipozi zimekuwa
ni kuwashinikiza wanavijiji na wamiliki wa
mashamba kuondoka na kumpisha “mwekezaji” ili aendelee na kazi yake.
Katika mkutano wa Jumapili ilidhihirika kwamba mpango wa
tahmini ya thamani halisi ya ardhi husika tayari kwa kuwalipa fidia walengwa
ili waupishe mradi huo wa miwa haukabaliki na walio wengi.
Hata alipopewa nafasi ya kusoma kilichoandikwa katika Fomu
Na: 69 Mthamini Mwandamizi kutoka Wizara ya Ardhi Evelyn Mugasha, alisononeshwa
pale aliposikia sauti ya wengi ikiitikia kwa kishindo kwa kusema “hatutaki
fidia, hatutaki fomu zenu!”
Fomu hiyo ambayo humtambua mmiliki halali tayari kwa kufanya
uchunguzi wa kina juu ya thamani ya ardhi husika na kisha kuwalipa fidia
walengwa imeonekana sawa kabisa na sumu kwa wamiliki hao wa mashamba.
Awali kabla ya kufikiwa kwa hatua hiyo kulikuwapo na hamasa
kubwa kutoka kwa viongozi wa wamiliki hao. Mwenyekiti wao Bw Ally Mbawe
alisikika akiwahamasisha wenzake na kusema “mnataka nishambuliwe na kudhuriwa
kama ilivyokuwa kwa Dkt Stephen Ulimboka na Mhariri Absalom Kibanda? Kwa nini
wengine mnabaki nyuma katika harakati zetu? Alilalama.
Alidai kwamba kamwe haitawezekana wao waiachie ardhi yao
ambayo wameitumikia kwa muda mrefu huku wakiwa wamewekeza pesa nyingi kwa ajili
ya kuendeleza mashamba yao. “Hatuchoki mpaka…alianzisha ghani hiyo na kuitikiwa
na umati wa watu wasiopungua 800 tena kwa kishindo… “kieleweke!”.
Baada ya hapo mwenyekiti huyo alimuachia kipaza sauti katibu
wake Bw Bessa William ambaye alisema bila kutafuna neno kwamba haya ni
mapambano kati ya wanyonge na mafisadi, “usitegemee kuletewa haki yako nyumbani
kwako ni lazima iufuate ilipo” alimaka mkulima huyo kijana.
Jitihada za Afisa Ardhi Maliasili na Mazingira Bw. Clement
Mkusa kuwatuliza hasira wananchi hao hazikuzaa matunda ingawaje alidhihirisha
kwamba anaufahamu vizuri mgogoro huo na ana uwezo mkubwa wa ushawishi kwa
wananchi hao.
“Jamani mimi nimekuwa nanyi siku zote nikitaka mpate haki yenu iweje leo mnayakataa
maelekezo ya viongozi wangu kutoka wizarani? Hamuoni kwamba mnapingana na
sheria za nchi? Naomba tafadharini sana mteue watu kumi ili wawakilishe kundi
lenu na tuanze mazungumzo na serikali yenu je mnaonaje wazo hilo?” aliuliza.
Baada ya mashuriano ya kina wamiliki wa mashamba walisema
watateua wawakilishi 10 kutoka katika makundi yote yaliyoguswa na mgogoro huo.
Wawakilishi hao watatoka katika makundi ya wakulima wakazi wa makaani, makundi
ya asasi za haki za binadamu na Shirika la HakiArdhi ambalo limekuwa
likipigania haki za wanyonge katika migogoro yote ya ardhi.
Katibu Bessa alitamba kwamba wao ni kundi lililojotosheleza
na kwamba miongoni mwa watu wanaopigania ardhi hiyo wakiwakilisha wanyonge wamo
mawakili, madaktari, wahadhiri wa vyuo na wasomi wengine. “tuna hazina kubwa ya
watu wenye uelewa hatutaichia ardhi yetu hivi hivi, tutapambana,” alitamba.
Wakulima hao walitoa onyo kwa kigogo yeyote anayetaka
kuingilia mgogoro huo hata kabla hukumu katika kesi ya msingi haijatolewa
ajiendae kupambana nao popote iwapo sheria hazitazingatiwa. “mahakama ndiyo
mwisho, alisema kwa msistizo mkubwa”.
Historia inaonesha kwamba mabavu na ubabe vimekuwa vikitawala
kwa sehemu kubwa dhidi ya wanyonge hao. Kwa mfano uvunjaji wa ofisi ya Chama
Cha Mapinduzi Tawi la Makaani Gama ulifanywa hata kabla hati ya umiliki wa
ardhi haijatolewa na Kamishna wa Ardhi.
Mwandishi wa habari hizi alipomfuata Mkuu wa Wilaya Kipozi na
kumhoji alipata wapi ujasiri wa kuivunja ofisi ya CCM kabla hukumu ya Mahakama
Kuu haijatolewa wala hati ya umiliki alijibu kwa kujiamini akisema “mimi
nawakilisha maslahi ya serikali wailayani hapa, tayari serikali imemkabidhi
ardhi mwekezaji na hawa wanavijiji wanakwamisha mradi huo.
Mwandishi wa habari hizi alifika katika ofisi za Uhamiaji
Makao Makuu ili kujiridhisha iwapo taratibu za idara hiyo zilifuatwa katika
kutoa kibali cha makazi ya kwa mwekezaji wa Daraja A. Majibu ya afisa
mwandamizi mwenye cheo cha Kamishina yalidhihirishwa kwamba taratibu
hazikufuatwa.
Kwa kawaida sheria za uhamiaji zinamtaka mwekezaji ahamie
nchini baada ya kukamilisha taratibu zote ikiwamo zile za Kituo cha Uwekezaji
(TIC). Kwa mujibu wa taarifa zilizopo mwekezaji wa kampuni ya Eco-Energy, Bw. Anders
Bergfors ameishi nchini Tanzania tokea mwaka 2007 bila kuwa na shughuli yoyote
ya uzalishaji hali inayozua maswali mengi kuliko majibu.
Mahojiano kati ya mwandishi wa habari hizi na mwekezaji
yalihudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Fedha wa kampuni hiyo Bw. Amani Sinare.
Baada ya Afisa Uhamiaji wa Vibali (Residence Permits) kubanwa
na mwandishi ni kwa nini Uhamiaji walishindwa kuchukua hatua na kumshauri
mwekezaji huyo arejee nchini kwao wakati wawekezaji wenzake katika mradi huo
waliopo nchini wakitafuta muafaka, alijibu kwa kifupi, Bwana mwandishi serikali
imesema tutoe kipaumbele kwa wawekezaji wakubwa katika kilimo wewe unawasiwasi
gani?
Naye mwekezaji alipofuatwa na mwandishi wa habari hizi
kuelewa imekuwaje anaishi Tanzania tokea mwaka 2007 mpaka leo bila kazi yoyote
alijibu kwamba kampuni yao ni ya kimataifa na kwamba aliingia nchini kwa
kampuni ya SEKAB ambayo baadaye aliachana nayo na ardhi hiyo kuchukuliwa na
Eco-Energy.
“Bw Mwandishi fanya uchunguzi wako vizuri mimi nimeingia ubia
na serikali wa kuzalisha miwa katika ardhi hiyo jukumu la kunitafutia vibali
vya uhamiaji ni la serikali siyo langu,” alijibu kwa kujiamini “mwekezaji huyo”
Baada ya mwandishi kuwasiliana na Uhamiaji ili kufahamu iwapo
taratibu zimebadilishwa na kwamba sasa serikali ndiyo inawatafutia vibali
wawekezaji afisa mwandamizi wa Uhamiaji ilijibu kwa ukali kidogo, Bwana
mwandishi taratibu hazijabadilika hata hivyo siyo lazima serikali ikupatie siri
zake!
Alipaombiwa kwamba kuna usiri gani katika uwekezaji na kwamba
mwandishi huyu naye alikuwa akifuatia maslahi ya umma afisa Uhamiaji huyo
aliangua kicheko na kukata simu. Hali hii ya sintofahamu ndiyo inayozua maswali
kwamba nyuma ya mwekezaji Eco-Energy kuna mtu mzito anayetumia idara za
serikali kufaniksha mpango huo.
Huku kukiwa na lindi la kushambulia waandishi wa habari na kutoa vitisho hali mikoani pote ni hiyo
hiyo linapokuja suala la ardhi. Kwa mujibu wa taarifa ya mahitaji ya kiusalama
ambayo inahusisha mikoa 16, miwili Tanzania Visiwani na 14 Tanzania Bara
miongoni mwa watetezi wa haki za binadamu walio katika mazingira hatarishi ni
wale wanaofuatilia masuala ya ardhi.
Tuwasiliane: 0754-826272
na 0715-076272 na
barua pepe: mhegera@gmail.com
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni