Jumapili, 6 Julai 2014

ZENGWE LA KATIBA MPYA! NANI ATAOKOA MCHAKATO?

Mwenyekiti wa Umoja wa Asasi za Kiraia (AZAKI) Katika Mchakato wa Kupata Katiba Mpya Bw. Irenei Kiria akisoma tamko la AZAKI tarehe 24/4/2014 katika Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC)

Na Elias Mhegera
KUPINGWA kwa mchakato wa katiba mpya unaoendelea mjini Dodoma na makundi mbalimbali ya wanajamii, ni ishara tosha kwamba mtindo wa uendeshaji wa Bunge Maalumu la Katiba (BMK) unaotumika hauwezi kutoa katiba ya wananchi.
Hofu ya kuvurugwa kwa mchakato huo ilianzishwa na Rais Jakaya Kikwete mwenyewe, pale alipolihutubia Bunge hilo mjini Dodoma mnamo tarehe 21 Machi, ambapo kiongozi huyo wa kitaifa alidiriki kuikejeli Tume ya Mabadiliko ya Katiba (TMK) ya Jaji mstaafu Joseph Warioba.
Kejeli ya kazi hiyo na matumizi ya takwimu vikachochea wanachama wa chama chake, yaani Chama Cha Mapinduzi (CCM) kufuata mkumbo na kuanza kurusha makombora dhidi ya Mzee Warioba na timu yake.
Ni kutokana na muendelezo huo unaotaka kuuteka mjadala huo kwa manufaa ya CCM, ndipo makundi mengine ikiwa ni pamoja na wabunge wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) na wanajamii wengine ikiwamo asasi za kiraia, wamepinga kwa namna mbalimbali kutekwa kwa mchakato huo.
Wanafunzi wa vyuo vikuu
Siku chache zilizopita, mtandao wa umoja wa wanafunzi wa vyuo vikuu chini ya mwamvuli wa Tanzanian Students Networking Programme (TSNP) kwa kushirikiana na Shirika la Kijerumani la Konrad Adenauer-Stiftung (KAS) waliandaa mjadala kuhusu nafasi ya vijana katika katiba mpya.

Katika mjadala huo uliofanyika katika hoteli ya Landmark, Ubungo Riverside, sauti nyingi zilionekana kuitetea Tume ya Mabadiliko ya Katiba maarufu kama Tume ya Jaji Warioba pamoja na rasimu yake ya katiba ambayo sasa inaelekea kuwekwa pembeni kutokana na ubabe unaofanywa na CCM dhidi ya wananchi waliotoa maoni yao kupitia tume hiyo.
Akiwakaribisha vijana wenzake zaidi ya 60 katika kongamano hilo, Katibu Mkuu wa TSNP, Alphonce Lusako, alisema kwamba vijana wametengwa sana na utawala uliopo madarakani ikiwa ni pamoja na kutokushirikishwa katika mambo mengi ya kitaifa.
Alisema kwamba vijana wengi wanaohitimu kutoka katika vyuo vikuu hujikuta hawana ajira na hivyo wengine kushawishika kujiunga katika makundi mbalimbali mazuri na mabaya katika kuhaha wakitafuta maisha na mkate wao wa kila siku.
Alisema hali ni mbaya zaidi kwa wale ambao hawajafika katika ngazi ya vyuo vikuu na hao ndio wanaouawa na polisi katika maandamano ya vyama vya upinzani wakiwa katika kutafuta watetezi wa hatima zao.
“Vijana tumeonewa sana, wamachinga wanafukuzwa hapa na pale kila kukicha, vyuo vikuu vinafungwa kila uchao, ufisadi umetamalaki kila mahali nchini, ni lazima tupiganie katiba mpya itakayolinda maslahi yetu,” aliwahamasisha wenzake.
Naye Mkuu wa Utawala wa KAS, Richard Shaba, alisema kwamba taasisi yake ililetwa na Mwalimu Julius Nyerere Baba wa Taifa la Tanzania ili kuanzisha Chuo cha Itikadi Kivukoni, ambacho kiliwaandaa viongozi bora wa nchi hii ambao alidai kwa sasa wamebakia wachache sana.
Humphrey Polepole afichua siri nzito
Aliyekuwa mmoja wa makamishna wa TMK, Humphrey Polepole, alisema kwamba kuna siri nzito zinazofanya watawala na vibaraka wao waichukie rasimu ya katiba inayoendelea kujadiliwa Dodoma.
Alisema miongoni mwa mambo hayo ni kupunguzwa kwa madaraka ya rais, kuwekewa msisitizo wa maadili ya viongozi, kupunguzwa kwa idadi ya wabunge na kuwekwa kipengele cha kuweza kumng’oa mbunge aliyepo madarakani.
“Sasa hivi mimi naongea kama kijana, kama mwana-asasi za kiraia na vile vile kama Mtanzania mwenye uchungu na nchi yake, mimi simuogopi mwanadamu yeyote na nipo tayari kuyasimamia yote yaliyotajwa na tume yetu (TMK),” alisema na kuasababisha hamasa kubwa ukumbini.
Akiendelea kufafanua kwa kujiamini, alidai kwamba tume yake ilifanya utafiti wa kina na kuyajadili, na kuchuja yote yaliyotokana na tafiti hizo ndipo wakaja na rasimu ambayo inaelekea kuwa mwiba mkali kwa watawala.
“Huwezi ukang’ang’ania muungano katika muundo uliopo sasa ambapo Zanzibar imeunda katiba yake inayosema Zanzibar ni nchi na kisha inakataa kuitambua Mahakama Kuu ya Tanzania, Taasisi ya Viwango (TBS), hawachangii kodi za mapato na wala hawamtambui Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, huu ni unafiki mkubwa,” alimaka Polepole.

Alifichua pia kwamba katika kipindi cha kuunganishwa kwa mataifa haya, Wazanzibari chini ya hayati Abeid Amani Karume walikuwa wanauhitaji muungano kwa udi na uvumba ili kuzuia uwekezano wa kurejea kwa utawala wa Sultani, na hivyo labda leo hawana hofu hiyo tena na ndiyo maana wameamua kuja na katiba yao inayotanguliza utengano badala ya kuongeza ushirikiano.
Alisema kelele za wanasiasa wa Tanzania Bara (Tanganyika) kuililia Zanzibar hazitokani na kuwapenda Wazanzibari, bali kwamba muundo wa muungano uliopo unawabeba wao ili kuendelea kujikita madarakani kwa manufaa yao na kwa hasara kubwa kwa Watanzania waliosalia.
Polepole alishangazwa na kitendo cha Rais Kikwete kushindwa kuilinda katiba aliyoapa kwamba atailinda na kuitetea wakati aliposhuhudia ikivunjwa, lakini akapata ujasiri wa kumshambulia Jaji Warioba na timu nzima na hata Watanzania waliotoa maoni kupitia kwenye timu hiyo.
Wanavyuo wahamasika, waja juu
Baada ya mijadala yao, wanafunzi wa vyuo vikuu walihamasika na kutoa maazimio kama wakisema kwamba wananchi wachukue hatua ya kulivunja Bunge hilo iwapo halileti tija iliyotarajiwa.
Vijana waliipongeza TMK ya Warioba na kudai kwamba jaji huyo huyo aliwahi kuheshimiwa sana alipotafiti mianya ya rushwa, lakini leo anashambuliwa na watawala kwa sababu amegusa maslahi yao.
Walionya mara moja kutumika kwa vitisho kwamba jeshi litaipindua nchi iwapo muundo wa serikali tatu utapitishwa, vijembe na matusi yanayoendelea ndani ya BMK. Na pia walisema watahamasishana ili vijana wote waliofikia umri wa kupiga kura wafanye hivyo na kuleta mabadiliko ya dhati nchini Tanzania.
Walitoa onyo kwa vyombo vya dola kutumika kwa manufaa ya watawala katika kile kinachoitwa “kulinda amani ya nchi” na hivyo kuwageuza vijana kuwa asusa wa kupigwa risasi na kuuawa mara kwa mara pale wanapoonyesha kuwa na misimamo tofauti na watawala wa nchi hii.
Waliahidi kuendelea kuwahamisha vijana wenzao kwa njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutembeleana vijiweni na katika mitandao ya kijamii kama vile facebook, twitter na blog na kushiriki katika mijadala mitandaoni kama vile Jamii Forum, Wanabidii, Wanamabadiliko.
Viongozi wa kiroho nao wachachamaa
Wakati hayo yakiendelea kwa vijana, viongozi wa kiroho nao walionyesha kukerwa na mchakato unavyoendelea na wakapeleka maazimio yao Dodoma kwa ajili ya kumkabidhi Mwenyekiti wa BMK, Samuel Sitta.
Mwamvuli uliotumika unaitwa Baraza la Mahusiano ya Dini mbalimbali kwa Amani Tanzania (IRCPT) watumishi hao wa Mungu kutoka madhehebu ya Kihindu, Baahai, Kikristu, Kiislamu na Wabudha, walitoa maoni na mapendekezo yao kufuatana na mjadala wa katiba mpya.
Walidai kwamba katiba mpya iache kuendekeza mambo ya kufichaficha masuala yanayowahusu wananchi na wakataka katiba mpya ilete uwazi, umoja, ilinde hadhi ya taifa na uwajibikaji. Pia walitaka taifa lizilinde kwa dhati tunu zake kupitia katika katiba yake.

Wakati viongozi hao wakijiandaa kupeleka madai hayo, ndipo hati za muungano zikatolewa hadharani kwa mara ya kwanza jambo ambalo linaacha maswali mengi kuliko majibu, kwamba kulikoni nyaraka hizo za taifa zinafichwafichwa? Je, kuna siri gani inafichwa hapo?
Miongoni mwa mambo muhimu waliyodai katika mkataba mpya ni pamoja na rais mstaafu kufikishwa mahakamani kwa makosa ya kijinai aliyoyatenda wakati akiwa madarakani.
Asasi za kiraia nazo zakerwa
Labda katika kuonyesha ni kwa kiwango gani Watanzania wengi hawaridhishwi na jinsi mchakato mzima wa kupata katiba mpya unavyoendeshwa, asasi za kiraia nazo hazikubakia nyuma.
Akisoma tamko kwa niaba ya asasi zaidi ya 500, mwenyekiti wa jumuiko la mitandao na asasi za kiraia (NGOs) na Networks, Irenei Kiria, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Asasi ya Sikika, alisema wana-azaki wanalaani jaribio la kuuteka nyara mchakato wa katiba kwa manufaa ya watu wachache na kupuuzwa kwa maoni ya wananchi kama yalivyokusanywa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya Jaji Warioba.
mhegera@gmail.com Simu: 0754-826272

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni