Pichani: Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akizungumza na wanakijiji wa
Mtanzania Januari 16, 2013 wakati alipokwenda kuwapa pole kufuatia
uvamizi waliofanyiwa na watu wanaosadikiwa kuwa wafugaji ambao waliua
watu watatu na kuchoma nyumba . Kulia kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Manyara,
Erasto Mbwilo.
Na Elias Mhegera
Asasi za kiraia
na wadau wa ardhi wameendelea kuonyesha wasi wasi wao kutokana na kushindwa kwa
serikali kukabiliana na migogoro ya ardhi ambayo tayari imesababisha madhara
makubwa ikiwamo kupotea kwa maisha ya watu kadhaa.
Wasi wasi huo
ulijidhirisha katika mjadala uliondaliwa na asasi ya uchambuzi wa sera na
mipango ya Policy Forum ukiwa ni mdahalo wa kumaliza mwezi Januari.
Mdahalo huo
uliofanyika katika ukumbi wa British Council tarehe 31 Januari, ambapo
ilidhihirika kwamba migogoro ya ardhi imeporomosha uchumi wa taifa kwa kiwango
kikubwa.
Mdahalo wenye
kichwa cha habari “Migogoro ya Ardhi na Misitu ni Suala la Kiutawala? Ulilenga
katika kuchambua vyanzo vya migogoro ya ardhi, athari zake kwa taifa na
kushauri juu ya ufumbuzi wa migogoro hiyo.
Mada ya ufunguzi
ilizungumzia uhusiano uliopo kati ya uwekezaji katika kilimo na migogoro ya
ardhi, na mtoa mada Bw Alais Morindat ambaye ni mshauri mwelekezi wa masuala ya
ardhi na mazingira akiwakilisha taasisi ya Institute for Environment and
Development (IIDE).
Mtaalamu huyo
alisema kwamba migogoro mingi imekwama kwa sababu ya kukosekana kwa utashi wa
kuisuluhisha kutoka serikalini. “Huwezi kupata ufumbuzi wa migogoro ya ardhi
kwa kuanza na fikra kwamba tabaka moja halitikiwi kuwapo” alisema Morindat.
Alikuwa
akiirejea kauli ambayo mara kadhaa imekuwa ikitolewa na viongozi mbali mbali
akiwamo Rais Kikwete kwamba ufungaji wa makundi makubwa ya ng’ombe umepitwa na
wakati.
Kwa bahati mbaya
kauli hiyo imekuwa pia ikitolewa na wanamazingira wengi licha ya wanasiasa.
Hata hivyo mtaalamu huyu ambaye anaweka bayana kwamba anatoka katika jamii ya
wafugaji wa Kimasai anapingana na dhana hiyo.
Anasema ufugaji
wa kienyeji ni suala la kimila na kiutamadani licha ya kwamba pia ufugaji umekuwa
na mchango mkubwa katika pato la taifa.
Anautetea
ufugaji kwamba hauna madhara makubwa katika ardhi na kinyume chake kinyesi cha
mifugo husaidia kuongeza rutuba na hata kwa kutengeneza gesi na hivyo kuokoa
miti na mazingira kwa ujumla.
Anatetea kwamba
wafugaji wamekuwa wakifanya mambo makubwa kiuchumi kwa sababu wanafanya
shughuli mbili kwa pamoja, kilimo na ufugaji kwa wakati mmoja.
Hivyo basi
anaulaani mtazamo hasi dhidi ya wafugaji hususani wale wa kimasai ambao
huonekana kwamba ni watu walioachwa nyuma, wakorofi na wasiopenda kubadilika
“huu ni mfumo mbaya na unawadhalilisha wafugaji,” anatetea.
Anayachambua
mambo kadhaa anayodai kwamba ndiyo chimbuko la kuwatenga na kuwabagua wafugaji.
Kwanza anasema ni mitazamo ya kiutandawazi inayolenga kukamata ardhi ya Afrika
kwa kisingizio cha uwekezaji.
Pia anasema
kwamba watunga sera wanatakiwa kuwa makini badala ya kukurupuka na kuanza
kutimiza mambo kadhaa kisiri siri kabla ya kuwashirikisha wananchi, anasema
jambo hili ni hatari kwa mustakabali wa usalama wa nchi.
Anashauri kwamba
badala ya kutafuta namna ya kuondokana na ufugaji wa kimila serikali inatakiwa
kupanga mikakati ya kushirikiana na sekta nyingine kwa lengo la kuwaendeleza
wafugaji hao.
Na zaidi ya hayo
adai kwamba serikali haiwezi kujivuna kwamba inazingatia haki za binadamu na
utawala bora wakati ikishindwa kulilinda tabaka kubwa la wazalishaji
linaloelekea kuangamia.
Katika kuachana
na dhana ya utetezi wa kundi la wafugaji, muwasilishaji mwingine Bw Steven
Mariki ambaye ni Mkurugenzi wa Taifa wa Mradi wa Uratibu wa Madhara ya
Mabadiliko ya Tabia Nchi katika Ofisi ya Makamu wa Rais (UNDP) anakuja na
mtizamo tofauti.
Analiangalia
tatizo la migogoro ya ardhi katika mtazamo mpana zaidi na kusema kinachotokea
sasa ni hitimisho la matatizo yaliyojengeka kwa muda mrefu. Anasema kwamba
matatizo ya sasa yanatokana na udhaifu uliosababishwa na mambo mengi.
“huwezi
kuielezea migogoro ya ardhi kwa kutumia kiashiria kimoja, bali unatakiwa
kufahamu kwamba kuna udhaifu katika sera zaardhi, katika sheria na hata katika
mchakato wa kupanga vipaumbele vya taifa” anadokeza.
Akifafanua zaidi
anasema kwamba mabadiliko ya kisiasa na kiuchumi duniani pia yamechangia sana
katika migogoro ya ardhi inayoendelea nchini.
Kwa mfano;
utolewaji wa fedha za wafadhili kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya kilimo
umesababisha watu ambao hapo zamani hawakuwa na mawazo ya kujishirikisha katika
kilimo kuhamia huko ghafla.
Pia anasema
kujengeka kwa miundombinu ya barabara kumesababisha watu wengi kuyafikia kwa
urahisi zaidi maeneo ambayo hapo zamani yalikuwa na changamoto kubwa.
Lakini pia
anasema sera za uwekezaji katika kilimo, kwa malengo mbali mbali kama vile
uzalishaji wa mazao kwa ajili ya uzalishaji wa nishati kama vile miwa na
jatropha yamechangia katika kukithiri kwa migogoro ya ardhi.
Anakiri kwamba
kwa bahati mbaya uwekezaji huo umeambatana na kuondolewa kwa nguvu kwa wakulima
katika maeneo yao vijijini kwa lengo la kuikabidhi ardhi yao kwa “wawekezaji”.
Anasema yapo
matatizo mengi ikiwamo udhaifu wa uendeshaji katika wizara ya ardhi ambao
husababisha urasimu na wakati mwingine hata hutokea watu kadhaa wakagawiwa
ardhi hiyo mara mbilimbili kama siyo tatu na mamlaka hiyo hiyo.
Bw Mariki
anasema kwamba hata kabla ya kuingia kwa ukoloni watu wa makabila mbali mbali
waliweza kujipangia matumizi ya ardhi na kubakia na amani lakini leo migogoro
yote inaishia mahakamani ambako kuna ucheleweshaji mkubwa wa kupatikana kwa
ufumbuzi.
Kwa upande wa sera
na mipango ya ardhi anasema kwamba lipo tatizo la kuachana na mipango ya muda
mrefu ya matumizi ya ardhi na kukimbilia katika mipango mipya isiyoeleweka
vizuri.
“Inashangaza
kuona kwamba ardhi iliyowekewa mipango ya muda mrefu kwa ajili ya uhifadhi wa
vyanzo vya maji mara inageuzwa kuwa kwa ajili ya uwekezaji na hata ardhi kwa
ajili ya vijiji inageuzwa kwa ajili ya mwekezaji, haya ni mabadiliko hasi
yanayoleta mkanganyiko mkubwa, “ anaonya.
Anashauri kwamba
kabla ya Kituo cha Uwekezaji (TIC) kupokea maombi iwasiliane kikamilifu na
taasisi nyingine ili kuepuka uwezekano wa migogoro ya ardhi. Anashauri kwamba
kabla ya serikali kugawa ardhi iwashirikishe wadau wengine zikiwamo asasi za
kiraia.
Katika michango
ya mawazo kutoka kwa wadau mbali mbali wanaonesha hasira kwamba serikali
imewatupa wanyonge tofauti ni ilivyokuwa enzi za Mwalimu Julius Nyerere, Baba
wa Taifa la Tanzania ambaye alitoa kipaumbele kwa maendeleo ya vijijini likiwamo
suala la usalama.
Prof. Adolfo
Mascarenhas anasema kumekuwapo na udanganyifu mwingi juu ya malengo mahsusi ya
ardhi inayochukuliwa, “siamini kwamba ardhi yote inayochukuliwa ni kwa ajili ya
uwekezaji, na wala siamini kwamba kila kampuni inayotajwa ni kampuni halisi,
baadhi ya makampuni ni bandia kwa lengo la kupora ardhi tu” anaonya.
Hoja yake
inaungwa mkono na afisa mipango ambaye pia ni mwanasheria kutoka HakiArdhi Bw
Godfrey Massay anayesema kwamba kumekuwapo na kampeni kubwa katika vyombo vya
habari kwamba kuna wawekezeji watakaotoa ajira lakini mwisho wa siku wakulima
wanaoondolewa wala hawalipwi fidia.
Anadai jambo la
kushangaza zaidi ni kwamba ardhi inabakia bila uzalishaji kwa muda mrefu hali
inayooongeza umaskini hususani katika maeneo ya vijijini ambako ndipo kuna idadi
kubwa ya Watanzania.
“Kuna maeneo
mengi ambayo sasa hayazalishi kwa sababu eti wamekabidhiwa wawekezaji au kwa
sababu yapo katika kesi mahakamani na hivyo shughuli za uzalishaji zinasimama,”
anafafanua.
Naye Bi Ashura Kayupayupa
anayejitambulisha kwamba ni mwanaharakati wa haki za vijana anasema kwamba umilikishwaji
wa ardhi Tanzania unautata mkubwa kwa sababu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, anaweza kutoa tamko la kuchukua sehemu kubwa ya ardhi kwa kile
kinachoitwa manufaa ya umma lakini bila kuwafafanulia wananchi kwamba ni
manufaa gani hayo.
Maneno hayo
yanamnyanyua katika kiti Bw. Francis Uhadi kutoa Norwegian Church Aid anayesema
kwamba akiwa mtumishi wa asasi ya mtandao wa masuala ya ardhi, Tanzania Land
Alliance (TALA) alijifunza mengi juu ya dhulma zinazofanyika dhidi ya wanyonge.
“Kuna ulaghai
mkubwa katika uporaji wa ardhi, wanyonge wanaambiwa watoe vyeti au nyaraka za
kuthibitisha mikataba ya umiliki wakati inafahamika kwamba mambo hayo
hayakuwahi kupewa kipaumbele kwa muda mrefu, kinachosumbua si udhaifu wa sheria
bali ni tamaa za wanasiasa na matajiri wengine, ambao hawataki kuzingatia
sheria,” anasema kwa sauti ya ukali.
Anafafanua
kwamba leo taasisi za umma kama vile TIC, inaweza kutumika kisiasa kiasi kwamba
hao hao waliokuwa wanazungumzia uwekezaji katika miwa kwa ajili ya nishati sasa
hivi wamehamishia masikio ya Watanzania kwenye gesi asilia huku tayari wakiwa
wamejilimbikizia ardhi za wanyonge.
Naye Bw Geoffrey
Mwanjelwa anasema kwamba anahofu juu ya kile kinachoitwa ushirikiano kati ya
sekta binafsi na serikali “Public –Private Partnership” (PPP), anasema huo ni
mfumo mwingine wa wanasiasa wetu kujinufaisha na mali za umma.
“huwezi kujua
nani anamiliki hiyo sekta binafsi kwani unaweza kuwa ni mradi wa mwanasiasa na
akatumia nafasi yake kuipatia kampuni yake iliyosajiliwa kwa jina la mtu
mwingine,” anafichua na kusababisha kicheko ukumbini.
Anasema kila
siku kuna miradi na mipango mipya kama ilivyokuwa kwa Kilimo Kwanza na hata Southern Agricultural Growth Corridor of Tanzania (SAGCOT) ambao yeye anauona kwamba ni muendelezo wa mikakati
hiyo hiyo ya kupora ardhi za wanyonge na kuwaacha katika lindi la umaskini.
Naye
mtaalamu wa misitu Bw. Kahana Lukumbuzya anasema kwamba pamoja na kwamba watu
wenye nafasi wamekuwa na tamaa ya kujilimbikizia mali, lakini pia kumekuwapo na ongezeko kubwa la
Watanzania ambao kabla ya uhuru walikuwa chini ya milioni kumi lakini leo
wanakaribia milioni 50.
Hata
hivyo hoja hiyo ilimnyanyua tena Prof Mascarenhas akipinga vikali kwamba hoja si
ongezeko la idadi ya watu bali ni ongezeko la ubinafsi na tamaa mchango huo
unasabibisha vicheko vingi ukumbini.
“Tumepoteza
tunu za umoja wa kitaifa” anasema kwa kujiamini mzee huyo ambaye amekwisha vuka
umri wa zaidi ya miaka 70.
Naye
Bi Maureen Kwilasa ambaye ni mtetezi wa masuala ya jinsia ambaye kwa sasa yupo
katika mafunzo kazini katika shirika la Oxfam anasema kwamba wakati kunapokuwa
na mijadala juu ya migogoro ya ardhi mara nyingi wataalamu husahau kuangalia
athari za ziada kwa watoto na akina mama.
Anakumbusha
kwamba migogoro ya siku hizi huendana na ukatili na uvunjifu mkubwa wa haki za
binadamu ambayo huwaathiri zaidi wanawake na watoto ambao hawawezi kuchukua
silaha na kukabiliana na wavamizi.
Bw
Laurent Joshua kutoka Tume ya Haki za Binamu na Utawala Bora (CHRAGG) anasema
kwamba kulingana na tafiti zilizofanywa na taasisi yake migogoro mingi ya ardhi
husababishwa na rushwa.
Hoja
hiyo inaungwa mkono na mwansheria kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu
(LHRC), Bw. Paul Mikongoti ambaye anasema kituo chake pia kimepata taarifa za
kuwepo na matumizi ya rushwa katika upatikanaji wa ardhi hali ambayo mwishowe
husababisha migogoro mikubwa.
Anakumbusha
hali yenye utata ya bonde la Kapunga ambayo ilimfanya Waziri wa Ardhi na
Maendeleo ya Makazi Prof. Anna Tibaijuka kushindwa kutoa msimamo unaoeleweka
hali inayoonyesha kwamba kuna utata katika baadhi ya maamuzi ya serikali.
Maeneo
yanayotajwa kuwa na migogoro hatarishi kwa sasa ambayo hupoa na kuibuka tena ni
pamoja na maeneo mengi mkoani Morogoro, Bonde la Ihefu, Kilombero, Ulanga,
Basuto, Bonde la Mto Rufiji, Mvomero, Kiteto, Simanjiro, Loliondo, Babati na
Mpanda.
Mwaka
2010 ikiwa ni siku chache kabla ya Uchaguzi Mkuu Mbunge wa Maswa Mashariki? Bw.
John Shibuda alisema kwamba kumekuwapo na ubaguzi wa namna masuala ya wafugaji
yanavyoshughulikiwa akidai kwamba wafugaji wa Kisukuma hawana msaada kama
ilivyokuwa kwa makabila mengine ya wafugaji.
Haileweki
kauli yake hiyo ilikuwa na ukweli kwa kiwango gani au ililenga kupata manufaa
ya kisiasa na ndiyo maana itatolewa kwa wanahabari. Lakini msimamo kama huo
unaungwa mkono na mfugaji wa kisukuma aliyepo Mkoa wa Katavi Dom training
ambaye anasema kwamba wafugaji wanahangaika na makundi yao ya mifugo baada ya
kufukuzwa eneo moja kwenda jingine.
Hivi karibuni
mwandishi wa habari hizi alishuhudia habari katika mojawapo ya vituo vya televisheni
wananchi wa Babati ambao walikuwa na kilio kikubwa baada ya kuchomewa nyumba
zao na watu waliodaiwa ni askari wa wanyama pori kutoka katika Wizara ya
Maliasili na Utalii.
Akijibu hoja za
mwandishi wa habari za televisheni Mkurugenzi Mtendaji wa TANAPA Bw. Alan
Kijazi alisema nyumba zilizochomwa ni za watu waliolipwa fidia miaka minane
iliyopita lakini walikuwa wamekaidi agizo linalowataka wahame katika maeneo ya
hifadhi.
Hoja ya Kijazi
kwamba walioondolewa watapewa maeneo mengine ilipingwa vikali na wananchi hao
huku mmoja wao akitamka “eti wanasema watatulipa fidia hatutaki fedha tunazo za
kutosha, tunataka ardhi yetu” alimaka.
Kauli za
wanavijiji hao zinawakilisha wananchi wengi ambao wanasema serikali imekuwa haiwashirikishi
kikamilifu katika kuchukua ardhi bali inawaburuza kwa kutumia vitisho na Jeshi
la Polisi, ikiwamo uchomaji wa nyumba za wakulima.
Mkuu wa Wilaya
ya Babati Bw. Khalidi Mandia naye anadai kwamba wananchi walikwisha lipwa fidia
na anaonekana hana majibu ya uhakika kwa wananchi wenye hasira isipokuwa
anaweza kutimiza tu “maagizo ya serikali” ya kuwaondoa katika maeneo
yanayodaiwa kuwa ni ya hifadhi.
Asasi za kiraia
zinashauri kuwepo na uwazi na uhakiki zaidi juu ya wamiliki halisi wa hayo
yanayoitwa ni makampuni ya wawekezaji ambapo kumekuwapo na tabia ya viongozi wa
juu serikalini kuanzisha makampuni bandia na kudai eti ni ya wawekezaji kwa
lengo la kupora ardhi.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni