Jumapili, 6 Julai 2014

HATUJAWAFADHILI UMOJA WA KATIBA YA WANANCHI -KAS




Wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba wanaotokana na vyama vya CHADEMA, CUF, NCCR-Mageuzi na DP kikiwakilishwa Mch. Christopher Mtikila, wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), wakiondoka bungeni kwa madai kwamba wenzao CCM wameuteka nyara mchakato wa kupata katiba mpya. 

Na Elias Mhegera
Taasisi ya Kijerumani yenye uwakilishi nchini Tanzania ya Konrad Adenaeur Stiftung (KAS) imekanusha kwamba inawafadhili wabunge wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) ili wasusie vikao vya Bunge Maalumu la Katiba.
Katika mahojiano yaliyofanyika ofisini kwake mtaa wa Upanga Isimani hivi karibuni, Mwakilishi Mkazi wa KAS nchini Tanzania Bw. Stefan Reith alisema anasikitishwa na propaganda chafu zinazoelekezwa kwa taasisi yake kwamba ndiyo inayowafadhili UKAWA kwa lengo la kuharibu mchakato wa kupatikana kwa katiba mpya.
“Ninasikitika kwamba kuna waandishi wanaoshindwa kuzingatia maadili ya taaluma yao na kisha wanaandika habari za kutunga mezani ambazo zinaweza tu kuandikwa na waandishi wasio ifahamu vizuri taaluma yao na pia kuchapishwa na vyombo visivyoheshimika.” anasema.
Kujiondoa kwa wabunge wa vyama vya upinzani vya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Chama cha Wananchi (CUF) na National Convention for Construction nand Reform (NCCR-Mageuzi) kumeleta sintofahamu iwapo kweli katiba mpya itapatikana katika mazingira ya sasa.
Kujitoa huko kulikofanyika mwezi Aprili kumesababisha pia mgawanyiko mkubwa kwa wananchi kwa ujumla huku wale wanaounga mkono muundo wa serikali tatu wakiwaunga mkono UKAWA na wale wanaopenda muundo wa serikali mbli uendelee wakiwashambulia wabunge hao wa upinzani.
“Si taasisi yangu wala ubalozi wa Ujerumani tunaowafadhili UKAWA, bali kinachoendelea ni matunda ya mabadiliko ya kisiasa ndani ya Tanzania. Gazeti hilo limeaindika uongo mtupu kwa kudai eti tunatoa kiasi cha shilingi 450,000 kwa siku na ndiyo maana wabunge wa UKAWA wameamua kujitoa kwa sababu posho yao ni shilingi 300, 000/= huu ni uzushi mkubwa” anasema Reith.
Pia anashangaa kuona kwamba mashambulizi yanaelekezwa kwenye taasisi yake sasa bila kukumbuka kwamba taasisi hii imekuwapo nchini Tanzania kuanzia mwaka 1964 walipoanza ujenzi wa chuo cha itikadi cha TANU Kivukoni, kwa wakati huo, kwa sasa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere. 
Anakumbusha kwamba taasisi yake ambayo kwa sasa inashambuliwa pamoja na kuwa mstari wa mbele katika kutibu majeraha yaliyosababishwa na kampeni chafu za udini ambazo zilisababisha kuanza kwa mitafaruku ya udini ambayo tayari ilikwisha sahaulika nchini kwa muda mrefu.  
Anashangaa kuona kwamba taasisi yake ndiyo inashambuliwa kwa taarifa mbaya wakati zipo taasisi nyingine kutoka nchini mwake na hata nje ya Ujerumani zikiwa na mahusiano na vyama vya siasa vingine kama ilivyokuwa kwa CHADEMA na KAS.
“Kuna shirika la Friederich Ebert Stiftung (FES) ambalo linaushirikiano na Chama Cha Mapinduzi (CCM) lakini halishambuliwi, kuna shirika la Friederich Naumann Stiftung lenye ushirikiano na (CUF) lakini yote hayo hayashambuliwi, mitazamo ya kuishambulia KAS ni hafifu” anasema.
Bwana Reith anasema kwa upande mwingine mashambulizi hayo yanampatia faraja kwamba shirika lake linafanya kazi nzuri. Lakini anaonya tabia ya kulihusisha shirika lake na masuala ya dini kwa sababu hilo siyo lengo lao hata kidogo.

Kinyume chake anakumbusha kwamba shirika lake limeitisha mikutano mingi kulikoni taasisi yoyote hapa nchini Tanzania na hata kuchapisha taarifa za mikutano hiyo na kuwakaribisha wanaoyahitaji waende ofisini kwake. Anasema machapisho hayo yamewahusisha watu wa dini zote kama vile Wakristu, Waislamu, Baahai , Wahindu n.k katika kutafuta amani ya kudumu nchini Tanzania.
Anasema Baraza la Viongozi wa Dini la Kutafuta Amani Tanzania (IRCPT) ni mshirika wake mkubwa na watu wote makini wanalifahamu hilo hivyo anasikitishwa na tabia ya kuingiza udini katika shughuli za KAS-Tanzania.
“Nakemea sana kampeni za udini kwani ndizo zimesababisha majeraha makubwa katika jamii ya Watanzania, viongozi kadhaa wa kiroho wameshambuliwa, makanisa yamechomwa moto, haya yote ni makovu ya siasa chafu za uchochezi,” anasisitiza.
Ni dhahiri malalamiko hayo ya Bw. Reith yatarejesha kumbukumbu kwamba kampeni za udini ziliwahi pia kufanywa na chama hicho hicho bingwa wa kuwagawa Watanzania kwa manufaa ya muda mfupi kama ilivyofanyika mwaka 2000 dhidi ya Prof. Ibrahim Lipumba akigombea kwa tiketi ya CUF.

Bw Reith anasema njia pekee ya hao wanaoeneza kampeni chafu dhidi ya shirika lake ni kujibu hoja za wananchi katika masuala kadhaa yanayoendelea nchini kama vile kwa nini Watanzania wanataka maoni ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba (Tume ya Jaji Warioba),  yazingatiwe, na vile vile mambo mengine kadhaa.
Anawashauri wanahabari kufanya uchunguzi wa kina ili kuwabaini wanaohusika na uharamia dhidi ya tembo na faru katika mbuga za wanyama, na hata dhidi ya ufisadi katika maeneo mbali mbali yaliyotajwa katika sekta za madini, nishati na Benki Kuu ya Tanzania.
Anawasihi wanahabari kutoa msaada wa mawazo kwa serikali ni jinsi gani inaweza kushughulikia suala la deni kubwa la taifa, tatizo la ajira, kuanguka kwa sekta ya elimu na hata ubadhirifu katika sekta ya usafirishaji. Hususani ukwepaji wa kodi bandarini n.k.
Malalamiko ya Bw. Reith yanakuja wakati ambapo makundi mengi ya wanajamii wakiwamo wasomi, asasi za kiraia na hata viongozi wa kiroho Waislamu kwa Wakristu, wakidai kwamba Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya Jaji Joseph Warioba ilizingatia maoni ya wananchi kwa hiyo ni bora yakazingatiwa badala ya kutanguliza itikadi za vyama.
Ni wakati muafaka sasa kwa watawala na mawakala wao wakafahamu kwamba katika jamii yoyote iliyostaarabika ni lazima kutakuwapo ni mijadala yenye kuleta afya na manufaa kwa jamii hata kama mijadala hiyo haiwafurahishi watawala hao.
Suala la katiba mpya si mali ya CCM, CHADEMA, CUF wala NCCR-Mageuzi bali ni mchakato wa Watanzania na hivyo hakuna mwenye haki ya kumuita mwenzake kwamba ni mchochezi.

Tuwasiliane: mhegera@gmail.com 0754-826272

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni