Jumapili, 6 Julai 2014

Jamanii ee, Watanzania sasa wanataka serikali tatu siyo mbili! Tanganyika ni lazima!


Mchungaji Christopher Mtikila ni mmoja wa watu walioipigania Tanganyika kwa muda mrefu na tumuunge mkono na wale wote wanaotaka serikali tatu au uwepo wa Tanganyika ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 

Na Elias Mhegera
19/02/2014
VUTA nikuvute ya Katiba mpya imefika pazuri ambapo ingekuwa ligi ya soka tungesema imefikia ‘patamu’. Hoja hii inatokana na mivutano inayoendelea chini kwa chini kutoka vyama vya siasa na makundi mengine ya kijamii.
Kwa sasa mada zinazoelekea kugusa mijadala zaidi ni muundo wa Serikali ya Muungano, rasilimali za taifa na madaraka ya rais. Wachambuzi wa masuala ya Katiba wametaja kwa nini mada hizo zimepewa umuhimu kuliko nyingine.
Katika warsha ya Februari 13 chini ya maandalizi ya Chama cha Walimu wa Uraia (CETA) na ile iliyofanyika Januari 31, kwa maandalizi ya pamoja ya taasisi tatu za Konrad Adenauer Stiftung (KAS), Jukwaa la Katiba (JUKATA) na Friedrich Ebert Stiftung (FES) ilidhihirisha kwamba muundo wa Serikali ya Muungano ni hoja nzito kupita zote katika mtazamo wa washiriki wengi.
Akifafanua hofu na manufaa ya kuundwa kwa serikali tatu, Profesa Josephat Kanywanyi, ambaye ni mhadhiri wa sheria mstaafu kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam anasema ni wazi muundo wa serikali tatu utauvunja muungano iwapo Watanzania hawatakuwa makini.
“Ni dhahiri iwapo serikali ya Tanganyika itazaliwa na kupata rais mwenye nguvu kuliko wa serikali ya muungano basi hilo linaweza kusababisha kuzaliwa kwa Serikali ya Zanzibar kwa kuzingatia katiba yao ya mwaka 2010,” anaonya msomi huyo.
Profesa Kanywanyi anasema kimsingi ingawa muundo wa serikali tatu ambao umepitishwa na Tume ya Jaji Warioba kwa ajili ya mjadala wa kitaifa bado ni jambo jema lakini upo uwezekano wa kuibuka kwa rais wa serikali ya Tanzania (Bara) mwenye nguvu kuliko hata wa serikali ya Muungano.
Kimsingi msomi huyo hapingani na hoja ya walio wengi kwa sasa ya kutaka serikali ya Tanganyika. Awali wakati wa ufunguzi wa semina hiyo wakurugenzi wa KAS, Stefan Reith na Rolf Paasch wa FES walisema mjadala wa Katiba mpya ni wa Watanzania, kwa manufaa yao.
Naye Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba, Deus Kibamba, anakiri kwamba kwa hali yoyote ile mwelekeo wa kuwapo kwa serikali tatu kutadhoofisha Muungano lakini haoni tatizo kwa hilo iwapo ndiyo chaguo la Watanzania.
Hata hivyo mwenyekiti huyo anaipongeza Tume ya Jaji Warioba kwa kufanya kazi nzuri ingawa awali kulikuwa na kusigana kwa hapa na pale kati ya tume hiyo na asasi za kiraia hususan JUKATA.
Anasema maeneo yatakayoathiriwa na muundo mpya wa Katiba ni umiliki wa maliasili, ardhi, mafuta na serikali za mitaa. Anatetea hoja yake kwamba baadhi ya mambo yemeachwa kwa sababu hayahusu muungano lakini yanaweza kuibuka katika sura mpya.

Naye mshauri mwelekezi wa masuala ya habari, Lawrence Kilimwiko, anasema hajaridhika iwapo Katiba mpya imejikita vya kutosha katika kuzingatia maadili ya viongozi. Pia anauliza sababu za vyama vya siasa kuendelea kuwa suala la muungano.
“Iwapo sasa tunaruhusu mgombea binafsi ni kwa nini suala la vyama linaendelea kuwa la muungano? Je, tunataka kuendelea na tume ya uchaguzi kama ilivyo ambayo imekuwa ikilalamikiwa?” anauliza.
Lakini katika warsha nyingine iliyoandaliwa na taasisi ya KAS kwa ushirikiano na ile ya Tanzania Development Initiative Programme (TADIP) suala la Tanganyika linaonekana kuwa kinara kuliko masuala yote yaliyopata wachangiaji wengi.
Mmoja wa Makamishina wa Tume ya Jaji Warioba, Profesa Mwesiga Baregu, anaainisha kipengele kwa kipengele sababu za yeye na wenzake kufikia muafaka huo.
Lakini Profesa Chris Maina anasema bado kuna mambo yaliyoachwa juu juu. Kwa mfano lugha zinazotumika katika viapo bado hazijaachana moja kwa moja na ile dhana ya utii kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, jambo ambalo wachambuzi wa masuala ya sheria na siasa wanasema lilisababisha kuwapo kwa matumizi mabaya ya madaraka.
Hata hivyo anaawacha wasikilizaji na kauli ya matumaini: “Naomba niweke wazi msimamo wangu kwamba napendelea muundo wa serikali tatu, nina matumaini kwamba kwa mara ya kwanza sasa Watanzania wataachana na katiba za kupandikizwa na kuwa na katiba yao,” anasema Profesa Maina.
Naye Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (CHRAGG), Jaji Mstaafu Amir Manento, anaibua furaha kwa wanaharakati na waandishi ukumbini kwa kusema: “Nipo tayari kunukuliwa popote pale msimamo wangu ni wa serikali tatu!” anasema.
Mjadala mkubwa hapo unajikita katika masuala ya muungano. Muwezeshaji kutoka Kituo cha Sheria na  Haki za Binadamu (LHRC) William Kahale, anatoa mada kwa staili yake ya kupiga kura.
Kura zinapigwa kabla ya mijadala na inaonekana kwamba watu 29 katika ya 57 wanataka serikali tatu lakini baada ya mijadala inaonekana asilimia 95 wanataka serikali tatu, hali inayothibitisha kwamba mijadala ina umuhimu katika kuwajengea wananchi uelewa juu ya masuala ya katiba.
Humphrey Polepole, Kamishina wa Tume ya Jaji Warioba, anasema walichokifanya wao ni kupata maridhiano ya makundi yote badala ya kuangalia masilahi ya vyama na itikadi za makundi yaliyowatuma.
Tuwasiliane: mhegera@gmail.com    simu: 0754-826272



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni