Mtanzania Jumapili Novemba 18, 2007
Na
Elias Mhegera
Rais Barack Obama wa Marekani, taifa moja miongoni mwa wafadhili wakubwa Tanzania
Hivi
karibuni serikali kupitia kwa waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa Bernard Membe iliwakumbusha (onya?) mabalozi wanaoziwakilisha nchi
zao hapa nchini kwamba hawatakiwi kuingilia mambo ya ndani ya nchi kama inavyotakiwa
katika makubaliano ya kidiplomasia ya Vienna (Vienna Covention).
Msingi
wa hoja hiyo ulitokana na shinimkizo la mabalozi kuitaka serikali itoe tamko
kuhusiana na tuhuma za ufisadi zinaoelekezwa kwa baadhi ya viongozi wake. Makala
haya yanatathmini uhalali wa mabablozi kutoa tamko lao.
Sote
tunafahamu kwamba mabalozi wawapo katika nchi wanakowakilisha (receiving countries),
hujitahidi kujifunza tamaduni, taratibu na kanuni za uendeshaji wa nchi hizo.
Lengo la kufanya hivyo ni kuzuia uwezekano wa kugongana kidiplomasia na nchi
wenyeji wao na hivyo hujaribu kulinda uhusiano uliopo badala ya kuudhofisha kwa
namna yoyote ile.
Hata
hivyo si kila wakati wana diplomasia wamekuwa wakimya wanapoona mambo
yanakwenda ndivyo sivyo katika nchi wenyeji wao, na ndipo hulazimika kutoa
tamko lao kuonyesha kutoridhishwa na mwenendo au mienendo ya nchi iliyowapokea.
Kelele za kudai mabalozi na wahisani wasiingilie mambo ya ndani ya nchi
hazijaanza leo. Mwaka 1994 nchi wahisani zilimshauri Rais Mstaafu wa awamu ya
pili Mzee Ali Hassani Mwinyi kumuwajibisha waziri wa fedha kwa wakati ule
Hayati Profesa Kighoma Malima.
Mara
Mzee Mwinyi na waziri wa mambo ya nje kwa wakati ule Hayati Hassan Diria
hawakuchelewa kuwakumbusha wahisani kwamba walikuwa wanaingilia mambo ya ndani
ya nchi. Wahisani hawakuchoka na kelele zao na ndipo hatimaye Profesa Malima
alijiuzulu.
Rais
wetu wa sasa Jakaya kikwete atakuwa na kumbukumbu nzuri sana ya dhahama hiyo
kwani yeye ndiye alimrithi Malima katika nafasi ya waziri wa fedha. Kwa hiyo
kelele za sasa za wahisani ni ishara kubwa kwake kwamba mambo si shwari tena
lazima afanye njia ya kuisafisha serikali yake.
Tayari
wawakilishi watatu wamekwisha iomba serikali kutoa tamko kuhusiana na tuhuma za
ufisadi. Kwa upande wake pia serikali imetoa ahadi ya kufuatilia tuhuma hizo na
kwamba kama itathibitika kwamba tuhuma hizo zina ukweli basi hatua madhubuti
zitachukuliwa dhidi ya wahusika wote.
Tayari
msemaji wa umoja wa nchi za Jumuia ya Ulaya (EU) ameiomba serikali kutoa tamko,
mwingine aliyetoa tamko la namna ile ni balozi wa Marekani nchini Mark Green
pia mwakilishi wa wahisani David Stanton wote hao wameishauri serikali
kujitakasa mbele ya umma.
Ukiachana
na hao bado kuna kelele za vyombo vya habari, na viongozi wengine wa kijamii
kama vile Mkurugenzi wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Joseph Butiku na viongozi wa
dini kama vile kiongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri nchini Tanzania
Askofu Alex Malasusa naye ameiomba serikali kufuatilia na kutoa taarifa za
uhakika kulingana na tuhuma zinazoelekezwa kwa baadhi ya viongozi wake.
Pamoja
na tamko la Waziri Membe bado nchi wahisani zitaendelea kuwa na dukuduku juu ya
tuhuma hususani hizi zilizotolewa hivi karibuni na Dkt. Wilbroad Slaa Mbunge wa
Karatu, tuhuma zinazohusu ujenzi wa majengo pacha ya Benki Kuu, na tuhuma
kadhaaa kuhusiana na mikataba tata ukiwamo ule wa Buzwagi ambao ulishupaliwa
sana na mbunge Zitto Kabwe kutoka chama cha upinzani (CHADEMA).
Ni
imani yangu kwamba wapo wengi watakao niunga mkono kwamba wahisani au hata kwa
jina lolote tutakaloamua kuwaita yaani wafadhili au washirika katika maendeleo
wana haki ya kufuatilia matumizi ya misaada yao ambayo hutokana na walipa kodi
wao katika nchi husika. Ni dhahiri kwamba wahisani hufarijika pale wanapoona
misaada yao imetumiwa vizuri kwa malengo yaliyokusudiwa na wala si vinginevyo.
Kwa
mfano tarehe 15 Januari mwaka huu serikali ya Uingereza ilitangaza azma yake ya
kuipatia Tanzania Pauni za Uingereza milioni 105 (sawa na shilingi bilioni 262)
ikiwa ni mchango wake kwa bajeti ya serikali ya Tanzania mwaka wa fedha 2007/8.
Kwa
maana hiyo baada ya kuwa wametimiza ahadi hiyo hatua inayofuata ni kuangalia
kama kweli pesa hizo zimetumika kwa mambo yenye tija kwa wananchi wote badala ya
kuwanufaisha wajanja wachache.
Wahisani
ni watu ambao wanatakiwa wasikilizwe pale wanapotoa ushauri ili waweze kuendelea
kutuunga mkono na hasa katika maeneo ambayo yanaelekea kusahaulika kama vile
kilimo ambacho ndio uti wa mgongo wa uchumi wa taifa letu.Kama tungeendelea
kuwatumia vizuri wahisani leo tungekuwa tunafikiria masuala ya kupata matrekta
kwa ajili ya kuyapeleka vijijin na pembejeo nyingine ili kuendeleza kilimo.
Kinyume
chake serikali yetu imejiingiza katika mfumo wa kuagiza vitu vya kifahari kama
magari aina ya mashangingi na kutokana na kushindwa kuinua kilimo ndiyo maana
tunaona vijana wote sasa wanakimbilia mijini kwa sababu huko vijijini hakuna
mvuto kumesahaulika kabisa.Vijana wanayo haki ya kukikimbia kilimo kilichopitwa
na wakati kwa sababu kilimo cha jembe la mkono hakijajengewa mazingira mazuri
na hicho ndicho chanzo kingine cha kuongezeka kwa uovu katika jamii kama vile
biashara haramu ya ukahaba na unyan’ganyi.
Ni
sera mbovu au sera ambazo zinabakia katika nadharia bila utekelezaji ambazo
zinasababaisha vijana kuyakatia tamaa maisha ya vijijini na kuamua kukimbilia
mijini ambako hata hivyo pia hawakubaliki. Na pia wanakutana na mazingira
magumu zaidi.
Kama
serikali imeshindwa kuviendeleza vijiji basi inastahili kuzitumia pesa za wafadhili
katika kutoa mikopo kwa vijana waliopo mijini ili wawe wajasiriamali na
kuhalalisha maisha yao badala ya kubakia wakifukuzana na askari mgambo mjini
wakiwazuia kufanya biashara zao za umachinga.
Ni
dhahiri serikali inapoomba misaada nje hutaja maeneo mbalimbali ikiwemo
kuwasaidia akina mama, vijana na, makundi mengine katika jamii lakini inapofika
katika utekelezaji hapo ndipo penye tatizo.Kwa mfano hali ingekuwaje kama vijana
wote waliomaliza kidato cha nne au hata darasa la saba wangepatiwa elimu ya
ufundi stadi na baadaye wakawezeshwa kujiajiri? Ni dhahiri tatizo la wamachinga
lingekuwa limepata ufumbuzi wa kudumu.
Nashangazwa
na kauli kali ya serikali kama vile ombi la wahisani dhidi ya serikali ni sawa
na ujasusi (espionage) kumbe viongozi wetu wanapenda kusifiwa tu na kupambwa
lakini hawataki kabisa kukosolewa au hata kuambiwa ukweli?Tatizo letu ni kule
kujisahau kwamba tuna uchumi tegemezi kwa hiyo wahisani wanahaki ya kufuatilia
misaada yao ili kuhakikisha kwamba imetumiwa kikamilifu kama ilivyokusudiwa.
Lakini
kwa upande mwingine tusisahau pia kwamba wahisani haohao wanazo taarifa nyingi
zinazotuhusu kwa sababu katika dunia ya utandawazi tuliyonayo mataifa ya dunia
ya tatu kama Tanzania ndiyo yanaathirika zaidi kwamba hayana tena uwezo wa kudhibiti
taarifa zao hata zile amabazo yanaziona kwamba ni nyeti.
Ninachomaanisha
hapa ni kwamba tusije tukadhani kwamba nchi wahisani wamezipata taarifa za ufisadi
kutoka magazetini tu bali magazeti yetu yamekuwa nikichocheo tu cha wao kutamka
kwamba wanaona ni jambao jema serikali ikajitakasa ili kurudisha imani ya
wananchi na wadau wengine.
Kwa
mujibu wa katiba ya nchi yetu Ibara ya 18 inawapa ruhusa Watanzania kutoa maoni
yao na kujieleza bila ya vipingamizi ili mradi hawavunji sheria. Pamoja na hayo
sheria ya magazeti ya mwaka 1976 inaziruhusu mamlaka husika ikiwa ni pamoja na
rais wa nchi kuzuia uchapishaji wa magazeti au machapisho ambayo yanakwenda
kinyume na maslahi ya taifa.
Mpaka
sasa hakuna yeyote kati ya waliotuhumiwa kwa ufisadi ambaye ameishachukua hatua
za kisheria kama vile kuwashitaki waliomtuhumu au hata magazeti yanayochapisha
tuhuma hizo. Hali hiyo inaashiria kwamba tuhuma zilizotolewa dhidi ya wahusika
inawezekana zikawa na ukweli na ndiyo maana wanasita kuchukua hatua dhidi ya
waliowatuhumu.kwani wanahofu ya kuumbuliwa mahakamani.
Ukiachana
na suala la vyombo vya habari ni vyema tufahamu pia kwamba wahisani wanafahamu
fika matatizo ya nchi za dunia ya tatu kama Tanzania kwani wengine tayari huwa
wameyasomea katika vyuo nchini mwao kabla ya kuja kufanya kazi barani Afrika.
Wakati
mwingine wanao uzoefu kutoka katika nchi nyingine kwani si kwamba Tanzania
ndiyo nchi ya kwanza kuitumikia barani Afrika bali mara nyingi wengi huwa
wameishazunguka katika nchi kadhaa barani humu hivyo wanao uzoefu wa kutosha
juu ya uendeshaji wa mambo katika nchi zetu.
Kwa
hakika wahisani hawawezi kupiga kelele kama wanaona serikali inajitahidi kujenga
miundo mbinu bora kama ilvyokusudiwa wakati wa kuomba misaada yetu.hawawezi
kupiga kelele kama wanaona nchi yetu inajenga hospitali shule na inawajibika
katika kuendeleza taasisi za kimaendeleo.
Lakini
wahisani wanakerwa wanapoona misururu mikubwa ya viongozi wetu katika ziara
zao, au wanapoona tuna matumizi makubwa kuliko uwezo wetu kiuchumi kwa mfano
ununuzi wa magari ya kifahari ya serikali, au pale wanaposhuhudia viongozi wetu
wanashiriki katika kugombea raslimali za taifa kama vile ununuzi wa nyumba za
serikali umiliki wa migodi na ardhi kubwa bila kuangalia uhalisia wa mambo
nchini.
Wahisani
wanafahamu fika kwamba viongozi wetu wamewekeza mitaji yao kwa wafanya biashara
wakubwa, pia wanafahamu kwamba baadhi ya miradi inayoanzishwa na serikali haina
tija kwa watu wa kawaida isipokuwa inaanzishwa kwa malengo ya kuwanufaisha
wajanja wachache wenye nafasi kubwa kiuchumi.
Wahisani
wanafahamu kwamba kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi hapa nchini kumechangia
katika kuleta matabaka, kwani uchumi wa soko huria umewapa uhalali wenye nacho
kuumilik uchumi, na kupandisha bei za bidhaa mbalimbali bila kuwakumbuka wanyonge.
Ni
ukweli usiopingika kwamba mabadiliko ya kiuchumi ambayo yametoa mwanya kwa
wawekezaji kutoka nje kuwekeza vitega uchumi vyao nchini Tanzania na hivyo
kuweza kuingia ubia na wawekezaji kutoka nje katika biashara mbalimbali kama
vile sekta ya utalii, mahoteli, makampuni ya simu za mikononi n.k.yametoa
uhalali kwa wachache walionacho na kuwabagua wanyonge.
Ni
jambo la kusikitisha kwamba viongozi wetu hujenga mazingira mazuri ya kuwalinda
wawekekezaji na miradi yao kwa sababu wao pia ni wabia katika makampuni hayo ambayo
kimsingi baadhi ya makampuni hayo hayatoi mchango wa maana nchini mwetu bali
yanachangia katika kuhamisha raslimali fedha (cash outflow).
Ni
nadharia hii inayowavuta baadhi ya matajiri katika siasa za Tanzania kwa sababu
hali haikuwa hivyo enzi za utawala wa Mwalimu Nyerere. Kwa lugha nyingine kwa
sasa kwa tajiri kuwa mwanasiasa ni njia mojawapo ya kulinda mali zake.
Haishangazi kwamba baadhi ya makampuni yanayohusishwa na wanasiasa wetu
huanguka ghafla pale wanapostaafu au kupoteza nyadhifa zao serikalini.
Leo
mashindano makubwa yapo katika kujipenyeza katika himaya ya kisiasa (hegemony),
kwani mara baada ya kupata nafasi hiyo, inakuwa rahisi zaidi kufanikisha
upatiakanaji wa leseni za biashara, mikataba yenye utatata na ujumbe katika
bodi za mashirika mbalimbali na taasisi za umma.
Ujanja
unaotumika ni uhalalishaji wa utawala kwa njia ya kuwashirikisha baadhi ya wananchi
wa kawaida, kwa mfano wafanyakazi, wakulima n.k. ili kulinda maslahi yao
yaliyofichika, kwa mfano baadhi ya wahadhiri wa vyuo vikuu leo wanagombea ujumbe
wa halmashauri kuu ya chama tawala lakini watu hao hao wamo katika bodi nyingi
na tume mbalimbali.
Siasa
za leo siyo sawa na zile za zamani zilizotokana na dhamira ya dhati ya utumishi
bali siasa za leo zimekuwa ni biashara, ni mtaji, ni njia nyepesi ya kujitajirisha
kwa wachache na kuwabagua walio wengi na hasa wale wanaojaribu kuipinga mifumo
tawala.hali siyo tofauti hapa Tanzania
Katika
mchanganuo wa tathmini ya maendeleo wa USAID nchini Tanzania, mwaka 2005-2014
(2004), taarifa inasema mabadiliko yaliyoanzisha mfumo wa vyama vingi mwaka
1992, yameleta mabadiliko madogo kimuundo ambayo hata vile yamejenga mazingira
ya kisiasa na kisheria kwa manufaa ya chama kilichopo madarakani hususani katika
kuendeleza umiliki wa uchumi.
Hali
ya sasa imeigeuza siasa kuwa biashara sawa na biashara nyinginezo. Wanasiasa ni
watu wenye nguvu, utajiri, na wanao uwezo wa kujipatia mahitaji ya lazima kwa
njia nyepesi zaidi kuliko mtu mwingine yeyote yule.Taarifa ya UNDP kuhusiana na
maendeleo mwaka 2005 zinaonyesha kwamba Tanzania bado haijachukua hatua
madhubuti dhidi ya ufisadi licha ya kutoa taarifa mbalimbali kwamba imo mbioni
kufanya hivyo.
Taarifa
hiyo inasema Tanzania imebahatika kuwa na amani na utulivu ambao ni kivutio kikubwa
kwa wawekezaji lakini kikwazo kikubwa ni rushwa ambayo imechangia kuteremka kwa
thamani ya pesa yetu mara kwa mara na hivyo wawekezaji wanahofu ya kupata
hasara iwapo watawekeza katika mazingira yasiyo na uhakika wa faida kwa miradi
yao
Kwa
upande mwingine taarifa hiyo inaonyesha udhaifu mkubwa wa vyombo vya dola
katika kutimiza wajibu wao, hofu hiyo inatokana na uwezo mdogo wa wataalamu au
uhaba wao, japo wanao uwezo na taaluma za kuosha. Ni katika mazingira hayo
ndipo watafiti wanahisi kwamba rushwa inatumika katika kuzima utendaji wa baadhi
ya vyombo vya dola.
Kwa
mfano mahakama zetu zinonyesha kwamba zimezidiwa na mzigo wa kesi
zisizosikilizwa na wakati mwingine rushwa inachangia katika utendaji duni wa
mahakama zetu. Kwa upande mwingine taarifa hiyo inaonyesha kwamba hadi mwezi
Juni 2004, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ilikuwa imepokea taarifa10,319
za tuhuma mbali mbali za rushwa lakini ni kesi 357 tu ndizo zilikuwa
zimesikilizwa na zote hizo zilizosikilizwa zilikuwa zinawahusu watu wa kada ya
chini katika utumishi wa umma.
Inakuwaje
kila siku kuna tuhuma zinazowahusu viongozi wakubwa wa kisiasa lakini
hawachukuliwi hatua? Jibu ni dhahiri kwamba siasa imekuwa kitega uchumi wanasiasa
ni matajiri wasioguswa. Hata katika harakati za kugombea uongozi si kwamba
wananchi ndiyo wanowatuma wanasiasa wawakilishe, bali wanasiasa wanatumia pesa
zao kuwashawishi wananchi wawapigie kura, ili wawahalalishe katika madaraka,
uwezo huo wanaupata kwa sababu ya pesa zao na lugha tamu wanazotumia wakati wa
kutafuta uongozi.
Ni
mazingira hayo ambayo yametujengea siasa za upambe, baadhi ya wajanja ambao
wamefanikiwa kujipenyeza ndani ya mfumo wanajifanya wanakipenda chama tawala
lakini ukweli wa mambo ni kwamba tukiwachunguza kwa undani baadhi yao hawana hata
chembe ya itikadi ya chama alichokiasisi Mwalimu Nyerere bali wana itikadi ya
kujitafutia chao tena mahali popote penye urahisi wa kufanya hivyo. Kwa hiyo
kwa sasa wamo ndani ya CCM kwa sababu hiyo tu (opportunists).
Katika
kitabu chao ‘Africa Works’ (1999), waandishi Patrick Chabal na Jean- Paschal
Daloz wanajenga hoja kwamba siasa za utajirisho ndizo zimechangia katika kuwapo
kwa madikteta barani Afrika kama vile Hayati Bokassa wa Jamhuri ya Afrika ya
Kati ambaye aliugeuza uteuzi wa uongozi kuwa mradi wa kuwanufaisha ndugu na
rafiki zake wa karibu na hivyo ndiyo maana alikaa madarakani kwa muda mrefu kwa
sababu wanufaika walimlinda.
Waandishi
hao pia wanazungumzia tabia ya baadhi ya wanasiasa kuzigeuza taasisi za umma
kama vile ni mali zao binfisi. Katika hilo wanamzungumzia Frederick Chiluba
ambaye wakati wa utawala wake alimfukuza kazi mkurugenzi wa wa televisheni ya
taifa baada ya mkurugenzi huyo kulalamika kwamba televishenu hiyo ilikuwa
inatumia muda mrefu kwa kutangaza vipindi vya ‘walokole’ madhehebu ambayo
Chiluba ni mfuasi wake.
Nakubaliana
kwa kiwango kikubwa kwamba uanzishaji wa asasi za kiraia wakati mwingine
umekuwa hauwalengi watu wa kawaida bali wanufaika ni watu wa mijini ambao asasi hizo ndiko zimejikita zaidi huku
viongozi wake wakiwa na kila aina ya ukwasi, magari mazuri, malipo kutoka kwa
wahisani n.k.
Ujanja
ujanja ndiyo imekuwa uendeshaji wa mambo katika nchi zetu kwani hata viongozi
wetu hawataki kuachia madaraka. Kuna ukweli usiopingika kwamba kipo kizazi
kinaelekea kurukwa kutokana na baadhi ya viongozi kung’ang’ania madaraka
matokeo yake ni kwamba wasomi wetu wameamua kutafuta mbinu nyingine za kufaidi
‘matunda ya uhuru’.
Upo
utani kwamba kizazi hicho ng’ang’anizi (rigid), kimekula matunda, majani na
sasa kinamalizia kula mizizi ya uhuru na hivyo kuna hatari ya vizazi vijavyo
kukosa urithi kutokana na kila raslimali zetu kuhamishwa na wenye mamlaka kwa
sasa.
Tusipozingatia
angalisho au tahadhari tunazopewa na wataalamu wetu, wahisani, viongozi wa dini
tunataka tumsikilize nani? Vinginevyo tunataka tuache matabaka yakomeae na
baadaye tuingie katika machafuko kama yale ya Sierra Leone, Liberia, au DRC
ambapo katika machafuko hayo baadhi wanasiasa wanajinufaisha kwa kuendeleza
biashara haramu kama vile kuiba madini, kuuza silaha kwa njia za magendo,
uvushaji wa madawa ya kulevya hali ambayo imewaathiri kwa kiwango kikubwa
wanyonge wasio na hatia.
Bila
kuwakemea viongozi wetu wanaweza kujisashau na kudhani kwamba wao ndio pekee
wenye hatimiliki ya majimbo au himaya zao za kisiasa. Kwa lugha nyingine
viongozi wetu wanaweza kujenga ukuta kati ya wananchi na wahisani ili wananchi
wasifahamu serikali inapokea kiasi gani cha msaada kutoka nje lengo likiwa ni
kujitafutia sifa kwamba wanatimiza wajibu wao wakati hali halisi ni tofauti.
Ni
katika mazingira ya kujisahau ndipo viongozi kama vile Felix Houphet Boigny wa
Ivory Coast aliweza kujenga kanisa mfano wa Basilica la mjini Rome nchini
Italia.
Kwa
upande mwingine Mobutu Seseko yeye alijenga uwanja wa ndege ambao unaiwezesha
ndege aina ya Concorde kutua kijijini kwake.Yote hayo ni matatizo ya kulewa
madaraka kutokana na kukosa nguvu kubwa ya ukosoaji. Kwa hiyo ukemeaji,
ukosoaji na mambo ya aina hiyo yanastahili kuangaliwa katika mtazamo chanya
badala ya kuonekana kwamba viongozi waliopo wanaonewa wivu au wanabughudhiwa na
watu wasiohusika.
Mwandishi
wa makala haya anapatikana kwa simu 0754 826 272, na barua pepe mhegeraelias@yahoo.com

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni