Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU)
JE NI
MFUPA ULIOMSHINDA FISI? (SERIKALI)
Septemba
22, 2007 Mtanzania Jumapili
Na Elias Mhegera
Hivi karibuni Chama Cha Mapinduzi CCM,
kiliendesha zoezi la chaguzi mbalimbali za ndani, katika zoezi ambalo baadhi ya
viongozi na wagombea walituhumiwa kwa kutoa hongo na hivyo kuvunja imani za
wanachama waadilifu.
Makala hii inachambua tatizo la rushwa katika
ujumla wake kama tatizo la kijamii na ambavyo linagusa nyanja nyingi za maisha,
na athari zake za muda mrefu.
Miaka kadhaa nyuma na hasa katika kipindi cha
uongozi wa Mwalimu Nyerere siasa za Tanzania hazikuwavutia sana matajiri wakubwa,
kwa kusema hivyo sina maana kwamba ni kosa kwa tajiri kuwa mwanasiasa.
Ninachokusudia kusema ni kwamba siasa za leo
zimetawaliwa sana na mambo ya pesa na hivyo zinawakwaza watu wasiokuwa na uwezo
mkubwa kipesa.
Tatizo ni kwamba kutokana na baadhi ya watu
wasio waadilifu kupenda kujiingiza katika siasa sasa baadhi ya wanajamii
wameamua kujinufaisha kwa kudai hongo nyakati za chaguzi bila kujali athari za
muda mrefu za mtindo huu.
Kimsingi ni kwamba tunapokuwa na wanasiasa wengi
waliotumia rushwa katika uchaguzi tunajenga mazingira magumu ya kuondokana na
rushwa katika utawala wa wanasiasa hao.
Rushwa ikitawala katika jamii madhara yake ni
kwamba itaibuka jamii isiyo na usawa, ufisadi unaweza kuchochea hata vita vya
wenyewe kwa wenyewe kama ilivyokuwa kwa nchi za Burundi, Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo na Rwanda.
Mara nyingi matatizo ya aina hiyo hupikwa kwa muda
mrefu kabla hayajalipuka na kusababaisha madhara makubwa.
Uadilifu katika uongozi unapopotea ndipo watu
mbalimbali hujaribu kuitumia siasa kama kitega uchumi lengo likiwa ni kupata
madaraka ili kujichumia mali ya umma.
Kwa maana hiyo maadili yote yahusuyo uongozi huwekwa
kando, lengo la viongozi hubadilika kutoka kwenye kuwatumikia watu na kuwa kujinufaisha
kwanza mtu binafsi na ndipo uongozi unapogombaniwa kwa mbinu zote ikiwamo
rushwa.
Hali inakuwa mbaya zaidi kwenye nchi zenye
demokrasia changa kama Tanzania kwani siasa za ushindani wa vyama zinatazamwa
katika misingi ya uadui badala ya watu kuona kwamba ushindani ni sehemu ya
mchezo wa siasa.
Mwaka 1992 serikali ya Tanzania iliruhusu rasmi
kurejeshwa kwa mfumo wa siasa za vyama vingi na kwa mara ya kwanza uchaguzi
uliofuatia wa mwaka 1995, ukavihusisha vyama vingi.
Kwa bahati mbaya tokea wakati huo vyama vya
upinzani vinazidi kudorora na hivyo chama tawala kimekosa mkosoaji wa dhati.
Hali hiyo pia imeendana na lindi la wapinzani
maarufu kurejea katika chama tawala, CCM. Kwa mifano michache ni Dkt. Masumbuko
Lamwai aliyekuwa tishio kipindi alipokuwa katika chama cha upinzani cha
NCCR-Mageuzi, leo hasikiki tena wengine ni Richard Hiza Tambwe, Dkt Festus
Limbu, Dkt Walid Kaborou, n.k.
Wote hao wamerejea katika CCM ambako wanaendelea
kupwaya wakati huo huo wakiiacha kambi ya upinzani ikiwa hoi bin taabani.
Uamuzi wa mtu kurejea katika chama tawala ni wa
mtu binafsi bila kujali kama ameshawishiwa na mtu kufanya hivyo lakini jambo
lenye manufaa zaidi ni kuangalia nini hatma ya siasa za Tanzania kama kila
mwenye nguvu atamezwa ndani ya CCM (co-optation).
Ni kwamba kwa hali yoyote ile chama tawala
kinahitaji mkosoaji ili kiweze kufanya kazi zake kwa uwazi na umakini zaidi.
Kazi hiyo inatakiwa ifanywe na vyama vya upinzani, asasi za kiraia, vyombo vya
habari, taasisi za elimu ya juu, madhehebu mbalimbali ya dini, na wachambuzi wa
masula ya kisiasa, kiuchumi na kijamii ndani na nje ya nchi.
Ndiyo maana kabla ya kuangalia rushwa katika
jamii inabidi tuangalie kwanza rushwa inavyotumika katika uchaguzi kwani hapo
inawagusa watunga sheria za nchi kama vile wabunge na wawakilishi wengine.
Makundi ya wawakilishi ndiyo yanawagusa watanzania
wote katika ujumla wao na ndipo inabidi tujiulize maswali kama tutakuwa na
viongozi watoaji au wapokeaji wa rushwa watawezaje kutetea maslahi ya wengi
katika nchi?
Siku moja nilibahatika kutoa mada kwa wanafunzi
wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, mada yenyewe ilihusiana na maendeleo ya
kisiasa tokea kupatikana kwa uhuru hadi awamu ya tatu ya Rais Mstaafu Benjamini
Mkapa.
Nilizungumza mengi katika mada ile lakini
sikuona kama inapokelewa kwa msisimko niliotarajia. Hata hivyo baada ya mada
yangu kulikuwa na mapumziko mafupi na ndipo nilipoona wasikilizaji wangu
wakinifuata mmoja baada ya mwingine kwa hakika kila mmoja alitaka kuondoa
dukuduku lake kuhusiana na kile nilichokisema ukumbini.
Kwa hakika wengi walikubaliana na maudhui ya
mada yangu lakini walishindwa kuchangia kutokana na migongano ya kimaslahi.
Japo mimi niliamini kwamba mwanachuo wa chuo
kikuu chochote nchini anaweza kuwa mchambuzi makini wa masuala yanayoihusu
jamii yake lakini kwa upande wa chuo hicho jambo hilo linakuwa gumu kwani
takribani watu wote wanakuwa katika ajira za serikali au wanakuwa ni wafanyabiashara
binafsi.
Mambo yote hayo yanawatia woga wasomi hao
kuchangia hoja yoyote ya kitaaluma au hata kuwa na hofu ya kuhatarisha ajira
zao serikalini.
Ni imani yangu kwamba hali kama hiyo haiwezi
kujitokeza katika vyuo vyenye wanafunzi wanaotokea shuleni moja kwa moja (direct
entrants), kwa hiyo woga wa wasomi huo una jambo la msingi ndani yake.
Lakini ukweli ni kwamba wahusika walinifuata nje
ya ukumbi na kila moja akaunga mkono mada yangu ni jambo lililonipa faraja
kwamba ujumbe wangu uliwafikia walengwa.
Kwa maana
hiyo tunaweza kusema wapo watanzania wengi wanaoichukia rushwa katika sura zake
zote lakini bado hawajajengewa mazingira mazuri ya kuikemea hadharani
Kwa hiyo jambo lililodhahiri ni kwamba tunakosa
ujasiri japo tunaichukia rushwa mahali popote inapotumika kwani inatunyima haki
zetu za kimsingi iwe ni mahakamani au katika jeshi la polisi. Kwa hiyo makala
hii italenga katika kutoa ushawishi wa kujenga ujasiri wa kuikemea rushwa
mahali popote ilipo.
Ni lazima tukubaliane kwamba siku zote maisha
yetu yamegawanyika katika sehemu kuu mbili: ushujaa (heroism) na uovu
(villainy). Kwa hakika ni lazima wawepo mashujaa wanaokemea uovu ili jamii
iweze kwenda katika mstari ulionyooka na katika dira inayostahili.
Kwa bahati mbaya ushujaa ninaouzungumzia hapa
huwagharimu sana wale wanaojaribu kukemea, Kwani wote hao huonekana kana kwamba
ni wanafiki, mabaradhuri na hivyo hutengwa na jamii zao mara moja.
Lakini kwa upande mwingine ni dhahiri kwamba
yeyote yule aliyeamua kupingana na uovu basi ni lazima ajiandae kwa adhabu
inayotokana na azma yake hiyo.
Siku zote watu ambao wanajaribu kuirudisha jamii
katika dira sahihi huonekana kwamba wemekanganyikiwa (social rejects).Hii
inatokana na ukweli kwamba watu wa namna hii huonekana kwa wenzao kama kero kutokana
na azma yao ya kuwaondolea raha waliyoizoea.
Ndiyo maana nimekuwa nikisisitiza kwamba katika
azma ya kuondoa ufisadi na uovu mwingineo katika jamii inabidi viongozi wa dini
wahusike kikamilifu Kwani imani ya dini inaweza kupunguza kwa kiwango kikubwa
madhara yatokanayo na ufisadi kama si kuyaondoa kabisa.
Kwa mfano katika imani za kikristu tunaamini
kwamba Bwana Yesu Kristu aliibadilisha alama ya msalaba kutoka kwenye alama ya
kuulia wahalifu na kuigeuza kuwa alama ya ushindi ndiyo maana wakristu
hupendela kuvaa misalaba kuashiria ushindi huo.
Leo watu wengi wanavaa ishara hiyo ya ushindi ya
msalaba wakiwa wamesahau kwamba ushindi huo uliambatana na kumwagika kwa damu
ya Bwana Yesu Kristu. Hivyo basi ni muhimu kufahamu kwamba ushindi wa muda
mrefu wa jambo lolote uanahitaji kujitoa mhanga.
Kwa hiyo wale wote wanaopigania kuondoa ufisadi
katika jamii na kuyatetea maadili mema katika jamii kwa ujumla wawe tayari
kusutwa, kuzongwa zongwa.misukosuko ya kila aina na wakati mwingine hata kuuawa
lakini mara yanapojitokeza hayo iwe ni faraja kwamba ujumbe wetu umewafikia
walengwa.
Kwa mfano mbunge aliyeshinda kwa kutoa hongo
anakuwa amejijengea mazingira mazuri ya yeye mwenyewe kupokea hongo kwani tayari
anakuwa amekiuka maadili na kujijengea mazingira mabaya kiroho. Mbunge huyo
anaweza akapewa hongo ili aipitishe bajeti fisadi kwa asilimia mia moja.
Ukweli wa jambo hilo ni kwamba ni lazima mtu
yeyote ajuilize ni kwa nini amuhonge mtu anayetaka kumtumikia vinginevyo huyo
mgombea ndiye anastahili kupewa zawadi na wanajamii kwa kuamua kuwatumikia.
Labda wapo wanaoweza kujiuliza maswali mengi
kwamba bajeti fisadi ni ipi hiyo? Katika kujibu hilo mwandishi Jorge
Martinez-Vazguez katika chapicho lake Corruption,
Fiscal Policy, and Fiscal Management
anasema miaka kadhaa nyuma wataalamu mbalimbali walikwepa kuizungumzia rushwa
na ufisadi kwa sababu waliona ni mfumo wa kawaida (inherent) uliomo katika
mifumo yote ya kisiasa.
Lakini siku hizi hali imebadilika kwa sababu wachambuzi
wa masuala ya kisiasa na kijamii wamegundua kwamba rushwa ndiyo kikwazo cha
maendeleo popote ulimwenguni na ndiyo maana wanapigania kwa nguvu zote kuwa na
utawala bora ambao utaondokana na ufisadi kwanza ndipo mambo mengine yafuate.
Maelezo wanayotoa ni kwamba kunapokuwa na
ufisadi utendaji unakuwa legelege kwa mfano waziri atajihusisha na mikataba
hewa, wabunge watashindwa kumkosoa, polisi watashindwa kumkamata, na hata
wakimkamata atatoa hongo na kushinda mahakamani kwa hiyo mzunguko huo wa uovu
ndiyo chanzo cha ulegelege wa serikali.
Athari za muda mrefu za mzunguko huo wa uovu ni
kuwavunja moyo wafadhili kwa sababu hawaoni manufaa ya kuendelea kuzifadhili
serikali zetu baada ya kujua kwamba misaada haiwafikii walengwa (walalahoi)
bali wajanja wachache.
Na kwa bahati mbaya hali inapofikia hapo kila chombo
kinakuwa kimeathirika vikiwemo vyombo vya habari, asasi za kiraia na hata
wasomi ambao humezwa katika mfumo huo fisadi. Kwa hiyo katika mazingira ya aina
hii, si jambo la ajabu kuona kwamba Bunge linapitisha bajeti fisadi.
Ni kwamba viongozi wakuu wa nchi wakianza
kujihusisha na ufisadi basi hata taakwimu mbalimbali zinaweza kupikwa ili
kukidhi matakwa yao. Katika mazingira ya aina hiyo maadili katika jamii hushuka
kwa kiwangio kikubwa watu huanza kuhama ovyo kutafuta namna ya kujikimu.
Katika uhamaji huo usioratibiwa uhalifu wa kila
aina unaweza kujitokeza kwa mfano: ugaidi, matumizi ya madawa ya kulevya na
hata ongozeko la ugonjwa hatari wa UKIMWI.
Katika mantiki hiyo ni lazima tufahamu kwamba
kabla ya kuanzisha vita dhidi ya ufisadi ni lazima kwanza tuwaelimishe watu
wetu kwamba tunastahili kuichukia rushwa badala ya kuikumbatia, tuwaelimishe
wafanyakazi kwamba mishahara yao ni midogo kwa sababu watu wanakwepa kulipa
kodi zinazostahili.
Ni lazima tuwafahamishe watu kwamba rushwa ndiyo
inakwamisha maendeleo yao, kwamba kila mmoja anatakiwa atoe mchango wake katika
kupambana na rushwa. Kwamba jukumu la serikali ni kusimamia au kuratibu zoezi
la kupambana na rushwa lakini ni jukumu la kila mwananchi kuisadia serikali
katika mapambano hayo.
Vita dhidi ya rushwa ni vita vitakatifu kwa hiyo
kila mmoja anastahili kuchangia kwa uwezo wake wote kwa sababu ufumbuzi
ukipatikana utawanufaisha wote pia.
Kwa hiyo ndiyo maana wananchi wanatakiwa kuitaja
mianya yote ya rushwa kwa sababu wanaifahamu, wao ndiyo wanaotakiwa kupigania
nidhamu ya matumizi ya pesa za halmashauri zao na raslimali zingine za umma.
Kama kila mwananchi atatoa mchango wake katika
hilo basi tutakuwa tumeirahisiha kazi ya Taasisi ya kuzuia na Kupambana na
Rushwa (TAKUKURU). Kwa ujumla jukumu lao ni uendeshaji (co-ordination) wa shughuli
zote zinazoelekezwa katika kupambana na rushwa, lakini wao pekee hawana uwezo
wa kuiangamiza rushwa.
Mambo yote hayo yanawezekana iwapo
tutajiaminisha kwamba maana ya utumishi wa umma ni kuhudumia watu bila ya
kuwabagua, wala kutegemea vipato haramu.Watumishi hao ni lazima wafahamishwe
kwamba wao ni watoa huduma na wala si wafanya biashara.
Mkakati mzima wa kuondoa rushwa ni lazima uziainishe
kwanza aina zote za rushwa yaani kubwa na ndogo. Kwa mfano mawaziri na
wakurugenzi wa makampuni makubwa ya umma wanajinufaisha kutokana na mikataba
minono inayosainiwa na serikali au makampuni yao hata kama hawapati malipo ya
pesa moja kwa moja.
Hali hiyo ikiachwa ikaendelea kushamiri huleta
matabaka makubwa katika jamii ambapo wale wasionufaika na uchumi au mikataba
inayosainiwa hukata tamaa na kuanza kuhujumu uchumi katika azma ya kujikimu.
Kwa mfano askari polisi trafiki anajenga nyumba
kubwa, anaendesha gari zuri, anaishi kifahari lakini mwalimu na daktari hawawezi
kujenga wala kujikimu katika maisha yao ya kila siku ndipo hujitokeza walimu
wakafelisha wanafunzi kwa sababu muda mwingi huutumia kutafuta vipindi vya
ziada nje ya ofisi zao.
Tukichukulia mifano halisi katika nchi za Kenya
na Tanzania tunaona kwamba rushwa imekuwa ikiathiri utendaji wa serikali hizo
katika maeneo mengi.
Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na taasisi
iitwayo The African Centre for Economic
Growth ikihusianisha rushwa na umaskini nchini Kenya kwa mwaka 2000,
inaonyesha kwamba rushwa imekuwa kero kubwa nchini humo kwa sababu inawahusisha
wanasiasa wakubwa na hasa mawaziri.
Kwa upande mwingine rushwa imeiathiri kwa
kiwango kikubwa serikali ya Kenya kwa sababu watendaji wengi wamekuwa
wakijichukulia “kidogo dogo” kila mtu kwa wakati wake na nafasi yake.
Jambo hilo limekuwa na athari mbaya kwa sababu
ndilo limechangia kuwepo na mfumuko wa bei na kuanguka kwa taasisi za pesa kama
vile benki na mamlaka za ukusanyaji kodi.
Kwa mujibu wa taasisi hiyo rushwa mbaya zaidi
nchini Kenya ni ile ambayo inahusu tenda hewa, miradi inayofadhiliwa na
serikali, mashirika na wafadhili wengine ambapo pesa hizo huishia mifukoni kwa
wajanja wachache.
Kundi jingine linalotajwa na ripoti hiyo linawahusu
wasomi ambao kutokana na taaluma zao na ukaribu wao na viongozi mbalimbali
serikalini wameweza kujipatia mikataba minono kama vile utoaji wa elimu
mbalimbali katika maeneo ya sheria, teknolojia, mazingira, n.k.
Watu hawa hutafuna mamilioni ya pesa na kuwaacha
walengwa bila chochote chenye manufaa kwao. Kwa upande wa Tanzania ripoti ya Afrobarometer iliyotolewa an REPOA April 2006, inasema rushwa
imejikita katika maeneo mbalimbali na imeathiri kwa kiwango kikubwa maeneo
muhimu ya kiuchumi.
Ripoti hiyo inasema rushwa imeendelea kuwepo
nchini Tanzania kwa sababu bado watu hawajaelimishwa vya kutosha juu ya athari
za rushwa na kwa upande mwingine nchi haijajiweka tayari kwa ajili ya
kuondokana na rushwa hiyo.
Kukosekana kwa uwazi, uwajibikaji na utawala
bora vimechangia kwa kiwango kikubwa katika kuenea kwa rushwa nchini Tanzania.
Kwa maana hiyo rushwa imekuwepo katika maeneo mabalimbali kama vile serikali za
mitaa jeshi la polisi, mamlaka ya kodi, mahakamani, n.k.
NINI BASI
KIFANYIKE?
Rushwa inaweza kusambaratishwa kama itapewa
kipaumbele kwa mfano na makundi yote makuu husika katika jamii kama vile jeshi
la polisi, mamlaka ya mapato (TRA), mahakama,na afya. Pia vyombo vya habari
vinawajibika kutoa elimu kwa umma mzima kwa njia mbalimbali, kama vile
magazeti, redio, televisheni vipeperushi, nyimbo, n.k.
Njia nyingine ni kujenga utawala bora wenye
uwazi na uwajibikaji, kuunga mkono tasisi husika kwa watu kutoa taarifa,
kujituma kwa wafanyakazi bila kujali kupata hongo na kwa upande mwingine
serikali ifuatilie vilio vya wafanyakazi hususani madai yao ya kimsingi.
Kwa kushirikiana kwa taasisi mbalimbali jamii
nzima inaweza kujikuta imeichukia rushwa na kuona ni jambo lisilofaa. Kwa maana
hiyo jamii nzima itawaunga mkono mashujaa wa mapambano (heroes) na kuwakataa
waovu (villains) baada ya hapo sote tutakunywa mvinyo wa kifikra tukishangilia
ushindi dhidi ya RUSHWA.
Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu
0754-826272 au barua pepe: mhegeraelias@yahoo.com

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni