Jumatatu, 14 Julai 2014

NKWABI NG’WANAKILALA: MSOMI, MJAMAA WAKALA NA MFUASI WA FALSAFA YA KIAFRIKA ‘UBUNTU’!

Marehemu Nkwabi Ng'wanakilala, mwanazuonii aliyetangulia mbele ya haki 

Na Elias Mhegera
Miongoni mwa habari zilizoshtua Watanzania wengi kwa kiwango kikubwa hivi karibuni ni kifo cha mwanahabari mahiri Nkwabi Ng’wanakilala, kilichotokea jijini Mwanza na baadaye mwili wake ukaletwa Dar es Salaam kwa ajili ya maziko.
Kwa kawaida wanapofariki watu wa aina ya mwandishi huyo mahiri huwa hawajadiliwi wao bali yale waliyoyasimamia. Sitaki kusema hapa kwamba yeye alikuwa mtakatifu na nikifanya hivyo nitakuwa mnafiki mkubwa.
Lakini kwa upande mwingine ninajiona kwamba nina wajibu wa kushiriki katika zoezi la kumuaga hapa duniani kwa njia ya kalamu walau hata kwa sababu moja tu, kwamba alikuwa mwalimu wangu katika Chuo cha Mt. Agostino jijini Mwanza.
Nasema kwa sababu hiyo moja tu nilitakiwa kuwa sehemu ya kumuaga walau katika kuuweka mwili wake kaburini, lakini kwa bahati mbaya sikupata nafasi hiyo kwa sababu zisizozuilika. Lakini labda mimi nina sababu mbili za ziada za kumuenzi mzee huyo.
Kwa wale waliofundishwa na marehemu Ng’wanakilala masomo mawili ‘media and democracy’ au ‘media and politics’ hapo ndipo haswa lilikuwa eneo lake.
Alishangazwa na tabia ya wasomi kuzungumzia somo la maadili kwa kunukuu mambo ya Ulaya tu kama vile hapa Afrika hapajawahi kuwa na maadili. Hivyo akaunga mkono watetezi wengine wa maadili ya Kiafrika (Afriethics).
Marehemu huyu gwiji wa habari alipata kuniambia kwamba niachane na mtindo wa kuandika makala pekee na badala yake nielekeze nguvu katika uandishi wa vitabu kwa sababu ya utunzaji wa kumbu kumbu za siasa.
Alipendelea kuniita mwalimu kwa sababu nimesoma mara tatu Chuo cha Mt. Agustino taaluma za uandishi na muda huo huo nikiendelea na ualimu katika seminari ndogo ya Mt. Maria Nyegezi mahali ambapo pia nilisoma kwa miaka sita kidato cha kwanza hadi cha sita na kurejea kama mwalimu miaka 19 baadaye nikafundisha kwa miaka minne.
Akizoea kuniambia; “mwalimu mimi nitabakia mwana CCM daima lakini hii iliyopo sasa siyo ile ya Mwalimu Julius Nyerere, hii ni ya wachumia tumbo” kisha aliangua kicheko mara kadhaa alipozungumza mada za aina hiyo.
Sifa moja aliyokuwa nayo ni kwamba yeye alikuwa ni mtu wa marika yote akiwa na vijana hujiona kana kwamba ni kijana mwenzao na mara akairejea kwa watu wa makamu yake huongea kwa namna inayostahiki kwa rika hilo.
Mwaka 2005 katika sherehe za kuazimisha uhuru wa habari ambapo yeye alishirikiana nasi kulikuwa na mchezo wa kuvutana kwa kamba. Kwa bahati nzuri mzee huyu alikuwa upande wangu na mgeni rasmi ambaye alikuwa ni mkuu wa wilaya ya Nyamagana akawa upande wa pili.
Niliwekwa mbele na upande wa pili akawekwa Bw. Emmanuel Chacha mwandishi wa The Guardian nakumbuka nilipata nguvu za ziada tukawaangusha wenzetu nguvu zangu kama mtangulizi zilitokana na heshimwa kwa mzee huyo na wavuta kamba wote wanafahamu mtu wa mbele ni muhimu sana katika zoezi hilo.
Kwetu sisi tuliobahatika kufundishwa na watu ambao licha ya kuwa wahadhiri pia wamewahi kushika nyadhifa serikalini basi somo halikuwa nadharia peke yake bali kubadilishana uzoefu au labda niseme kupokea uzoefu wa wakongwe hao.
Licha ya Ng’wanakilala alikuwapo Profesa Fortunatus Lwanyantika Masha ambaye muda mwingine alituchekesha kwamba Mwalimu Nyerere hakuwaamini watu kama yeye waliosomea Marekani. “nilikuwa na bahati mbaya Mwalimu aliponiona siku ya kwanza akauliza huyo kijana anatoka wapi? ni Mtanzania huyo?
Profesa Masha alisema Mwalimu Nyerere aliuliza hivyo kwa sababu alimuona akitanga tanga kutafuta picha akiwa na kamera mkononi akiwa amevaa suti za kimagharibi. Kwa hiyo kwa Mwalimu Nyerere maadili ya Kitanzanaia na hasa kwa viongozi hakuyaangalia katika umiliki wa mali bali hata mavazi yao.
Walimu aina ya Ng’wanakilala na Masha walikuwa wanakumbusha mara kwa mara kwamba wanahabari wanaweza kuirudisha Tanzania mahali pake, sielewi ni kwa kiwango gani wanahabari wanatamiza azma hiyo,  wasomaji ndiyo wanaweza kutuhukumu.
Marehemu Ng’wanakilala alizoea kusema kwamba misingi ya mwalimu ilianza kuporomoka pale nchi iliporuhusu mfumo wa vyama vingi mwaka 1992. Anasema kipindi cha mfumo wa chama kimoja viongozi walichunguzwa sana maadili yao.
Anasema kinyume chake baada ya kuruhusu siasa za ushindani mafisadi walianza kukifadhili Chama Cha Mapinduzi na kisha watu hao hao wakatokea kuwa wakwepa kodi wakubwa na wengine wakijihusisha na ufisadi mkubwa wa aina mbali mbali.
Pia akasema urafiki mkubwa kati ya viongozi wa CCM na baadhi wafanyabiashara wakubwa ulikuwa unafifisha vita dhidi ya ufisadi. Siku moja akaja na rundo kubwa la magazeti na kutuambia tusome jinsi mgogoro kati ya wafanya biashara Yusufu Manji na Mwenyekiti Mtendaji wa IPP Mzee Reginald Mengi ulivyokuwa unaripotiwa.
Akauliza “nyie wachambuzi mnaona hapo serikali ipo upande wa nani katika mgogoro huu? je ni kwa nini hali hii inajitokeza? haya ndiyo mambo mnayotakiwa kujiuliza kama wanataaluma” akasema.
Kipindi kile mara kadhaa vyombo vinavyomilikiwa na IPP Media viliandika kwamba kulikuwapo na ubia wa kutia mashaka kati ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) , CCM na Serikali yake.
Naamini njia mojawapo ya kumuenzi mwanahabari huyo mahiri itakuwa ni kupambana na ufisadi na pia kuyapitia machapisho pamoja na vitabu vyake ili kuusambaza ujumbe wake kwa kizazi cha sasa.
tuwasiliane: mhegera@gmail.com simu 0754-826272

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni