26/09/2013 | Elias Mhegera |
KUKATALIWA kwa Balozi mpya wa Ujerumani, Hellwig-Boette, si
jambo geni katika ulimwengu wa kidiplomasia, lakini jambo hilo limeacha maswali
mengi kuliko majibu.
Maswali hayo yanatokana na ukweli kwamba mwanadiplomasia huyo
ameacha rekodi nzuri ya kupinga vitendo vya uvunjifu wa haki za binadamu nchini
Kenya.
Inasemekena ni mmoja wa washinikizaji wa kupelekwa The Hague,
Uholanzi watuhumiwa wa mauaji ya kimbari ya mwaka 2007baada ya Uchaguzi Mkuu wa
Kenya.
Lakini kukataliwa huko kunaacha maswali iwapo kuna uhusiano
wa jambo hilo na madai ya kwamba Ujerumani kupitia taasisi yake ya kupigania
demokrasia duniani ya Konrad Adaneur Stiftung (KAS), imekuwa nyuma ya mafanikio
ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Labda jambo la kushangaza ni kwamba uhusiano kama huo upo pia
kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na taasisi nyingine kutoka huko huko Ujerumani ya
FES, uhusiano ambao ulianza mwaka 1965.
Pia Chama cha Wananchi (CUF) kina uhusiano na taasisi
nyingine kutoka Ujerumani ya FNS tangu mwaka 1997.
Ingawa dhana ya kuamini kwamba mafanikio ya CHADEMA
yanatokana na ufadhili kutoka nje ni kiashiria cha uvivu wa kufikiri, lakini
pia tukio la kukataliwa kwa balozi huyo kunaonesha kwamba serikali yetu
imejikita katika kutafuta mchawi wa nje badala ya kuangalia wapi panapoleta ufa
wa kiuongozi ndani ya nchi ili kuuziba ufa huo.
Busara ndogo inatosha kuonesha kwamba kukubalika kwa CHADEMA
si zao la misaada ya ‘Wazungu’ au udini na ukabila kama ambavyo watu
waliofilisika kimawazo wanavyopotosha umma wa Watanzania.
Kinyume chake ni kwamba ahadi hewa na kushindwa kujibu
maswali ya wananchi kwa ufasaha ndicho chanzo cha kuporomoka kwa kasi kwa chama
tawala.
Kwa haraka haraka inaonesha kwamba miji yote yenye
mikusanyiko mikubwa ya vijana hususan wamachinga ndiyo ngome kuu ya CHADEMA,
kwa hiyo hasira ya vijana inatokana na kurubuniwa kama mtoto anavyonyamazishwa
kwa ahadi ya pipi kunakofanywa na watawala wetu wakati wa chaguzi kuu.
Ni dhahiri kukataliwa kwa balozi huyo hakutakuwa mwisho wa
uhusiano mzuri na wa kihistoria kati ya Tanzania na Ujerumani, kwani yapo mambo
mengi yanayoashiria kwamba uhusiano huu una mizizi kuliko upotoshwaji
unaofanywa na baadhi ya wanasiasa wazembe.
Ripoti iliyochapishwa na Mkurugenzi Mkazi wa KAS, Stefan
Reith, akishirikiana na mtafiti Danja Bergmann ilileta taharuki ilipochapishwa
na magazeti mbalimbali likiwamo Tanzania Daima.
Ndipo wakaibuka waandishi kuijibu ripoti hiyo wakidai kwamba
ushirikano kati ya CHADEMA na KAS umejikita katika misingi ya udini, hususan
dini ya Kikiristu, ambayo inatuhumiwa kuwa nguvu ya chama hicho kupitia kwa
madhehebu mbalimbali ya dini hiyo.
Ni ujinga kuuaminisha umma wa Watanzania kwamba eti uhusiano
wa Christian Democratic Union (CDU), KAS na CHADEMA ni wa kidini, sasa ule wa
CCM na FES au CUF na FNS ni wa ufisadi, rangi au nini?
Ingawa tunaamini kwamba Watanzania walio wengi kwa sasa
wamekwisha kufunguka na hawawezi kudanganywa na propaganada za kijinga kama
hizo, lakini pia ipo hofu kwamba zisipokemewa zinaweza kuaminika na kujenga
matabaka na chuki katika jamii yetu.
Wakosoaji marafiki wanafanya hivyo kwa sababu nchi
wanayoipenda ya Tanzania imeingia katika majanga ambayo hayajawahi kushuhudiwa
katika miaka 50 na zaidi ya uhuru wake.
Matukio ya hivi karibuni yanaogofya, si kwa watalii tu bali
hata kwa Watanzania wenyewe. Kwa mfano mtu anaweza kushambuliwa na kuumizwa
mwili wake na bado vyombo vya dola vikashindwa kumpata au kuwapata wahusika.
Majanga yaliyotokea na kukosekana kwa wahusika wa uhakika ni
pamoja na utekwaji wa Dk. Stephen Ulimboka, kiongozi wa Jumuia ya Madaktari Tanzania,
kutekwa kwa Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri, Absalom Kibanda na mauaji ya
Padri Evarist Mushi huko Zanzibar.
Yapo matukio mengine ya kutisha kama vile mashambulio ya
mabomu mara mbili mjini Arusha, moja likiwalenga waamini wa Kanisa Katoliki na
jingine kwa wafuasi wa CHADEMA. Lakini pia uchomaji wa makanisa Mbagala na
Zanzibar.
Mambo ya uchochezi wa udini kwa malengo ya kisiasa ndiyo
yalisababisha mauaji ya Mchungaji Mathayo Kachila wa Kanisa la Pentekoste
Buseresere, Geita.
Matukio ya aina hii yanaonesha kwamba dola imeshindwa
kutimiza wajibu wake wa kuwalinda raia na mali zao. Kwa hiyo serikali yetu
ikikumbushwa na marafiki wa muda mrefu wa nchi yetu kama ilivyokuwa kwa KAS,
wasikimbilie kurusha lawama bali wajizatiti pale walipoanguka.
Wale wanaozusha uongo kwamba taasisi kama KAS imedhamiria
kuiangusha CCM waangalie upande wa pili kwamba kuna taasisi gani nyingine
ambayo imewahi kugharimia mikutano ya maridhiano ya dini mbalimbali hapa
Tanzania ikiwa ni Wakristu, Waislamu, Wahindu, Mabudha, Baahai na wengineo
kupitia ushirika wa IRCPT.
Itoshe kwa ujumbe huu kusema kwamba kabla watu wasioitakia
mema nchi hii hawajaanza kurusha makombora kwa taasisi za wageni wajiangalie na
kujitathmini wao kwanza, wabaini chanzo na ndipo wapate ufumbuzi.
Tuwasiliane: mhegera@gmail.com
Simu: 0754-826272
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni