Ijumaa, 18 Julai 2014

UPUNGUFU WA WALIMU TANZANIA USHUGHULIKIWE




 uhaba wa walimu huchangia katika mlundikano wa wanafunzi kama huu 

Makala hii ilitumika katika gazeti la Mtanzania Jumapili Oktoba 21, 2007
Na Elias Mhegera
Kutokana na uhaba mkubwa wa walimu wa shule za msingi na sekondari hapa nchini serikali yetu kupitia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi  ilibuni mpango wa mafunzo ya miezi mitatu kwa wahitimu wa kidato cha nne na cha sita ili kukidhi mahitaji hayo.

Mpango huo umepongezwa na baadhi ya wadau wa sekta ya elimu lakini pia wapo walioukosoa mpango huo, hoja hiyo ndiyo mjadala wa makala haya.

Licha ya kwamba kila mtu anafahamu kwamba lengo la serikali yetu ni zuri katika mpango huo lakini wadau wengi wameonyesha wasiwasi wao juu ya kiwango cha elimu na hivyo kumekuwepo na mijadala mingi juu ya suala hilo miongoni mwa walioonyesha wasiwasi wao ni Chama cha Walimu Tanzania (CWT).

Lakini serikali tayari imejibu hoja zao kupitia kwenye vyombo vya habari kwa tamko lililotolewa na Naibu Katibu Mkuu wa wizara husika Bwana Oliver Mhaiki.

Nimeshawishika kutoa mchango wangu katika mjadala kama wafanyavyo watanzania wengine na kwa kuzingatia kwamba nami pia ni mdau katika sekta ya elimu.

Kabla sijaingia katika undani wa mjadala wenyewe napenda kutanabahisha kwamba hoja ya msingi inayotolewa na wale wanaopinga walimu wa mafunzo ya muda mfupi ambao wamebatizwa mitaani kama walimu wa vodafasta.

Wamekuwa wakisimamia katika msingi wa maandalizi kwamba muda wa miezi mitatu ni mfupi na hivyo hautoshi kumuandaa mwalimu na kuweza kutoa elimu yenye kiwango kinachokidhi mahitaji ya kitaalamu.

Sipendi kuipinga hoja hiyo lakini napenda tuangalie upande wa pili wa shilingi ambao ni kutoa elimu kwa watanzania wote kwa kuzingatia kwamba elimu ni haki ya kimsingi ya binadamu.

Kwa mantiki hiyo naamini mjadala wowote wenye kufanyiwa utafiti wa kina utalenga katika mambo yote hayo mawili ubora, na haki ya vijana wetu kupata elimu.

Labda tukianza na hilo la ubora napenda niseme kwamba ubora wa elimu huchangiwa na mambo mengi na wala si ubora wa walimu pekee.

Kwa mfano mazingira ambayo elimu hiyo hutolewa, vitendea kazi, motisha kwa walimu, malezi ya watoto nyumbani na shuleni, na pia msukumo na msaada wanaoupata watoto hao nyumbani katika dhamira ya kujiendeleza kielimu

Kuhusiana na hilo la mazingira ambapo elimu yetu inatolewa taasisi ya HakiElimu imekuwa mstari wa mbele kulipigia kelele kupitia katika vyombo vya habari japo wapo ambao wamekuwa wakidai kukerwa na matangazo hayo.

Katika hilo naomba tusiangalie mazingira katika mtazamo wa madarasa na nyumba za walimu bali pia mishahara yao, usafiri wa kwenda na kurudi kutoka ofisini, na marupurupu mengine yanayoweza kumvutia mwalimu ili aipende kazi yake.

Tukiachana na hilo la ubora wa elimu tuangalie upande wa pili ambao ni haki ya kila mtanzania kupata elimu katika mazingira tuliyonayo kijamii na kiuchumi.

Naomba kuweka wazi ukweli kwamba serikali kwa muda mrefu imeshindwa kutoa vivutio kwa walimu na hivyo wanajamii wengine wamekuwa na tabia ya kuibeza taaluma hiyo bila kukumbuka kwamba kila msomi amepitia shuleni kwa msaada wa walimu haohao tunaowabeza kutokana na vipato vyao duni.

Kwa maana hiyo si sahihi kusema kwamba Tanzania ina uhaba wa watu wenye taaluma ya ualimu bali inao wataalamu wengi katika taaluma hiyo ambao wameikimbia na kwenda kupata kazi katika maeneo mengine tofauti kama vile benki, jeshi la polisi, uhamiaji, jeshi la wananchi, uandishi wa habari n.k.

Kuhama huko kwa wataalamu hao kumeacha pengo kubwa katika taaluma hiyo na hivyo kuwafanya wachache waliojitolea ‘wenye wito’ kubeba mzigo mkubwa  na wakati mwingine kuonekana kwamba ni watu wasio na upeo wa kuona mbali (vision).

Ni hao hao wanaoendelea kutupatia wataalamu huku wakiendelea kupigania kuboreshwa kwa maslahi yao kwa kweli yataka moyo!

Kumbe hao walioamua kwenda kupata mafunzo ya muda mfupi wameonesha dhamira nzuri ya kuwasaidia kaka na dada zao walioelemewa na mzigo kwa nini basi tusiwaunge mkono badala yake tunawakatisha tamaa? Kwa hoja yangu hiyo nadhani tayari nimeishaeleweka ninasimamia wapi, naomba tufanye kila jitihada kuwaunga mkono hao walijitolea (volunteers) kwa kuwapatia kila aina ya msaada ili nao wasije kimbia kama wale waliowatangulia.

Baada ya kuona kumekuwepo na vipangamizi vya hapa na pale katika jamii niliamua nifuatilie mwenyewe ili nijue huko vyuoni walikoenda kwa miezi hiyo mitatu wamefundishwa nini na kuangalia kama kile walichofundishwa kitasaidia katika jamii kulingana na mahitaji tuliyonayo na lengo zima la kuwa na jamii yenye elimu au uelewa hata kama si kwamba wote watafikia ngazi ya vyuo vikuu.

Bila kurefusha mjadala nimejifunza kwamba vijana wetu wamefundishwa na kuelewa nini maana ya elimu yaani kwamba elimu ni mfumo endelevu unaodhamiria kumuandaa mwanafunzi katika majukumu fulani katika jamii yake.

Kwa maana hiyo elimu huanzia nyumbani na wala siyo shuleni kwani katika mila zetu tuna mafunzo ambayo humuandaa kijana, humjenga kitabia, humpatia nidhamu inayohitajika na pia kumfahamisha wajibu wake katika jamii yake, kwa hiyo elimu haishii katika kusoma na kuandika pekee bali katika kujiandaa kukabiliana na maisha ya baadaye.

Jukumu la mwalimu ni kuweza kuchanganua ni zipi tabia zinazofaa ambazo mwanafunzi anastahili kufahamishwa na kwa maana hiyo mwalimu anaweza kutoa ushawishi wa matendo mema, na anaweza pia kutumika kama nyenzo ya kuongeza uwezo wa mwanafunzi katika kukabiliana na maisha yake ya baadaye.

Kwa malengo ya muda mrefu mwalimu humuandaa mwanafunzi kujipatia utaalamu utakaomuwezesha kujiajiri mwenyewe au kuajiriwa katika taasisi mbalimbali na serikali yenyewe.

Lengo mahsusi likiwa ni kujikimu katika maisha yake ya baadaye.  Kwa elimu wanayoipata wanafunzi wa sekondari ni elimu tosha inayowawezesha kujiendeleza katika ujasiriliamali, kilimo, uvuvi na mambo mengine ya kimaendeleo.

Elimu hiyo ni ufahamu tu utakaowawezesha kuyapokea vyema maelekekezo watakayopewa na wataalamu mbalimbali kama vile wa kilimo, au tasisi zinazojihusisha na wajasiriamali kama vile FINCA, PRIDE, CARE, WORLD VISION n.k. kwa hali yoyote ile elimu ni muhimu sana katika jamii ya leo ili kuendana na mazingira yaliyopo kwa sasa.

Mjadala wangu umelenga katika elimu ya sekondari kwani huko ndiko wanakoelekezwa hao walimu wa maandalizi ya muda mfupi (crash programme), Bila kujali kwamba wanafunzi wetu wametokana na walimu wa namna ile bado wanaweza kujiendeleza na kufikia ngazi za vyuo vikuu kutegemeana na jitihada binafsi ya kila mmoja wao.

Lakini hata kama itajitokeza kwamba wanafunzi wetu wasibahatike kuipata elimu ya vyuo vikuu bado elimu wanayoipata katika sekondari inaweza kuwasaidia katika maisha yao ya kila siku.


Kwa mfano somo la uraia yaani civics limesheheni elimu inayoweza kumsaidia mhitimu uelewa wa kutosha katika jamii yake kama vile masuala ya demokrasia, elimu juu ya UKIMWI. Maadili mema na njia mbalimbali za kuondokana na umaskini.Ndani ya elimu ya uraia kuna mbinu za kilimo endelevu ambacho hakitaathiri mazingira, kuna haki za binadamu n.k.

Silengi kuwaambia vijana wetu wakomee kidato cha nne kwa sababu elimu hiyo imejitosheleza bali nataka kueleza kwamba kwa yule ambaye hatabahatika kukanyaga chuo kikuu asijione kwamba ana mkosi bali elimu ilivyoandaliwa kwa mtaala wa sasa imelenga katika kumuandaa katika maisha yake ya baadaye hata kama hatafanikiwa kupata elimu ya juu. Ni lazima pia tukumbuke kwamba bado tuna uhaba mkubwa wa vyuo vikuu na wahadhiri kwa hiyo safari bado ni ndefu katika medani ya elimu nchini Tanzania.

Tukirudi katika hoja yetu ya msingi je hao walimu wa mfunzo ya muda mfupi wanaweza kutoa elimu hiyo niliyoizungumzia hapo juu? Jibu ni ndiyo kwa sababu kulingana na kile nilichokiona walichojifunza vijana wetu ni kwamba japo mafunzo wanayopata ni ya muda mfupi lakini pia tukumbuke kwamba wao ni wahitimu katika elimu ya sekondari  kwa hiyo wanachoongezewa huko vyuoni ni mbinu tu za ufundishaji.

Katika vyuo hivyo walimu hao hujifunza mambo kadhaa yanayoweza kuathiri au kufanikisha  uelewa wa mwanafunzi  (learning process)). Katika mbinu hizo walimu hufundishwa tabia na mambo ambayo wanaweza kukabiliana nayo darasani na jinsi ya kuyakabili.

Kwa maana hiyo walimu hao hupewa nyenzo zinazoweza kuwasaidia katika kuwaelekeza wanafunzi wao kwa  mambo yaliyo muhumu katika maisha yao na kuachana na yale ambayo yanaweza kuathiri maisha yao kama vile matumizi ya madawa ya kulevya, ulevi na uovu mwingine.

Kwa kufanikisha hilo walimu huelekeza nguvu zao katika falsafa na matarajio ya taifa letu kwamba kijana wa kitanzania anatakiwa awe wa aina gani kwa hiyo vijana hupata maelekezo sahihi  kulingana na utamaduni wetu na kwa kutumia maelekezo sahihi ya wanafalsasa wa elimu kama vile Mwalimu Nyerere na falsafa yake ya elimu ya kujitegemea.

Pia walimu hao huweza kung’amua ni jinsi gani ya kuwasaidia watoto wetu au vijana wenye matatizo mbalimbali ambayo yanaweza kuathiri uelewa wa mwanafunzi  kwa mfano ufukara uliokithiri nyumbani, malezi mabaya, n.k.

Pia walimu hao huweza kung’amua ni jinsi gani ya kuwasaidia watoto wetu au vijana wenye matatizo ambayo yanaweza kuathiri uwezekano wa wao kupata elimu kwa kiwango sawa na wenzao wasio na matatizo ya kijamii.

Ina maana japo walimu hao wamepewa mafunzo ya muda mfupi lakini pia wamefundishwa mbinu za ufundishaji na mazingira yanayoweza kuathiri au kusaidia kueleweka kwa somo na wala siyo kwamba baada ya kutoka vyuoni basi ndiyo ukomo wa wao kujifunza bali wanaweza kujiendeleza kwa njia mbalilmbali  kwa mfano kwa kuazima vitabu katika maktaba, kwa kujiendeleza katika Chuo Kikuu Huria n.k.

Basi ni vyema tuelewe mbinu walizofundishwa kulingana na kile nilichokipata mimi baada ya utafiti wangu binafsi.

Vijana hao wamefundishwa tabia na mienendo ya binadamu juu ya uelewa kutokana na tafiti zilizofanywa na wataalamu kama vile Ivan Pavlov ambaye alifanya utafiti wake akiwahusisha mbwa pale mbwa anaposikia mlio wa kengele na kufahamu kwamba huo ni muda wake wa kupata chakula.

Kwa hiyo tafiti hizo zimeingizwa katika mbinu za ufundishaji kwa walimu. Mambo mengine waliyojifunza ni umuhimu wa kurudia somo, ubaya wa adhabu, na adhabu zinazostahili kwa wanafunzi na motisha mbalimbali ambazo zinaweza kuchagiza katika wanafunzi kuongeza jitihada katika masomo yao (positive reinforcements).

Ninapotetea kuwepo walimu wa aina hiyo ni kwa sababu nimeridhika kwamba japo kuna malalamiko kwamba wanaweza kushusha kiwango cha elimu lakini wakosoaji wengi wameshindwa kupendekeza njia mbadala ya kuisadia serikali yetu kukabiliana na upungufu wa walimu.

 je wakosoaji hao wamejipa nafasi ya kufuatilia nini walichofundishwa walimu wetu hao? Binafsi ninapoangalia kile walichofundishwa na kwa kuzingatia kwamba elimu ni haki ya kimsingi ya binadamu naona serikali imechukua uamuzi wa busara ili kuwapa uwezo wale ambao walikuwa wamesahaulika.

Kwa mfano katika baadhi ya mambo ambayo wamefundishwa walimu wetu hao tunaowabeza ni jinsi mihemuko (emotions) inavyoweza kuathiri tabia za vijana katika rika fulani hivi elimu kama hiyo nayo lazima ukae miaka minne chuoni ndipo uonekane kwamba umeiva?

Baada ya kuupitia mtaala wao nimejiridhisha kwamba mbinu walizopewa japo ni kwa mafunzo ya muda mfupi lakini zinagusa maeneo mengi yanayomuwezesha mwanafunzi kupata uelewa darasani (cognitive domains).

Kwa hiyo kinachofuata sasa ni jinsi ya kuyaweka katika utekelezaji yale waliyofundishwa jambo hilo linategemeana na uwezo au kipaji cha kila mmoja.

Mtaalamu wa saikolojia Robert Gagnèanasema suala la uelewa halitegemei tu nini kimefundishwa darasani lakini pia uwezo wa mwanafunzi mmoja mmoja kutafsiri kile alichojifunza. Katika hilo anasema wapo wenye uwezo wa kushika mara moja kile walichojifunza, wapo wenye uwezo mdogo wa kuelewa na hivyo wanahitaji muda mrefu wa ziada ili kuelewa kile walichojifunza  na lipo kundi la tatu ambalo ni kama la wasindikizaji kwani wao huchukua muda mrefu zaidi kuelewa somo hilo hilo ambalo wenzao wamelielewa kwa muda mfupi tu.

Ninaungana mkono dhana hiyo kwa sababu sote tunafahamu kwamba wapo watoto wetu ambao bila tuisheni mambo hayaendi, wapo pia ambao kuwatafutia walimu wa tuisheni ni sawa na kupoteza pesa zetu bure kwani huelewa somo mara walipatapo darasani.

Katika msingi huo siyo sahihi kabisa kumlaumu mwalimu na kwa maana hiyo tunapojadiliana uwezo wa wanafunzi kuelewa ama kutokuelewa tusikimbile kuwatupia lawama walimu wa kitanzania bali tuangalie mazingira yote hayo na jinsi ambavyo yanaweza kuathiri taaluma kwa ujumla.

Mtaalamu huyo Gagnèanasema njia sahihi ya kutatua tatizo hilo ni kuwatenganisha wale wenye vipaji maalumu na wale wenye uwezo mdogo wa kuelewa (slow learners).

Maana yake ni kwamba kama wanafunzi hao wataendelea kukaa katika darasa moja basi mwalimu atalazimika kurudia mara kadhaa kwa lengo la kuwasaidia  ‘slow learners’ hali hiyo inaweza kuwakera ‘fast learners’. Naamini serikali yetu ilizangatia ushauri huo wa kitaalamu na ndiyo maana kukawepo na shule zenye vijana wenye vipaji maalumu.

Lakini hii haimaanishi kwamba ‘slow learners’ watelekezwe kwani hata wao mara baada ya kurudia mara kadhaa wanaweza kujikuta wamepata uelewa sawa na wenzao lakini katika kundi la tatu huko ndiko ambako muda wa ziada huhitajika na wala si kwamba hali hiyo hujitokeza katika shule za sekondari pekee bali hata katika ngazi ya vyuo vikuu inaweza kujitokeza.

Nikilenga kuonyesha kwamba serikali inaweza kuwatumia vipi walimu hao wa muda mfupi basi labda uwepo utaratibu ambao utawawezesha wahusika kufanya kazi katika shule za kawaida badala ya kuwapeleka katika shule za watoto wenye vipaji maalumu tukifanya hivyo tunaweza kuondosha tatizo la uhaba wa walimu bila kushusha ubora wa elimu yetu hususani katika shule za sekondari na zile za msingi.

Pamoja na kuzingatia ubora wa elimu bado ni muhimu tukumbuke pia kwamba suala la elimu ni haki na hasa kwa kuzingatia ukweli kwamba elimu ya msingi imepitwa na wakati  kulingana na mazingira ya sasa kwa mantiki hiyo lengo liwe ni kuhakikisha kila mtanzania anapata elimu ya kiwango cha chini isiyopungua kidato cha nne.

Tamko la haki za binadamu la mwaka 1948 linasema elimu ni mojawapo katika haki za msingi za binadamu, kwa wakati ule elimu iliwekwa katika fungu la tatu la haki za binadamu lakini kwa wakati tulionao elimu inatambuliwa kwamba ni haki ya kimsingi na hivyo ni haki iliyo katika daraja la kwanza (fundamental rights).

Katika hilo napenda kuwakumbusha wale wote wanaobeza jitihada za serikali kutoa elimu ya sekondari kwanza kwa kudai kwamba serikali imefanya papara kwa kujenga sekondari za kata, na pili kwa kuwaruhusu hao walimu wa muda mfupi kufundisha kwamba wameonesha kukosa uzalendo na fadhila kwa serikali yao kwa sababu hawajatoa suluhisho mbadala.

Kimsingi serikali isingeweza kuchukua uamuzi ule kwa lengo la kuwadhuru wananchi wake, isipokuwa kuna ukweli kwamba katika dhamira njema hiyo ya serikali yapo mambo kadhaa ambayo pia hayakuzingatiwa.

Katika hilo sina pingamizi, kwa mfano ubora wa baadhi ya majengo ya sekondari za kata unatia mashaka, nimeshuhudia majengo mengi ya sekondari za kata yakianguka hata kabla hayajaanza kutumika.

Katika hoja hiyo hiyo kuna tatizo la mazingira ambamo shule hizo zimejengwa.Jambo hilo ni la kisera zaidi na pia linaendana na mwenendo mzima wa siasa za nchi yetu kwa sasa yawezekana kuna utetezi kwamba hali ya uchumi ni mbaya.

Kwa mfano tukifuatilia kwa makini tutaona kwamba ni kata chache sana nchini zenye huduma muhimu kama vile maji na umeme hiyo ni pamoja na miundo mbinu mingine kama vile barabara zinazopitika katika kipindi cha mwaka mzima.

Mazingira ya aina hiyo yanaweza kuondosha ari za walimu kufanya kazi katika sekondari hizo ambazo zimechipuka kama uyoga nchini pote.

Sanjari na hilo ni urasimu uliopo katika Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi yawezekana urasimu huo unatokana na uendeshaji mbaya lakini pia inawezekana kwamba wizara hiyo imeelemewa na mzigo kutokana na ukweli kwamba imeajiri watu wengi kuliko wizara yoyote nchini.

Mwaka 1990 rais wa awamu ya pili Mzee Ali Hassan Mwinyi aliunda Wizara ya Sayansi Teknlojia na Elimu ya juu katika kupunguza mzigo uliokuwa unaikabili wizara ya elimu kwa wakati ule. Pamoja na jitihada hizo bado matatizo ya shule yanaelekezwa katika halmashauri za wilaya lakini bado inaonekana jitahada zote hizo hazijapunguza kwa kiwango kikubwa matatizo yanayoikabili wizara hiyo.

Pamoja na kuzidiwa na mzigo wa uendeshaji kutokana na wingi wa shule bado kuna tatizo la mfumo usiozingatia haki ambapo watendaji wizarani hupendelea kusikiliza upande mmoja yaani wa wakuu wa shule bila kuwasikiliza walimu ambao ni wataalamu na taifa limewaelimisha kwa gharama kubwa kwa hiyo yote hayo ni mazingira yanayostahili kuzingatiwa katika dhamira ya kuboresha viwango vya elimu katika sekondari zetu.

Ukiondoa mapungufu hayo machache naamini wizara husika inajitahidi kwa kiwango kikubwa katika jukumu lake la kutoa elimu kwa watanzania wote bila ubaguzi wa dini, kanda, kabila, rangi na mambo kama hayo.

Yapo marekebisho machache yanayohitajika ili kuwavutia walimu waendelee kuipenda taaluma yao  (retention scheme)  kwa hiyo wizara inatakiwa kubuni mbinu za kutoa motisha kwa walimu.

Kwa sababu wote tunaona umuhimu wa watoto wetu kupata elimu bora ni muhimu pia tukatoa mchango wetu wa jinsi ya kuboresha elimu nchini badala ya kuwa wakosoaji wazuri bila kutoa njia mbadala.

Naomba kutoa changamoto hiyo kwa wakosoaji wote na hasa ikizingatiwa kwamba mwishoni mwa miaka ya sabini serikali ilianzisha mpango wa elimu ya msingi kwa wote Universal Primary Education (UPE).
Mpango huo pia ulikutana na upinzani kama huu ulijitokeza sasa. Wapo waliodiriki kuwakejeli walimu wale kwamba walikuwa walimu weupe kwa maana ya kwamba hawakuwa na lolote vichwani mwao.

Basi na tuwape nafasi hawa walimu wetu badala ya kuwavunja moyo, lakini si kwamba tuangalie upande huo wa kwamba watatoa elimu tu bali kwamba hiyo ni njia mojawapo ya serikali kutoa ajira kwa vijana wake ambao vinginevyo wanaweza kijiingiza katika vitendo viovu kutokana na kusahauliwa na serikali yao.

Tukumbuke ambavyo serikali imekuwa ikiahidi kutoa ajira kwa vijana mara kwa mara hatuoni kwamba kwa njia hii serikali imefanikiwa kwa kiwango fulani kupunguza ukali wa maisha kwa vijana wetu ambao katika umri wao hutawaliwa na ndoto nyingi labda kutokana na vyombo vya habari ambavyo vianaonesha mambo ambayo wakati mwingine hayaendani na hali halisi?

Jambo la muhhimu ni kuwaongoza ili wakamilike katika dhamira yao (professional guidance). Kwa mfano tukiangalia katika jeshi la wananchi tutakuta wapo askari wengi ambao walianzia katika ngazi ya mgambo lakini wamewezeshwa na kupanda ngazi mbalimbali hadi kufikia viwango vya juu jambo hili linafanyika katika taaluma nyingi, jeshi la polisi, magereza.  

Katika mahospitali wapo wahudumu ambao baadaye wamegeuka na kuwa wauguzi wazuri au hata madaktari kwa nini isiwe katika ualimu?

Na wala  si hivyo tu hata tukienda katika vyuo vikuu tutawapata wahadhiri waliobobea ambao walianzia katika ngazi ya ukutubi na wameweza kupanda hadi kufikia ngazi ya uprofesa kamili katika fani ya uandishi wa habari wapo waandishi walioanzia katika ukarani leo ni waandishi maarufu.

 Naamini mifano hiyo michache inatosheleza kuonesha kwamba si jambo jema kuwabeza walimu hao waliobatizwa huku mitaani kwamba ni walimu wa vodafasta bali waungwe mkono kwa kila hali na serikali, wadau na wananchi wote kwa ujumla.

Nategemea mjadala haujafungwa bado upo wazi kwa kila mtanzania kuchangia ili mradi uchangiaji huo uwe una lengo la kufanikisha kwa maana ya kujenga wala siyo kubomoa ni ukweli usiopingika kwamba vyama vya kitaalamu kama CWT vinayo nafasi kubwa ya ushawishi katika masuala yanayohusiana na elimu lakini pia tusisahau kwamba elimu ni haki ya kimsingi ni vyema tukawawezesha na wenzetu wakaipata kama tulivyobahatika kuipata sisi.

Naamini mawazo yangu yatachukuliwa katika mtazamo chanya kwamba yametolewa kwa kuzingatia haki za binadamu na wala si katika misingi ya kisiasa

Mwandishi wa mkala haya anapatikana kwa simu 0754 826 272
Na kwa barua pepe mhegeraelias@yahoo.com



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni