Jumapili, 6 Julai 2014

MAPIGANO YA WAKULIMA NA WAFUGAJI NI AIBU KWA TAIFA



pichani ni miongoni mwa nyumba ambayo ziliteketezwa na inaosadikiwa kuwa ni wafugaji wa Kimasai katika mgogoro wa kugombea ardhi katika bonde la mto Mgongola wilayani Mvomero 

Na Elias Mhegera
Oktoba 28 /2013
Miongoni mwa majukumu magumu kabisa ambayo mtu anaweza kuachanganyikiwa na kukosa ufumbuzi iwapo atakabidhiwa ni jukumu la kusuluhisha migogoro inayoendelea nchini Tanzania kati ya wakulima na wafugaji.
Na kwa msingi huo naamini kwamba nitaitendea haki mada ninayotaka kuijadili kwa sasa iwapo nitavaa joho la msuluhishi asiye na upande katika migogoro yenyewe. Na pili ni lazima niwe na busara ya kukumbuka kwamba wanaouana ni Watanzania wenzangu tena kutoka tabaka moja la ‘walalahoi’ lililosahaulika.
Kwa bahati mbaya wakati hali hiyo ikiendelea kuna mabadiliko kadha wa kadha yanaotokea nchini ambayo ni ya kisiasa, kiuchumi, kiitikadi na hata kimaadili ambayo yamesababisha umiliki wa ardhi ulete migogoro mikubwa isiyo na kifani.
Katikati ya maendeleo hayo hasi kuna jambo limejitokeza nalo ni kusambaratika au kudhoofika kwa nguvu ya dola inayolenga katika kuwaunganisha Watanzania, na badala yake kuibuka kwa matumizi makubwa ya nguvu za dola na hivyo kuzidisha uchonganishi badala ya upatanishi mfano hai ukiwa ni Kiteto.
Mchango wa viongozi
Ni dhahiri ukitaka kuijadili migogoro mikubwa inayoendelea nchini ni lazima uanze kwa muktadha mpana wa kuangalia tulikotoka na kule tunakoelekea. Kwa mfano miaka ya utawala wa Mwl. Julius Nyerere alilenga kuupenda ujamaa, kilimo, na Uafrika.
Leo hii taarifa nyingi kuanzia katika asasi za kiraia (NGOs) na hata za waandishi wa habari mikoni zinaonesha kwamba NGO zinazojihusisha na masuala ya ardhi na mazingira zipo katika hali ngumu kiusalama na pia wanahabari wanakuwa na hali ngumu pale wanapogusia masuala ya ardhi.
Katika ujumla wao watetezi wa haki za binadamu wanakuwa na changamoto zaidi pale wanapogusa maslahi ya ardhi ambayo kimsingi ni ya kisiasa. Kwa mfano Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Jukwaa la Katiba (JUKTA) na hata Chama cha Wanasheria wa Mazingira (LEAT) hawawezi kuwekwa katika kundi moja na NGO zinazotetea wanawake na watoto kama vile WLAC au TAWLA.
Katika muktadha huo huo waandishi wa habari wanaguswa na vyombo vya dola pale wanapoandika juu ya ufisadi katika halmashauri za miji kwa sababu huko kuna miungu watu waliojitangazia ufalme na pale wanapogusa maslahi ya wakubwa kama vile ardhi zinazoporwa kutoka mikononi mwa wanyonge.
Binafsi nimebahatika kutembelea mikoa taribani 18 ya Tanzania Bara na pia Unguja na Pemba. Nimehuhudia jinsi ambavyo viongozi wetu waliopo madarakani na wale waliostaafu wanavyojimilikisha maeneo makubwa ya ardhi hali ambayo sasa imesababisha uhaba mkubwa wa raslimali hiyo kwa wakulima na wafugaji ambao kwa upande wao wameshindwa kumtambua adui yao halisi ni nani.
Tembelea Morogoro, Manyara, Bahi n.k.  utakuta wakuu wa wilaya wamehusika kwa kiwango kikubwa katika kupora ardhi kwa niaba ya wakubwa zao waliowatuma. Na kwa maana hiyo basi wakati mwingine ndiyo maana wanashindwa kuitatua kwa sababu kimantiki ni vigumu kwa mtu yeyote kuutatua mgogoro kwa weledi yakinifu iwapo yeye mwenyewe anamaslahi ndani ya mgogoro huo.
Mgogoro wa Mvomero
Ingawaje mwandishi wa makala hii hajafanya tafiti za kina juu ya migogoro ya ardhi lakini kwa kiwango fulani anaweza kujigamba kwamba ana uelewa wa kutosha wa kuizungumzia. Kwani amewahi kuhudhuria warsha kadhaa za HakiArdhi, taasisi inayojihusisha na tafiti na ufuatiliaji wa masuala mbali katika ardhi na hata kufanya mahojiano na afisa mwandamizi wa taasisi hiyo Wakili Joseph Chiombola kwa ajili ya uandaaji wa makala kama hii.
Pia amepata kuwapokea wakulima kutoka mkoani Morogoro kwa nyakati tofauti tofauti na kuwasaidia kutoa taarifa zao kwenye vyombo vya habari. Kilichodhahiri kutokana na tafiti zake ni kwamba Mkoa wa Morogoro ni miongoni mwa mikoa iliyoathirika sana kutokana na uvamizi wa matajiri wengi wakiwamo viongozi wa serikali kutoka Dar es Salaam.
Kwa lugha nyingine ukaribu wa mkoa huo na jiji la Dar es Salaam ndiyo umechagiza zaidi ulafi wa wenye pesa katika kijitafutia maeneo makubwa ya ardhi mkoani humo. Katika siku za hivi karibuni lugha kuu zinazotumika ni kama tatu hivi. Kwanza ni Kilimo Kwanza, pili ni Hafidhi za Taifa na tatu ni Utunzanji wa ardhi oevu chini ya Mkataba wa Ramsar nchini Iran wa mwaka 1971.
Mazoezi yote hayo yamekuwa yakiendeshwa bila ushirkishwaji wa kutosha wa wakulima ambao wengi wao uelewa wao ni mdogo.  Kwa mfano katika mkutano mmoja ambao mwandishi wa makala hii alihusika kwa kumsaidia kiongozi wa wakulima kutoka Morogoro, kiongozi wa msafara alidai kwamba ardhi yao imeporwa na akakabidhiwa muarabu mmoja anayeitwa Ramsar.
Msafara huo ulikuwa na watu wasiopungua kumi, ikabidi kuwauliza wakulima wale suali la kizushi kama wote wamewahi kumuona huyo muarabu anayeitwa Ramsar wakasema ni kweli wamekuwa wakimuona na kisha wakaanza kuelezea jinsi alivyo.  Mkanganyiko huo ulitosha kuonesha kwamba hapakuwa na ushirikishwaji wa kutosha kwa wakulima hao kabla ya kuanza kuwanyakua mashamba yao.
Kwa hiyo taswira nzima ya mkoa wa Morogoro haipishani sana isipokuwa namna masuala hayo yanavyoshughulikiwa. Mgogoro wa Mvomero ulimpatia nafasi mwandishi wa makala hii kushuhudia kinachoendelea mikoani ambako kuna vita vya wenyewe kwa wenyewe katika jina la wakulima na wafugaji ili labda kuondoa dhana ya kwamba wanaopigana ni Watanzania wenzetu.
Mgogoro wa Mvomero una taswira nyingi na labda unaweza kufananishwa kwa kiwango fulani na ule wa Kiteto. Mwandishi wa makala hii alifika wilayani Mvomero akiwa ni mmoja wa wajumbe wa asasi za kiraia nne, yaani ya wafugaji PINGOs kutoka Arusha, HakiArdhi kutoka Dar es Salaam, Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC) kutoka Dar es Salaam ambao mwandishi wa makala hii uliuwakilisha.
Baada ya kufika Morogoro timu hii iliunganika na taasisi mbili zenye makazi yao mkoani humo, yaani Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (MVIWATA) na Parakuiyo Pastoralist Indegenous Community Development Organisations (PACODEO) na pia ikaunganika na wanahabari Michel Msilo (ITV) na Juma Mtanda (Mwananchi) ambao walikuwa wameuripoti mgogoro huo kwa kina.
Muhtasari wa visa na mikasa
Ili msuluhishi apate busara katika mgogoro huu ni vyema awaangalie wafugaji na wakulima kwamba wote ni sawa na watoto wake waliokosa maridhiano lakini yeye anawapenda wote kwa kiwango sawa.
Mtazamo wa nani ni mkorofi, nani siyo, nani ana nyaraka, nani hana, nani ni mwenyeji nani ni mgeni na labda nani anatumiwa na anatumiwa na yupi n.k. ndicho chanzo kikubwa cha kushindikana kwa muafaka wa mgogoro huo kwa njia ya majadiliano.
Kuna mengi yametokea wilayani Mvomero licha ya vifo vya zaidi ya watu 30, bado mpaka sasa kuna makovu ya watu kuchomewa nyumba na akina mama toka pande zote mbili za wakulima na wafugaji wakidai wamekuwa wakitishiwa kubakwa. Wawakilishi wa NGOs walikuwa na wakati mgumu kidogo wa kuchambua nani anasema ukweli kati ya wafugaji na wakulima chini ya umoja wao wa Umoja wa Wakulima Mgongola (UWAMGO)  
Eneo lililosababisha mauji ya watu sita mmoja akiwa ni mfugaji na wakulima watano ni bonde la mto Mgongola, Kambala, Hembeti, Mkindo na Msufini ambako kuna baadhi ya wakulima wanaishi na wengine kutoka kijiji kimoja kwenda kingine kwa ajili ya kilimo.

Hebu jaribu kudodosa kauli hizi za viongozi kama ifuatavyo;
Msimamo wa MVIWATA
Mkurugenzi wa MVIWATA Bw. Stephen Luvuga anaonesha uelewa na ushirikiano wa hali ya juu katika kutafuta utatuzi wa mgogoro huo. Hata hivyo katika maelezo yake anaonesha dhahiri kuwa na huruma kwa wakulima ambao chombo chake kimuundo ndiyo hasa jukumu lake kuhakiksha kwamba maslahi ya wakulima yanakumbukwa katika undeshaji wa nchi.
Hata hivyo Bw. Luvuga hafichi hisia zake anapoeleza kwamba mgogoro huu unamaslahi mengi yaliyofichika ingawaje hata baadhi ya wahusika wenyewe (wagomvi) hawayafahamu maslahi hayo na badala yake wamezingwa katika mitazamo ya kikabila na kutawaliwa na hasira kali zenye madhara makubwa.
Msimamo wa Askofu Jacob Maneo wa KKKT
Kiongozi huyo wa kiroho na Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania ni mtumishi wa Mungu mwenye viapo vya kuutetea ukweli bila woga. Anaeleza kwa kina anavyoufahamu mgogoro wenyewe tena akiwa na uchungu mkubwa kwa sababu baba yake mzazi Marehemu Paul Sendeu Moreto aliuawa mwaka 1991 wakati akitafuta ufumbuzi wa migogoro ya ardhi. 
Askofu huyo anaeleza kwamba anasikitishwa na jinsi baadhi ya vyombo vya habari vilivyokuwa vinaripoti matukio ya mgogoro huo na kuwafanya wanajamii ya Kimasai ambao yeye ni miongoni mwao waonekane kwamba ni watu katili. Anaeleza pia jinsi ambavyo jamii hiyo ya wafugaji wanavyoteseka na kwamba sasa wanatakiwa kuondolewa kwa kuonekana kwamba ni wavamizi.
 Msimamo wa wafugaji
Kwa upande wao wanajitetea kwamba wanauhalali wa kuishi katika maeneo yaliyopo bila kubughudhiwa kwa sababu wanazo nyaraka halali za makazi na shughuli za ufugaji ambayo kwa sasa yanagombewa. Wanatoa nyaraka zao kwa timu ya NGOs na kwa waandishi walioambatana na timu hiyo. Inadhhirika kwamba nyaraka hizo ni za muda mrefu na pia kuna ramani iliyochorwa kitaalamu.
Wakiongozwa na diwani wa zamani wa Kata ya Hembeti, Majuka Koira wanasema wamekuwapo kwa miaka mingi katika maeneo hayo na wanashangaa leo kuitwa kwamba ni wavamizi. Bw. Koira anasema alisoma katika Shule ya Msingi Hembeti mwanzoni mwa miaka ya 70. Anakosoa kwamba wakulima wamekodi kikundi cha Umwano ambacho hakitokani na wanavijiji hao bali ni watu wa kukodiwa kwa lengo la kuwadhuru wafugaji.
Msimamo wa wakulima
Wakiongozwa na mwenyekiti wa Bi. Zawadi Juma Chande wanaonekana kuwa na uchungu na hasira dhidi ya wafugaji na kuwaita majina ya kuwakana kama vile Wamasai au Wakenya. Lengo mahsusi la lugha hizo ni kuwakana ili waonekane kwamba ni wageni wavamizi.  Wanaikanusha historia ya Askofu Maneo na ile ya Bw. Koira ambaye wanasema hasemi ukweli.
Wanahitimisha kwa kusema kwamba ongezeko la ghafla la mifugo limetokana na kufukuzwa kwa wafugaji wa Kimasai kutoka maeneo mbali mbali nchini na mwisho wa siku kuzamia Mvomero ambako wamepata unafuu. Kwa mujibu wa wakulima wafugaji hao ni watu wakorofi na wapenda vita.
Msimamo wa Mkuu wa Wilaya ya Mvomero Anthony Mtaka
Kwa bahati mbaya DC huyu kijana anaanza kwa kuwatazama wawakilishi wa NGO kwa mtazamo hasi kama ilivyokawaida kwa viongozi wengi serikalini ambao huona kwamba  asasi za kiraia zina tabia ya kukosoa hata pale zisipostahili kufanya hivyo. Kwa hiyo badala ya kujibu maswali yeye ndiye akawa muulizaji mkubwa kwa maswali kama “kwani nyie mlitakaje?” au wewe ungefanyeje? Hatimaye timu ya NGO inamuomba asilete malumbano yasiyo na tija.
Hapo DC anateremsha munkari na kuanza kujibu kwamba yeye amejitahidi kwa kadri ya uwezo wake kutatua mgogoro huo lakini kilichomkera ni pale magari kadhaa ya watendaji wake yaliporushiwa (kupopolewa) kwa mawe na wakulima wenye “hasira kali” kiasi kwamba licha ya kufunga bara walidhamiria hata kuwaduru viongozi wa wilaya.
Msimamo wa Afande OCD Idd Abdallah Ibrahim
Anakiri kwamba kutokana na ugeni wake katika eneo hilo bado hajauelewa mgogoro huo kwa undani lakini hata hivyo anaamini mbinu sahihi za usuluhishi hazitumika. Anashauri kwamba watendaji wangejipatia muda wa kutosha ili kuizisikiliza pande kuu zinazokinzana kwa nyakati tofauti na kisha kuwaweka pamoja wote wakulima na wafugaji.
Maoni ya Mkuu wa Mkoa Joel Bendera
Labda miongoni mwa mambo yaliyowashangaza wawakilishi wa timu ya NGO ni ile hali ya woga aliyokuwa nayo mkuu wa mkoa. Pamoja na kwamba RC huyo alitoa ushirikiano wa dhati kwa timu ya NGO lakini anaonekana kama vile anayejaribu kuukwepa mgogoro wenyewe.
Katika utetezi wake anadai kwamba mgogoro wenyewe upo katika Mahakama Kuu Kitengo cha Ardhi hivyo yeye hawezi kuuingilia mhimili huo ingawaje anakiri kwamba tayari alimuomba Jaji Mkuu Othman Chande ili kesi hiyo iharakishwe. Na pia anasisitiza kwamba mgogoro huo umo katika eneo la kiutendaji la DC wa Mvomero.
Mapendekezo ya asasi za kiraia
Miongoni mwa mapendekezo muhimu kutoka katika NGOs ni kwamba viongozi wa mkoa hawastahili kutoa utetezi wa aina yoyote na kwamba katika mazingira hayo DC hawezi kuachiwa kutatua mgogoro ambao umesababisha mauaji ya watu mara kadhaa. Hali kadhalika si jambo jema kwa kiongozi kujitenga na mgogoro unaendelea katika eneo lake kwa kisingizio cha kuogopa kuingilia uhuru wa mahakama, hadi mwaka jana mgogoro ulikuwa mahakamani kwa zaidi ya miaka minane.
Asasi za kirai zinashauri kwamba wabunge wa majimbo mawili la Morogoro Mjini Aziz Aboud na wa Mvomero Bw Amos Makala kwa kushirikiana na Mkuuwa Wilaya ya Mvomero, Mtaka, na Mkuu wa Mkoa wa Mkoa wa Morogoro, Bendera, wakutane mara kwa mara ili kupeana maendeleo ya usalama katika wilaya hiyo mpya na changa.
Na vivyo hivyo viongozi mbali mbali likiwamo Jeshi la Polisi na wanajamii wengine wajitahidi kuingilia katika kutatua migogoro badala ya kusubiri mauaji yatokee ndipo waanze kuhesabu miili ya marehemu na kulaani mauaji kama ilivyogeuka kuwa mchezo wa kawaida sasa.
Pia kuwepo na muingiliano wa kijamii kama vile michezo ya ujirani mwema kati ya wakulima na wafugaji, kupata chakula na vinywaji kwa pamoja, ngoma za kimila na hata kuoleana kwa makabila ya pande hizo mbili kama ilivyo jadi nchini Tanzania.
Tuwasiliane: mhegera@gmail.com simu: 0754-826272



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni